1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mapigano yanaendelea Syria

30 Oktoba 2011

Rais Bashar al Assad ametishia kutokea maafa makubwa katika mashariki ya kati, iwapo mataifa ya magharibi yataiingilia hali Syria

Rais Bashar al Assad wa SyriaPicha: AP

Vikosi vya usalama nchini Syria vimewaua raia 10 katika mapigano makali mjini Homs hapo jana. Hayo ni kwa mujibu wa ripoti za wanaharakati.

Raia 10 wameuawa katika mapigano mjni HomsPicha: picture-alliance/dpa

Kundi moja limesema kuwa wanajeshi wanaoshukiwa kutoroka jeshi la nchi hiyo, wamewaua wanajeshi 20 katika mji huo ambao umekuwa kitovu cha upinzani dhidi ya rais Bashar al Assad.

Umwagaji damu wa hapo jana, umejiri siku moja baada ya wanaharakati na wakaazi kusema kuwa vikosi vya Assad viliwaua watu 40 vilipowafyetulia risasi waandamanaji wanaotoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuwalinda dhidi ya serikali ya syria inayotumia mabavu kukandamiza mapinduzi ya miezi 7 nchini humo.

Picha: picture-alliance/dpa

Waandamanaji hao, wakihofia mashambulio ya angani, wametoa wito kwa Umoja wa Mataifa kupiga marufuku ndege kuruka katika anga ya nchi hiyo, kama ilivyofanyiwa Libya.

Katika mahojiano na gazeti la Jumapili la Uingereza, Sunday Telegraph, Rais Assad amesema, mataifa makuu ya magharibi yanahatarisha kuzusha maafa makubwa katika Mashariki ya Kati, iwapo yataingilia kati.

Vurugu za Ijumaa zilisababisha mawaziri wa kiarabu kwa mara ya kwanza kabisa kutoa wito mkali kwa Assad wakimtaka asitishe mauaji ya raia.

Mwandishi:Maryam Abdalla/rtr afp
Mhariri:Prema Martin