1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama TZ, imekubali ombi la kupinga Tume ya Samia

18 Desemba 2025

Mahakama Kuu ya Tanzania, imeyakubali maombi yaliyoletwa na walalamikaji kupinga uhalali wa Tume iliyoundwa na Rais wa Tanzania, kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani wakati wa Uchaguzi Mkuu wa Tanzania, Oktoba 29.

Tanzania 2025 | Mohamed Othman Chande
Mkuu wa Tume iliyoteuliwa na Samia kuchunguza ghasia za baada ya uchaguzi, Jaji Mtaafu Mohammed Othman Chande Picha: Commission of Inquiry Tanzania

Hayo yameelezwa na wakili wa waliofungua maombi hayo, Hekima Mwasipu, baada ya shauri hilo kusikilizwa kwa mara ya pili kwa ajili ya kupokea uamuzi wa mahakama.

Wakili Mwasipu amesema watafungua kesi hiyo kwa hati ya dharura, na kwamba watawasilisha tena maombi mahakamani kuomba tume hiyo izuiliwe kwa muda kufanya kazi hadi hapo kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.

Katika uamuzi wake uliosomwa na Naibu Msajili wa Mahakama Hussein Mushi, kwa niaba ya Jaji Hussein Salum Mtembwa aliyekuwa anasikiliza maombi hayo, Mahakama imesemawaruhusu wafungua maombi, kufungua kesi msingi ndani ya siku 14 kuanzia leo isipokuwa, mahakama imesema tume itaendelea na kazi yake hapo uamuzi utakapotolewa.

Tume ya Othaman Chande imepewa jukumu la kuchunguza yaliyotokea katika ghasia za baada ya uchaguzi wa Oktoba 29, uliomrejesha madarakani Rais Samia Suluhu Hassan.Picha: AP Photo/picture alliance

Itakumbukwa kuwa, Novemba 18 Rais Samia Suluhu Hassan aliunda tume ya watu wanane inayoongozwa na Jaji Mstaafu Mohamed Othman Chande na wajumbe wengine saba.

Hilo liliwainua Rosemary  Mwakitwange na wenzake ambao ni wanaharakati wa haki za binaadamu, kuipinga tume hiyo mahakamani wakidai kuwa imeundwa kinyume cha sheria na haina nia njema.

Shauri hilo liliendeshwa kwa njia ya mtandao ambapo upande wa serikali, uliwakilishwa na mjibu maombi ambaye ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali na wajumbe wote wanane wa tume hiyo wakiongozwa na Jaji Chande ulikuwa unakilishwa na Wakili Mwandamizi wa Serikali Daniel Nyakia, pamoja na Wakili wa Serikali Erigh Rumisha.

Upande wa waleta maombi Rosemary Mwakitwange, Edward Heche na Deogratias Mahinyila, uliwakilishwa na Wakili Hekima Mwasipu

 

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW