Makubaliano ya usalama ya DRC na Rwanda kuanza Oktoba
25 Septemba 2025
Nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Rwanda zimekubaliana kuanza utekelezaji wa hatua za kiusalama mwezi ujao chini ya makubaliano yaliyoratibiwa na Marekani. Tangazo hilo limetolewa katika taarifa ya pamoja siku ya Jumatano, katika kile ambacho kitakuwa ni hatua muhimu katika utekelezaji wa makubaliano hayo ya amani huku kukiwa na wasiwasi juu ya maendeleo yake.
Makubaliano hayo yaliyofikiwa katika mkutano wa Washington Septemba 17-18na kuripotiwa kwa mara ya kwanza na shirika la habari la Reuters, yataanza Oktoba 1, kwa mujibu wa taarifa ya pamoja, ambayo pia ilitolewa na Marekani, Qatar, Togo na Kamisheni ya Umoja wa Afrika.
Nchi hizo zilikubali kukamilisha hatua hizo ifikapo mwisho wa mwaka, vyanzo vitatu vinavyofahamu suala hilo viliiambia Reuters. Kongo na Rwanda pia bado hazijapanga tarehe kwa wakuu wa nchi kusafiri kwenda Washington huku mazungumzo ya Doha, yakisuasua.