1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Majaji Sudan, Marekani walaani ukandamizaji wa maandamano

Hawa Bihoga
21 Januari 2022

Mkuu wa mahakama Sudan na majaji wamelaani vurugu dhidi ya waandanamanaji, katika tamko la nadra Alhamisi, huku Marekani ikisema itachukua hatua dhidi ya wanaozuwia juhudi za kutatua mzozo wa kisiasa wa Sudan.

Sudan Khartum | Protest gegen die Machtübernahme durch das Militär
Picha: Ashraf Shazly/AFP/Getty Images

Raia wasiopungua 72 wamekufa nchini Sudan na zaidi ya 2,000 wamejeruhiwa katika ukandamizaji wa vikosi vya usalama dhidi ya maandamano ya mara kwa mara, tangu jeshi lilipotwaa madaraka Oktaba 25, kwa mujibu wa madaktari wanaoelemea upande wa vuguvugu la maandamano.

Wakikasirishwa na vifo saba vya raia mapema wiki hii, waandamanaji waliingia mitaani tena siku ya Alhamisi mashariki mwa Khartoum na maeneo mengine ya Sudan.

Viongozi wa kijeshi wamesema haki ya kuandamana kwa amani inalindwa na wameanzisha uchunguzi katika umuagaji damu uliotokea. Vurugu hizo zimeongeza mkwamo kati ya makundi yanayopigania demokrasia na uongozi wa kijeshi.

Soma pia: Waandamanaji 7 wauawa na vikosi vya usalama Sudan

Katika taarifa siku ya Alhamisi, baraza tawala la Sudan lilisisitiza haja ya majadiliano ya kitaifa, baraza la mawaziri ambao ni wataalamu, na marekebisho katika waraka wa katiba ya mpito iliojadiliwa baada ya kuondolewa kwa kiongozi wa zamani Omar al-Bshir katika mapinduzi ya 2019.

Waandamanaji mjini Khartoum wakipinga mapinduzi ya kijeshi ya Oktoba 25, 2020.Picha: Ashraf Shazly/AFP/Getty Images

Waraka huo uliunda msingi wa mpango wa kugawana madaraka kati ya jeshi na raia, ambao ulisitishwa baada ya mapinduzi.

Baada ya kushindwa kwa juhudi za waziri mkuu wa zamani Abdalla Hamdok kuokoa baadhi ya udhibiti wa kiraia kufuatia mapinduzi, Umoja wa Mataifa umekuwa ukijaribu kuwezesha mazungumzo kati ya makundi yanayokinzana.

Msaada uliozuwiwa

Mapinduzi hayo yalikosolewa na mataifa ya magharibi ambayo kwa sehemu yalizuwia msaada unaohitajika vibaya wa kiuchumi kwa Sudan.

Msaada huo ungerejeshwa tu baada ya kusitisha vurugu na kurejeshwa kwa serikali ya kiraia, naibu waziri wa mambo ya nje wa Marekani anayehusika na masuala ya Afrika Molly Phee aliyezuru Sudan, na mjumbe maalumu mpya David Satterfield walisema.

Soma pia:Madaktari Sudan waandamana kupinga mashambulizi dhidi yao 

Wakilaani matumizi ya nguvu dhidi ya waandamanaji, waliweka wazi kwamba Marekani itazingatia hatua za kuwawajibisha wale wanaohusika na kushindwa kusonga mbele kwa kipindi cha mpito na kukomeshwa kwa vurugu, ilisema taarifa ya Marekani.

Taarifa kutoka kwa majaji 55 wa Sudan kwenda kwa mkuu wa idara ya mahakama ilisema viongozi wa kijeshi wamekiuka makubaliano na mikataba tangu mapinduzi ya Oktoba 25, kwa kutekeleza ukiukaji wa kikatili dhidi ya waandamaji waio na ulinzi. Walitoa wito wa kukomesha vurugu na kufanya uchunguzi wa uhalifu.

Mkuu wa utawala wa kijeshi wa Sudan Jenerali Abdle Fattah al-Burhan.Picha: /AP/dpa/picture alliance

Katika jibu lake, mkuu wa idara ya mahakama alisema katika taarifa iliyokuwa na jina lake na majaji wa nchi hiyo kwamba baraza huru la taifa linapaswa kufanya chini juu, kuzuwia ukiukaji wa dhahiri dhidi ya watoto wa taifa lao, ambao hawawezi kuunyamazia.

"Sisi katika mahakama tunasisitiza kwamba hatutasita kuchukua hatua tulizo nazo kulinda maisha na haki za kikatiba za raia," ilisema taarifa hiyo.

Katika hatua tofauti, zaidi ya waendesha mashtaka 100 walitangaza kwamba wangesitisha kazi kuanzia siku ya Alhamisi ili kutoa wito kwa vikosi vya usalama kuacha ukiukaji na kuondoa sheria ya hali ya hatari. Walisema waendesha mashtaka wameshindwa kutekeleza majukumu yao ya kisheria ya kusindikiza polisi kwenye maandamano na kubaini matumizi yanakubaliwa ya nguvu.

Soma pia: Mjumbe wa Marekani kufanya ziara Saudi Arabia, Sudan na Ethiopia

Siyo jambo la kawaida kwa majaji wa Sudan na waendesha mashtaka kutoa matamko ya umma kuhusu tabia ya vikosi vya usalama.

Alipoulizwa kutoa kauli, kaimu waziri wa mawasiliano Nasreldin Ahmed alisema kiongozi wa kijeshi Abdel Fattah al-Burhan alikuwa ameamuru uchunguzi juu ya vifo vya waandamanaji siku ya Jumatatu, na kwamba tayari ucunguzi ulikuwa umeanza.

Waziri Mkuu wa kiraia aliejiuzulu Abdalla HamdokPicha: AFP

Mawaziri wapya

Wakati huo huo, kiongozi huyo wa kijeshi aliteuwa mawaziri 15 katika serikali, ilisema taarifa kutoka Baraza huru la utawala siku ya Alhamisi. Uteuzi wa Burhan unawajumlisha Ali Sadek alietuliwa kushika wadhifa wa waziri wa mambo ya nje, na Mohammed Abdallah Mahmoud kwa nafasi ya waziri wa nishati.

Mapema Alhamisi, Baraza hili lilikubaliana na ujumbe wa Marekani juu ya kuundwa kwa serikali huru ya kitaifa ya watalaama na kunazisha mdahalo mpana wa kitaifa ili kutatua mzozo wa sasa wa kisiasa.

Chanzo: RTRE

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW