1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magufuli: Buldoza aliepuuza Covid na demokrasia

18 Machi 2021

Rais John Magufuli aliwahi kusifikiwa kutokana na mtindo wake wa kutovumilia uzembe na ubadhirifu, lakini hatua yake ya kuanza kutawala kwa mabavu ilikandamiza demokrasia na akaruhusu ugonjwa wa Covid-19 kuenea.

Tansania Wahlen | Präsident John Magufuli
Picha: Ericky Boniphace/AFP

Magufuli aliingia madarakani kama mtu wa watu anaepiga vita rushwa, lakini kwa waangalizi wengi, namna alivyoshughulikia janga la Covid-19 iliumulika sana mfumo wake wa uongozi.

Mkristo huyo mwenye imani alidai kuwa sala zimeikoa nchi kutokana na Covid-19, akitilia maanani zaidi maombi kuliko kuvaa barakoa na kuzuwia kutangazwa kwa takwimu za maambukizi ya virusi vya corona, na alikataa kata kata kutekelezwa hatua zozote za kudhibiti maambukizi ya Covid-19.

Hata hivyo, kufikia mwezi uliopita, visa vilikuwa vinaongezeka kiasi kwamba, Kanisa, shule and taasisi nyingine za umma zilitoa maonyo ya wazi kuhusu kusambaa kwa virusi vya corona.

Soma pia: Magufuli afariki dunia akiwa na umri wa miaka 61

Kisha, makamu wa kwanza wa rais wa Zanzibar, Seif Sharif Hamad, akafariki baada ya chama chake cha siasa kukiri kwamba alikuwa na virusi vya corona. Kufuatia shinikizo kubwa, Magufuli alionekana kukubali kwamba virusi hivyo vipo.

Magufuli akiwa na aliekuwa makamu wa kwanza wa rais wa Zanzibar, Maalimu Seif Sharif Hamad, enzi za uhai wao.Picha: Tanzania Presidential office

"Wakati maradhi haya ya kupumua yalipozuka mwaka uliopita, tulishinda kwa sababu tulimtanguliza Mungu na kuchukuwa hatua nyingine. Nina uhakika tutashinda tena ikiwa tutafanya hivyo mara hii", alisema Magufuli na kuongeza kuwa magonjwa haya yakiwemo ya kupumua yapo, na yameuwa watu zaidi katika mataifa mengine... "tutakufa, iwe kwa ugonjwa huu au malaria au mwingine. Tumrudie Mungu, pengine tulikosea mahala", alisema Magufuli.

Kiongozi mwenye maamuzi makali

Magufuli alichaguliwa kwa mara ya kwanza mwaka 2015 kwa ahadi kali ya kupambana na rushwa, jambo ambalo lilimfanya apendwe na watu waliochoshwa na kashfa za rushwa.

Alichukuwa maamuzi makali ya haraka yaliowafurahishwa wananchi, kama vile kufuta sherehe za matumizi makubwa za uhuru na badala yake kutumia fedha zake kukarabati barabara na pia alipiga marufuku safari za nje za maafisa wa serikali.

Soma pia: Maoni: Magufuli, rais aliyependwa kama alivyochukiwa

Matukio kadhaa yaliopamba vichwa yalimshuhudia akijitokeza binafsi kuwahoji watumishi wa umma kwa nini hawako kwenye meza zao kazini, huku katika kisa kimoja, maafisa waliwekwa jela kwa muda mfupi kwa kuchelewa.

Hata hivyo tabia yake ya kukiuka utaratibu na kuchukuwa hatua za pupa iliwashtua washirika wa kimataifa, kuhusiana na kuminywa kwa demokrasia katika moja ya mataifa yenye utulivu zaidi Afrika Mashariki.

Magufuli akiwa rais mstafu Benjamin Mkapa, amabye pia alifariki dunia katikati mwaka 2020.Picha: DW/Said Khamis

Kuchaguliwa kwake kwa muhula wa pili Oktoba mwaka uliopita kulipingwa na wapinzania na kutiliwa mashaka na wanadiplomasia. Uchaguzi huo ulifanyika chini ya mazingira ya vitisho kufuatia ukandamizaji dhidi ya upinzani na kuzuwiwa kwa vyombo vya habari na timu za waangalizi.

Chini ya utawala wake, mkururo wa sheria kadhaa kali zilipitishwa huku kamatakamta ya waandishi habari, wanaharakati na wanasiasa wa upinzani zikiongezeka, na wanasiasa kadhaa wa upinzani waliuawa.

Soma pia: 

Magufuli aliamuru wanafunzi wa kike waliobeba mimba na kujifungua wafukuzwe shuleni, huku mashirika ya haki za binadamu yakilaani ukandamizaji dhidi ya watu wanaofanya mapenzi ya jinsia moja chini ya utawala wake.

Rais anaejua ni maana ya kuwa maskini

Wafuasi wake wanamsifu kwa kupiga vita rushwa, kampeni kubwa ya ujenzi wa miundombinu pamoja na kuifanyia mageuzi sekta ya madini, ambayo yalipekea kujadiliwa upya kwa mikataba na kampuni za kigeni ili kuboresha mgao wa nchi hiyo katika rasilimali zake.

Alipanua elimu ya bure, kuongeza usambazaji wa huduma ya umeme vijijini na kuanzisha ujenzi wa njia muhimu ya reli na bwawa kubwa la umeme ambalo litaongeza uzalishaji nchini humo..
Soma pia:Yuko wapi Rais Magufuli? 

Juhudi za Rais Magufuli, za kuimarisha Miundombinu Tanzania

02:21

This browser does not support the video element.

Magufuli alizaliwa katika wilaya ya kaskazini-magharibi mwa Tanzania ya Chato, kwenye fukwe za Ziwa Victoria, ambako alikulia akichunga ng'ombe na kuuza maziwa na samaki ili kuisadia familia yake. "Najua nini maana ya kuwa maskini," alikuwa akinukuliwa akisema mara kwa mara.

Alitunukiwa shahada ya uzamivu katika kemia kutoka chuo kikuu cha Dar es Salaam na pia alisoma katika chuo kikuu cha Salford nchini Uingereza. Magufuli alikuwa mwanachama wa chama tawala, chama cha mapinduzi CCM, ambacho kimekuwa madarakani tangu nchi hiyo ilipopata uhuru kutoka kwa Uingereza mwanzoni mwa miaka ya 1960.

Akiwa mbunge tangu 1995, ameshikilia nyadhifa kadhaa za uwaziri, ukiwemo wa mifugo, uvuvi na ujenzi, ambako alijipatia jina la Buldoza. Ameacha mke na watoto watano. Sote ni wa Mwenyezi Mungu, na kwake tutarejea.

Chanzo: Mashirika

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW