1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron aishinikiza Lebanon kuunda haraka serikali mpya

1 Septemba 2020

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amerejea Lebanon, nchi ambayo ipo katikati ya mgogoro usio wa kawaida, kwa ziara ya siku mbili iliyosheheni shughuli nyingi na mazungumzo ya kisiasa yanayolenga kuipa ufumbuzi nchi hiyo

Libanon Präsident Michel Aoun trifft Emmanuel Macron
Picha: picture-alliance/AP Photo/G. Fuentes

Macron alitua jana usiku mjini Beirut lakini mkutano wake wa kwanza haukuwa na waziri mkuu mpya aliyeteuliwa saa chache kabla, wala wanasiasa wanaozozana wa nchi hiyo au wanaharakati wa mashirika ya kijamii. Macron badala yake aliamua kumuona mwanamuziki nambari moja wa kike nchini Lebanon, Fairouz, ambaye ni alama ya kitaifa na mmoja wa vigogo wa nadra sana nchini Lebanon wanaopendwa na kuheshimiwa kote nchini humo. Mwanamuziki huyo maarufu katika ulimwengu wa Kiarabu, sasa ana umri wa miaka 86 na hajaonekana hadharani katika miaka ya karibuni. Mkutano na Fairouz ni ishara ya kibinafsi ya Macron.

Mustapha Adib, waziri mkuu mteulePicha: Reuters/M. Azakir

Kisha akakutana na waziri mkuu wa zamani Saad Hariri katika makazi ya balozi wa Ufaransa. Akizungumza katika uwanja wa ndege wa Beirut, Macron alitoa wito wa kuundwa haraka serikali mpya ya Lebanon kufuatia kuteuliwa kwa waziri mkuu mpya." Nimeona mchakato umeanza katika saa chache zilizopita ambao umewezesha kupatikana kwa waziri mkuu. Sio jukumu langu kumuidhinisha au kumbariki - ni uhuru wa Walebanon ambao ndio suala la msingi hapa - Lakini uhakikishe kuwa serikali yenye lengo inaundwa haraka iwezekanavyo ili kutekeleza mageuzi ambayo tunatambua kuwa yanahitajika kutoa huduma kwa Walebanon." Amesema Macron  

Macron aliwasili saa chache tu baada ya viongozi kumteuwa Mustapha Adib, mwanadiplomasia mwenye umri wa miaka 48, kuwa waziri mkuu mpya na mwenye jukumu la kuukabili mgogoro mkubwa wa nchi hiyo wa kisiasa na kiuchumi.

Rais Michel Aoun mwenye umri wa miaka 85 na mshirika wake wa kisiasa, kiiongozi wa Hezbollah Hassan Nasrallah, wameeleza kuwa tayari kubadilisha namna Lebanon inavyoongozwa. Hata amependekeza kutangazwa kwa taifa lisiloongozwa kwa misingi ya kidini. Chini ya mfumo wa sasa wa kisiasa wa Lebanon, waziri mkuu lazima atoke katika madhehebu ya Sunni, urais unaachiwa Mkristo na wadhifa wa spika wa bunge unatengewa madhehebu ya Shia.

Macron alikuwa kiongozi wa kwanza wa kigeni kuitembelea Lebanon, siku mbili baada ya mlipuko wa Beirut uliowauwa watu 188 na kuwajeruhi maelfu ya wengine. Aliahidi kurejea Septemba mosi kushiriki katika matukio ya kuadhinimisha miaka 100 ya uhuru wa Lebanon kutoka kwa Ufaransa.

reuters, afp, ap

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW