1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron afanya mazungumzo na viongozi wa upinzani

21 Juni 2022

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron anakutana kwa mazungumzo na viongozi wa vyama vikuu nchini humo leo Jumanne baada ya muungano wake wa kiliberali kushindwa kupata wingi wa viti katika uchaguzi wa Bunge.

Emmanuel Macron und Christian Jacob
Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa (kulia) akiambatana na kiongozi wa chama cha Les Republicains kabla ya kuanza kwa mazungumzo yao kwenye Ikulu ya Elysee mjini Paris.Picha: Mohammed Badra/AFP /Getty Images

Mikutano hiyo kwenye Ikulu ya Elysee inafanyika baada ya Waziri Mkuu wa Ufaransa Elisabeth Borne kuwasilisha barua yake ya kujiuzulu mapema leo kama sehemu ya utamaduni wa kawaida pindi uchaguzi wa Bunge unapomalizika.

Hata hivyo rais Macron amekataa kujiuzulu kwa mwanasiasa huyo na kuamuru serikali yake ibakie madarakani. Muungano wa kiliberali wa rais Macron wa Ensemble au "Pamoja" ulishinda viti 245 katika uchaguzi wa Bunge wa siku ya Jumapili. Idadi hiyo ni pungufu ya viti 44 vilivyohitajika ili kuuwezesha muungano huo kuwa na wingi wa viti bungeni.

Muungano wa wanasiasa wa mrengo wa shoto wa Nupes umeshinda viti 131 na kuwa upande wa upinzani wenye nguvu ndani ya chombo hicho cha juu cha kufanya maamuzi nchini Ufaransa. Wanasiasa wa mrengo mkali wa kulia wameambulia nafasi 89 ya viti katika bunge hilo la Ufaransa lenye jumla ya viti 577.

Hii leo Jumanne Macron anatazamiwa kukutana na wajumbe wa upande wa upinza ikiwemo rais wa chama cha Republicans Christian Jacob, mkuu wa chma cha kisoshalisti  Olivier Faure na kiongozi wa chama cha mrengo mkali wa kulia Marine Le Pen.

Kuna mikutano mengine kati ya kiongozi huyo na maafisa wengine ambayo haijawekwa wazi. Macron pia amepangiwa kukutana na wawakilishi wa chama chake na washirika wa vuguvugu la kisiasa aliloliunda.

Je, atafanikiwa kutanzua kiwingu kinachoikabili serikali yake? 

Matokeo ya uchaguzi wa Bunge umeiweka serikali ya rais Macron njiapanda.Picha: Eliot Blondet/abaca/picture alliance

Mazungumzo hayo yananuwia kutafuta "njia mwafaka" za kutatua mkwamo uliopo kuhusu hatma ya serikali anayoiongoza. Macron mwenyewe bado hajatoa maoni yake hadharani kuhusu uchaguzi wa bunge.

Chama chake ambacho ndiyo kina wabunge wengi bado kinaweza kuongoza serikali lakini kitalazimika kufikia makubaliano na wabunge wengi kupitisha maamuzi au miswada ya sheria.

Ili kuepusha mkwamo unaoweza kujitokesha siku zinazokuja, chama cha Macron na washirika wake wanajadiliana na wanasiasa wengine ili kuona maeneo wanayoweza kufanya kazi pamoja na kuungana mkono.

Macron alichaguliwa kwa muhula wa pili mnamo mwezi Aprili chini ya ahadi ya kuongeza uwezo wa kifedha wa raia mmoja mmoja nchini Ufaransa, kupunguza kodi na kupandisha umri wa kustaafu kutoka miaka 62 hadi 65.

Baadhi ya wanasiasa wasema wako tayari kuunga mkono baadhi ya sera za Macron

Kiongozi wa chama cha Kisoshalisti Olivier Faure akiwasili Ikulu ya Elysee kwa mazungumzo na rais MacronPicha: Ludovic Marin/AFP/Getty Images

Wakati akielekea kwenye ukumbi wa mikutano kwenye Ikulu ya Elysee, Jacob amesema chama cha Republicans chenye viti 61 kitabakia upande wa upinzani na haitoingia kwenye "makubaliano au muungano" wowote na waliberali wa Macron.

Hata hivyo amesema watakuwa tayari kuunga mkono baadhi ya sera zinazokwenda sambamba na ajenda ya chama chao. Amesema masuala kama mabadiliko ya pensheni ni sehemu ya ajenda wanazopigia upatu sawasawa na chama cha Macron.

Kiongozi wa Wasoshalisti, Olivier Faure aliwaambia waandishi habari kwamba "kuna uwezekano wa kusonga mbele pamoja lakini hatutaunga mkono sera zitakazokwenda kinyume na ahadi tulizowapatia Wafaransa".

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW