1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Majeshi ya Mali yawafurusha waasi kwa msaada wa Ufaransa

12 Januari 2013

Majeshi ya Mali yamewafurusha waasi wa Kiislamu kutoka mji muhimu katika eneo la kati nchini humo,baada ya Ufaransa kuingilia kati jana Ijumaa(11.01.2013)kwa mashambulio ya anga na kuzuwia waasi hao kusonga mbele.

Bewaffnete Tuareg-Kämpfer auf ihrem Pick-up; Nordmali am 15.02.2012. Nach dem Sturz von Gaddafi in Libyen ist der Bürgerkrieg in Mali zwischen Tuareg-Rebellen und den Regierungstruppen eskaliert. Fast 130.000 Menschen befinden sich laut UN auf der Flucht. Rund die Hälfte flüchtete ins Ausland, die andere Hälfte sind Binnenflüchtlinge. Durch die bestehende Nahrungsmittelknappheit in der Sahelzone droht eine humanitäre Katastrophe.
Majeshi ya MaliPicha: picture-alliance/Ferhat Bouda

Waasi wa nchi hiyo wanadhibiti eneo la kaskazini hadi sasa.

Serikali za mataifa ya magharibi , hususan mkoloni wa zamani wa nchi hiyo ufaransa , imeeleza hali ya tahadhari baada ya muungano wa waasi hao wenye mafungamano na kundi la al-Qaeda kuukamata mji wa Konna siku ya Alhamis (10.01.2013), ikiwa ni njia ya kuingilia katika mji mkuu Bamako, kilometa 600 kusini mwa nchi hiyo.

Ufaransa haitakaa kimya

Rais Francois Hollande amesema kuwa Ufaransa haitakaa kimya na kuwaacha waasi wakisonga mbele kuelekea upande wa kusini.

Rais wa Ufaransa Francois HollandePicha: Reuters

Ufaransa imekuwa ikionya mara nyingi kuwa wapiganaji hao wa Kiislamu kulikamata eneo la kaskazini mwezi Aprili kunawapa kituo cha kuweza kushambulia nchi jirani za Afrika pamoja na Ulaya.

"Tunakabiliwa na mashambulizi ambayo yanatishia kuwapo kwa Mali, Ufaransa haiwezi kukubali hali hii, " Hollande, ambaye hivi karibuni ameahidi kuwa Ufaransa haitaingilia katika masuala ya mataifa ya Afrika, amesema katika hotuba yake ya mwaka mpya kwa wanadiplomasia na waandishi wa habari.

Rais huyo amesema kuwa maazimio ya baraza la usalama la umoja wa mataifa, ambayo mwezi Desemba yametoa kibali kwa jeshi la Afrika kuingilia kati mzozo wa Mali, yana maana kuwa Ufaransa inafanya hivyo kwa mujibu wa sheria za kimataifa.

Operesheni ya jeshi la Ufaransa ya kuunga mkono jeshi la serikali ya Mali dhidi ya waasi wa Kiislamu, "itafanyika kwa muda wote itakapohitajika," balozi wa Ufaransa katika umoja wa mataifa , Gerard Araud, ameandika katika barua iliyotumwa kwa baraza la usalama la umoja wa mataifa, ambayo imepatikana na shirika la habari la Reuters.

Balozi wa Ufaransa katika umoja wa mataifa Gerard AraudPicha: AP

Mjini Washington , afisa wa Marekani ameliambia shirika hilo la habari kuwa wizara ya ulinzi ya nchi hiyo inapima uwezekano wa kuchukua hatua nchini Mali, ikiwa ni pamoja na kusaidia kutoa taarifa za ujasusi kwa ufaransa pamoja na msaada wa kimbinu.

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ufaransa Laurent Fabius amethibitisha kuwa Ufaransa imefanya mashambulio ya anga dhidi ya waasi kuwazuwia kukamata nchi yote ya Mali. Alikataa kufichua taarifa zaidi, kama vile iwapo majeshi ya Ufaransa yako katika ardhi ya Mali.

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ufaransa Laurent FabiusPicha: AP

Waasi wafurushwa

Kuingilia kati kwa Ufaransa haraka kumebadilisha uwiano wa nguvu za kijeshi, ambapo majeshi ya Mali haraka yaliingia tena katika mji wa Konna, kwa mujibu wa wakaazi wa eneo hilo.

Wanajeshi wa MaliPicha: Habibou Kouyate/AFP/GettyImages

Majeshi ya Mali yameurejesha katika udhibiti wake mji wa Konna kwa msaada wa majeshi ya washirika wetu. Tuko katika mji huo hivi sasa, "Luteni kanali Diaran Kone ameliambia shirika la habari la Reuters, na kuongeza kuwa jeshi hilo linafanya operesheni ya safisha safisha kuwaondoa kabisa wapiganaji wa Kiislamu katika eneo hilo.

Mwandishi : Sekione Kitojo / rtre

Mhariri: Iddi Ssessanga

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW