Mabomu ya mtawanyo yapigwa marufuku
4 Desemba 2008Lakini watengenezaji wakuu wa silaha kama Marekani,Urusi na China ni miongoni mwa nchi zilizokataa kutia saini.Licha ya nchi hizo na mataifa mengine yenye nguvu za kijeshi kutotia saini, nchi wanachama 18 wa NATO kutoka jumla ya 26 zimetia saini makubaliano yaliyosifiwa kama ni mafanikio ya kiutu.Waziri Mkuu wa Norway Jens Stoltenberg aliekuwa wa kwanza kutia saini alisema ,sasa wanaweza kusema kwa hakika kuwa silaha za mtawanyo zimepigwa marufuku kwa milele.
Hadi hiyo jana nchi 92 kutoka jumla ya mataifa 125 yaliyokuwepo mkutanoni yalitia saini.Ingawa si mataifa yote yanayotazamiwa kutia saini makubaliano hayo,ni matumaini ya maafisa wengi kuwa hadi nchi 100 au zaidi zitakubali kutia saini kabla ya mkutano huo kumalizika leo hii.Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Frank Walter Steinmeier amesema,hatua iliyochukuliwa ni muhimu lakini bado kuna mengi yakutekelezwa.Akatoa wito kwa mataifa mengine pia kufuata mfano wao na kusema:
"Tunachotaka hivi sasa ni kuona makubaliano hayo yakitiwa saini na mataifa yote 100 na silaha hizo kupigwa marufuku kote duniani."
Kwa maoni ya waziri mwenzake wa Uingereza David Milliband,makubaliano ya kweli ni yale yatakayotiwa saini na mataifa yote tu.Lakini Marekani mara nyingine tena juma hili ilikariri msimamo wake kuwa inaelewa madhara ya kiutu yanayosababishwa na mabomu ya mtawanyo lakini haitotia saini makubaliano jumla,kwa sababu yatahatarisha maisha ya wanajeshi wake na ya washirika wake.
Inatathminiwa kuwa tangu miongo kadhaa mabomu ya mtawanyo yameua au yamewafanya vilema hadi watu 100,000 au zaidi.Mabomu hayo hutawanyika sehemu kubwa na si yote yanayoripuka kwa hivyo huendelea kuwa kitisho kwa raia hasa watoto hata baada ya migogoro kumalizika.
Ni matumaini ya wengi kuwa makubaliano yaliyotiwa saini mjini Oslo yatasaidia kuyalaani na kuyapa sifa mbaya zaidi mabomu ya mtawanyo na hivyo makubaliano hayo kuheshimiwa na nchi zisizotia saini pia kama ilivyokuwa katika mwaka 1997 kuhusu mabomu yanayofukiwa ardhini.