1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron kusimamia mkutano wa wafadhili kwa ajili ya Lebanon

Sekione Kitojo
9 Agosti 2020

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron leo Jumapili(09.08.2020)atakuwa mwenyeji wa mkutano unaoungwa mkono na Umoja wa Mataifa na atashiriki rais Donald Trump pamoja na wawakilishi wengine kutafuta msaada kwa Lebanon.

Belgien PK Abschluss EU-Gipfel
Picha: Reuters/J. Thys

Macron siku  ya  Alhamisi  alikuwa  kiongozi  wa  kwanza  duniani kufanya  ziara  mjini  Beirut  baada  ya  mripuko  uliotokea  siku  ya Jumanne na  kuwaonya viongozi wa Lebanon  kuwa  wakati  msaada wa  kimataifa  utapatikana mageuzi  makubwa  yanahitajika  kutatua matatizo  ya  nchi  hiyo.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron akiwa mjini BeirutPicha: picture-alliance/dpa/AP/T. Camus

Mripuko  huo katika  bandari  ya  mjini  Beirut, ambao lawama zinaelekezwa  katika shehena  kubwa ya  kemikali  ya  amonia naitreti  iliyohifadhiwa na kuachwa kuoza kwa miaka  kadhaa  katika bohari, uliharibu eneo lote la  kitongoji. Mripuko  huo  umeongeza hasira  ya  Walebanon wengi  dhidi  ya  tabaka linaloongoza  nchi hiyo linalodaiwa kujitumbukiza  katika  ufisadi na rushwa pamoja na upendeleo.

Macron anatarajia  kwamba ahadi zitakazotolewa  katika  mkutano huo  kwa  njia  ya  vidio, utakaoanza  mchana  leo, utakuwa mchango thabiti na  fedha  hizo  zitatumika kwa  uwazi  na  kwa  lengo lililokusudiwa.

Akizungumza mjini  Beirut  baada  ya  ziara  yake  siku  ya  Alhamis, Macron  alisema  kuwa  mkutano  huo una lengo  la  kutafuta  fedha kutoka  mataifa  ya  Ulaya , Marekani na  mataifa  ya  eneo  hilo linaloizunguka  Lebanon kwa ajili  ya  madawa, huduma, chakula, na kuwapa  makaazi  watu  walioathirika.

Rais Donald Trump wa MarekaniPicha: picture-alliance/AP/T. Dejak

Haja ya mageuzi Lebanon 

"Pia  tutaweka uongozi wa wazi na sahihi  ili misaada  hii  yote , iwapo inatoka  Ufaransa ama  ya kimataifa, iweze kwenda  moja  kwa moja  kwa  watu, katika  asasi  za  kijamii na  timu katika  maeneo ambayo  yana  uhitaji, bila ya  uwezekano wa  kuhodhi  ama kupelekwa  mahali  ambako hakustahili," alisema.

Amesema  kwamba  haja ya mageuzi  makubwa  yanamaana "muda umewadia sasa wa uwajibikaji kwa Lebanon ya leo  na  viongozi wake" ambao wanahitaji " makubaliano  mapya  na  watu  wa Lebanon katika  wiki zijazo."

Waziri mkuu Hassan Diab  amesema  siku  ya  Jumamosi kuwa ataitisha  uchaguzi  wa mapema.

Waziri mkuu wa Lebanon Hassan Diab Picha: AFP/DALATI AND NOHRA

Trump  akithibitisha  kushiriki kwake katika  mkutano  huo, aliandika katika  ukurasa wa Twitter kuwa "kila mmoja  anataka kusaidia!"

Chanzo  katika  ofisi  ya  rais  ya  Ufaransa ambacho  hakikutaka kutajwa  jina , kimesema  kuwa  Umoja  wa  Ulaya, Uingereza, China, Urusi, Jordan na  Misri zitawakilishwa, licha  ya  kuwa haikufahamika  mara  moja katika  ngazi gani. Israel, ambayo Lebanon  haina uhusiano  wa kidiplomasia nayo, haitarajiwi kushiriki.

Mataifa  muhimu  ya  Kirabu katika  eneo  la  ghuba, ikiwa  ni  pamoja na  saudi Arabia, Qatar na  Umoja  wa  falme  za  Kiarabu yanatarajiwa  kushiriki  lakini  Iran, ambayo  ina  ushawishi  mkubwa katika  Lebanon  kupitia kundi la  Kishia  la  Hezbollah, haijaonesha nia  ya kushiriki, afisa  huyo  alisema.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW