1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya Uturuki

Abdu Said Mtullya21 Februari 2013

Wahariri wanatoa maoni juu ya kauli iliyotolewa na Kamishna wa Umoja wa Ulaya Oettinger kuhusu Uturuki kujiunga na Umoja huo.Pia wanatoa maoni juu ya mgogoro wa kisiasa nchini Bulgaria

Kamishna wa nishati wa Umoja wa Ulaya Guenther Oettinger
Kamishna wa nishati wa Umoja wa Ulaya Guenther OettingerPicha: AFP/Getty Images

Gazeti la "Reutlinger General Anzeiger " linaizingatia kauli iliyotolewa na Kamishna wa Umoja wa Ulaya Günther Oettinger juu ya Uturuki.Akizungumza kwenye mhadhara ulioandaliwa na Wakfu wa Konrad Adenauer, Bwana Oettinger alitabiri kwamba siku moja Kansela wa Ujerumani na rafiki zake wa Ufaransa wataenda Uturuki na kupiga magoti kuiomba nchi hiyo ijiunge na Umoja wa Ulaya.

Gazeti la "Reutlinger General -Anzeiger" linasema kauli hiyo imepagusa pale hasa panapostahili.Linasema Uturuki imo miongoni mwa nchi zinazostawi kwa kiwango kikubwa duniani. Hatahivyo mhariri wa gazeti hilo anatahadharisha kwamba itakuwa vizuri ikiwa Kansela wa Ujerumani pia atayazingitaa maadili ya Umoja wa Ulaya katika kulitafakari suala la uanachama wa Uturuki katika Umoja wa Ulaya.Ukweli ni kwamba Uturuki haiyafuati maadili yote ya Umoja wa Ulaya.Kwa mfano mpaka leo Uturuki haijaitambua Cyprus.Na pia inakabiliwana na mapungufu mengi juu ya uhuru wa kutoa maoni.

Mgogoro wa kisiasa unaendelea nchini Bulgaria na Waziri Mkuu wa nchi hiyo pamoja baraza lake la mawaziri wametangaza kujiuzulu. Gazeti la "Döbelner Anzeiger"linasema Waziri Mkuu wa Bulgaria Borisssow anaependa sana umaarufu aliingia madarakani akiwa na kinywa kilichojaa ahadi kwa watu wake.

Pamoja na mambo mengine aliahidi kuleta usasa,kuinua mapato ya watu wake na kupiga vita rushwa.Lakini Bulgaria ndiyo nchi masikini kuliko zote katika Umoja wa Ulaya. Hali halisi imemlazimisha Waziri Mkuu huyo kupitisha hatua kali za kubana matumizi ili kuirekebisha bajeti kulingana na mwongozo wa Umoja wa Ulaya unaouruhusu nakisi ya hadi asilimia tatu tu.

Matokeo yake ni kwamba watu wake sasa wanaishi chini ya kiwango cha wastani wa maisha barani Ulaya.

Gazeti la"Rheinpfalz" linatafakari madhara yanayoweza kutokea endapo Cyprus itajitoa kutoka Umoja wa sarafu ya Euro.Na linaeleza kwamba Cyprus ni nchi ndogo yenye watu wasiozidi milioni moja.Kwa kweli ni mbilikimo kiuchumi.

Gazeti la"Rheinpfalz"linasema ikiwa Cyprus itajiondoa kwenye Umoja wa Ulaya, baadhi wanafikiri hapatakuwa na haja ya kushika tama.Hayo ni mawazo mafupi. Gazeti hilo linaeleza kuwa licha ya udogo wake kiuchumi,madhara yatakuwa makubwa sana katika ukanda wa sarafu ya Euro ikiwa Cyprus itafilisika.

Mwandishi:Mtullya Abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri:Yusuf Saumu