Maduro afikishwa katika Mahakama ya New York
5 Januari 2026
Maduro na mkewe wamefikishwa mbele ya jaji Alvin Hellerstein wa Mahakama ya Shirikisho ya Manhattan mjini New York chini ya ulinzi mkali, hii ikiwa ni hatua muhimu ambayo huenda ikaanzisha mvutano mrefu wa kisheria wa kufahamu ikiwa Maduro na mkewe wanaweza kushtakiwa nchini Marekani.
Mawakili wa Nicolas Maduro wamesema watapinga kwanza uhalali wa kukamatwa kwake, wakisema mteja wao anayo kinga ya kushtakiwa kwa kuwa ni mkuu wa taifa huru la kigeni. Madai ambayo bila shaka yatatupiliwa mbali na Marekani ambayo haimtambui Maduro kama kiongozi halali wa Venezuela.
Maduro, mkewe, mwanawe na watu wengine watatu, wanatuhumiwa kwa kushirikiana na magenge ya ulanguzi wa dawa za kulevya wakirahisisha usafirishaji wa maelfu ya tani za kokeini nchini Marekani. Ikiwa watakutwa na hatia, wanaweza kukabiliwa na kifungo cha maisha jela.
Hali ya wasiwasi yashuhudiwa kimataifa
Rais wa mpito Delcy Rodríguez aliyehudumu kama makamu wa rais tangu mwaka 2018 na aliyechukua nafasi ya mshirika wake Maduro, sasa ametangaza "kushirikiana" na utawala wa Trump katika kile kinachotazamwa kuwa ni mabadiliko makubwa katika uhusiano kati ya Washington na Caracas.
Hata hivyo wachambuzi wanasema azma ya Marekani ya kutaka kuhodhi sekta ya mafuta ya Venezuela, itakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na hatua zitakazochukuliwa na Urusi na China ambazo hazitokubali kuona uwekezaji wao wa mabilioni ya dola katika sekta ya mafuta huko Venezuela ukipotea.
Katika hatua nyingine, ukosoaji wa kimataifa umeendelea kufuatia kitendo cha kutekwa kwa Maduro na makomandoo wa Marekani, huku baadhi ya mataifa yakishindwa kuwa na msimamo wa wazi juu ya tukio hilo.
Ujerumani kupitia Waziri wake wa Mambo ya Nje Johann Wadephul ametoa wito wa kurejesha hali ya utulivu wa kisiasa huko Venezuela na kusisitiza kuwa linalopaswa kuzingatiwa kwa sasa ni kutafuta namna ya kusonga mbele kwa kuzingatia sheria za kimataifa, demokrasia na kujitawala kwa watu wa Venezuela.
" Watu wa nchi hiyo wanaweza kujiamulia mustakabali wa nchi yao na wanapaswa kupewa fursa ya kufanya hivyo haraka iwezekanavyo kulingana na sheria na kanuni za kimataifa. Tutatoa mchango wetu katika mchakato huu mara tu utakapoanza, ” aliongeza waziri Wadephul.
Tukio la Marekani kumteka Maduro limezusha hali ya wasiwasi kwa mataifa mengine ambayo yamekuwa na msuguano na Trump. Rais wa Colombia Gustavo Petro amesema hivi leo kuwa yuko tayari "kuchukua tena silaha" ili kuilinda nchi yake, baada ya Trump kusema mwishoni mwa wiki iliyopita kwamba Petro anapaswa "kuwa makini" huku akimtaja rais huyo wa Colombia kuwa ni " mgonjwa wa akili anayezalisha kokeini na kuiuza nchini Marekani."
(Vyanzo: Mashirika)