1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Majirani wa Zimbabwe wabakia kimya

C.Stäcker - (P.Martin)10 Desemba 2008

Zimbabwe inazama lakini Rais Robert Mugabe anaendelea kubakia madarakani.Kwa sehemu fulani,hiyo ni kwa sababu majirani wa Zimbabwe wamekaa kimya kinyume na jamii za kiraia zinazopaza sauti.

Zimbabwean President Robert Mugabe attends the Southern African Development Community (SADC) Extraordinary Summit of Heads of State and Government at the Sandton Convention Centre in Johannesburg, South Africa, 09 November 2008. The ongoing political crisis in Zimbabwe as well as the conflict in the eastern Democratic Republic of Congo (DRC) are on the agenda for the talks scheduled for one day. EPA/JON HRUSA +++(c) dpa - Bildfunk+++
Rais wa Zimbabwe Robert Mugabe.Picha: picture-alliance/ dpa

Wazimbawe walio uhamishoni na jumuiya za wafanya kazi kusini mwa Afrika,wana msimamo mmoja tu yaani Robert Mugabe lazima aondoke madarakani,kwani yeye ndio alieitumbukiza Zimbabwe jangani.Akiendelea kushika wadhifa muhimu serikalini hakuna kitakachosuluhishwa kisiasa wala kiuchumi.Kwa maoni ya raia hao mizozo ya njaa na afya haiwezi kusuluhishwa ikiwa Mugabe atabakia madarakani.

Lakini wao si peke yao kuamini hivyo,kwani sasa hata baadhi ya viongozi wa Kiafrika katika duru za kidiplomasia wameanza kujitenga na mkongwe wa vita vya ukombozi wa Afrika Robert Mugabe.Na hasa ni viongozi wa kizazi kijana kama Waziri Mkuu wa Kenya Raila Odinga na Rais Ian Khama wa Botswana wanaothubutu kuzungumza wazi wazi na kutoa mwito wa kumtaka Rais Mugabe mwenye miaka 84 kuondoka madarakani.Kizazi kingine ndio kimebakia kimya na chini chini huunga mkono msimamo wa Mugabe dhidi ya nchi za Magharibi.Kwa mfano miezi michache iliyopita, Mugabe alipigiwa makofi alipohudhuria mkutano wa viongozi wa Kiafrika. Lakini kiongozi huyo anaposhambuliwa,hakosi la kujibu kama alivyofanya Julai mwaka huu.Mugabe alisema:

"Nataka kuona kidole kitakacho-ni-nyoshea mimi katika Umoja wa Afrika,ambacho hakina madhambi. "

Hapo hajakosea -miongoni mwake nani asie na madhambi?Janga la ugonjwa wa kipundupindu ulioripuka nchini Zimbabwe unadhihirisha jinsi serikali ilivyosambaratika.Lakini hakuna kilichotamkwa waziwazi na Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika wala Umoja wa Afrika.

Mito ya kumuondosha Mugabe madarkani iliyotolewa na Odinga na mshindi wa zawadi ya amani ya Nobel Askofu Mkuu Desmond Tutu hivi karibuni, imepingwa na Umoja wa Afrika.

Kuhusika na suala la kutumiwa nguvu kumuondosha Mugabe,msemaji wa mwenyekiti wa Umoja wa Afrika,Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete alijibu kwa kuuliza iwapo ugonjwa wa kipindupindu unaweza kudhibitiwa kwa silaha.Na Waziri wa Mambo ya Nje wa Afrika Kusini amesema,kutuma majeshi nchini Zimbabwe si suluhisho.

Kwa hivyo kama kawaida,mbinyo unatoka upande wa jamii za kiraia,vyama vya wafanyakazi na makanisa.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW