MAGAZETI YA UJERUMANI
4 Agosti 2011Basi tutaanza na gazeti la DER NEUE TAG linalosema:
"Rais wa zamani wa Misri alie na miaka 83 amepelekwa mahakamani, akiwa katika kitanda cha hospitali na amesema kuwa yeye hana hatia. Lakini hayo yote hayabadili ukweli kuwa hata madikteta, wanapaswa kuwajibika kwa vitendo vyao. Jukumu la kuwajibisha wale waliohusika na mauaji ya Yugoslavia ya zamani na nchini Rwanda, limebebwa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa kivita. Wamisri wanaweza kutekeleza jukumu hilo, bila ya msaada wa mahakama hiyo ya kimataifa. Vyo vyote itakavyoamuliwa kwa jina la umma, mradi isiwe adhabu ya kifo. Mapinduzi ya kidemokrasia wala hayastahili hilo."
Gazeti la DRESDNER NEUESTE NACHRICHTEN likiendelea na mada hiyo hiyo linasema:
"Kesi ya rais wa zamani wa Misri, Hosni Mubarak haitokuwa rahisi. Kwani huenda ikawa shida kuthibitisha iwapo baba huyo wa taifa, alietawala kwa miaka 30, kweli alitoa amri ya kuwaua waandamanaji. Na kuhusu mashtaka ya kutumia vibaya madaraka na kujitajirisha kwa njia zisizo halali, hata waziri wa zamani wa ulinzi na mkuu wa zamani wa idara ya upelelezi wanaweza kutuhumiwa makosa hayo. Lakini wote wawili, wapo katika serikali ya mpito. Kwa hivyo, itategemea iwapo mahakama na viongozi wapya mjini Cairo, wanataka kutoa funzo au wanataka upatanisho."
Janga la njaa katika Pembe ya Afrika ni mada nyingine inayoendelea kushughulikiwa na wahariri wa magazeti ya Ujerumani. DIE ZEIT linaeleza hivi:
"Hakuna fedha za kinga kwani msaada wa aina hiyo hautogonga vichwa vya habari na hukana harakati za kuokoa wala picha za kusikitisha. Kunakosekana jukwaa la mashindano ambako wafadhili wa kimataifa hupata fursa ya kujipigia debe. Hiyo ni sababu ya misaada kukawia kufika Afrika Mashariki.
Tukigeukia mada nyingine, gazeti la FLENSBURGER TAGEBLATT limeshughulikia ripoti mpya iliyotolewa na ofisi kuu ya takwimu ya Ujerumani kuhusu idadi ya watoto nchini humu. Limeandika:
"Ujerumani ni miongoni mwa nchi tajiri kabisa duniani, lakini ni masikini katika mambo matatu: kwanza ni kuwa licha ya tarakimu kuonyesha pato kubwa kwa kila mtu nchini, watoto wanazidi kuishi katika hali ya umasikini, hivi sasa ni watoto milioni mbili. Pili ni kwamba idadi ya watoto na vijana walio chini ya miaka 18, inazidi kupungua kwa hivyo hata furaha ya maisha hupungua. Tatu, wanasiasa hawakufanikiwa kuleta mazingira ya kuvutia watu kuwa na familia."
Mwandishi: Martin,Prema/dpae
Mhariri:Abdul-Rahman