1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron amfungulia kesi mshawishi wa mtandaoni Candace Owens

24 Julai 2025

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron na mke wake Brigitte wamefungua mashtaka dhidi ya Candace Owens, mshawishi maarufu wa mitandao ya kijamii nchini Marekani anayeegemea mrengo wa kulia.

Marekani 2024 | Candace Owens mshawishi wa mitandaoni
Candace Owens amethibitisha kufunguliwa kesi kwa tuhuma ya kutoa "kauli ya uongo ili kujinufaisha kupitia jukwaa lake binafsi, kujitafutia umaarufu, na kupata fedha."Picha: Dominic Gwinn/ZUMA/picture alliance

Kesi hiyo inahusu kashfa ambayo Owens alidai kwamba mke wa rais huyo alizaliwa mwanaume.

Owens alitoa madai hayo, miongoni mwa mengine dhidi ya wanandoa hao wa Ikulu ya Ufaransa, kupitia mtandao wa X na katika kipindi chake mnamo Machi 2024.

Kesi hiyo ya kisheria, ambayo Owens mwenyewe alithibitisha kupitia video ya YouTube, inamshutumu kwa kutoa "kauli hii ya uongo ili kujinufaisha kupitia jukwaa lake binafsi, kujitafutia umaarufu, na kupata fedha."

Miongoni mwa madai hayo ni kwamba Brigitte na Emmanuel Macron ni ndugu wa damu, na kwamba Emmanuel Macron alipata urais kwa msaada wa mpango maalum wa shirika la kijasusi la Marekani (CIA).

Kesi hiyo inasema kuwa Macron na mkewe wamekuwa wahanga wa "kampeni ya kuaibishwa duniani kote na isiyo na msingi wowote." Owens amekuwa akizua utata mara kadhaa kutokana na misimamo yake. Mnamo 2024, serikali ya Australia ilimkatalia kuingia nchini humo, ikitaja kusambaza kwake madai ya uongo kuhusu mauwaji ya Holocaust na Waislamu.