1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani au Urusi? Mzozo wa Ukraine waiweka njia panda Ghuba

28 Februari 2022

Kuchagua upande katika mzozo wa Ukraine kungekuwa rahisi waakti mmoja kwa mataifa ya Ghuba ya Kiarabu yanayolindwa kwa muda mrefu na Marekani, lakini uhusiano unaoongezeka na Moscow unayalazimu kuchukua tahadhari.

Saudi-Arabien Riyadh | Palast | Gulf Cooperation Council
Picha: Bandar Aljaloud/Saudi Royal Palace/AP/picture alliance

Wakati dunia ikikimbilia kulaani uvamizi wa Urusi dhidi ya jirani yake mdogo, nchi tajiri za Baraza la Ushirikiano la Ghuba (GCC) zikiwemo Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kwa kiasi kikubwa zimenyamaza.

Wataalamu wa Mashariki ya Kati wanasema kusita kwao kunaeleweka kutokana na kile masula muhimu -- nishati, pesa na usalama.

"Siyo tu uhusiano wa kiuchumi unaokua, lakini pia uhusiano wa usalama wa mataifa haya na Moscow," Anne Gadel, mtaalam wa Ghuba na mchangiaji wa Taasisi ya Ufaransa ya Montaigne alisema.

Soma pia: Ulaya yawakaribisha wakimbizi wa Ukraine

Siku ya Ijumaa, UAE ilijizuia pamoja na China na India, kupigia kura azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kutaka Moscow iondoe wanajeshi wake.

Urusi kama ilivyotarajiwa ilipinga azimio hilo lililotayarishwa na Marekani na Albania, huku wajumbe 11 kati ya 15 wa baraza hilo wakilipigia kura.

Viongozi wakuu wa mataifa ya Ghuba ya Kiarabu wakiwa kwenye mkutano wao mjini Riyadh.Picha: Bandar Aljaloud/Saudi Royal Palace/AP/picture alliance

Baada ya kura hiyo, shirika la habari la serikali ya Emirati, WAM, lilisema UAE na mawaziri wa mambo ya nje wa Marekani walizungumza kwa njia ya simu kupitia "maendeleo ya kimataifa". Hakukuwa na utajo wowote juu ya Ukraine.

Wizara ya mambo ya nje ya Urusi wakati huo huo ilitangaza kuwa mawaziri wa mambo ya nje wa UAE na Urusi wangekutana Jumatatu mjini Moscow kujadili "kupanua zaidi uhusiano wa pande nyingi kati ya Urusi na UAE".

Saa chache kabla ya Urusi kuanzisha mashambulizi yake makubwa ya ardhini, baharini na angani dhidi ya Ukraine siku ya Alhamisi, UAE ilikuwa "imesisitiza urafiki wa kina" na Moscow.

Soma pia: Vita vya Ukraine vyahatarisha hali ya maisha Yemen na Misri

Taifa kubwa la Ghuba Saudi Arabia haijazungumzia uvamizi huo, kama ilivyokuwa kwa UAE, Bahrain na Oman. Kuwait na Qatar zimeshutumu tu ghasia hizo, na kuacha kuikosoa Moscow.

Kwa zaidi ya miongo saba, Marekani imekuwa na jukumu muhimu katika kanda ya Mashariki ya Kati iliyokumbwa na mizozo, ikihudumu hasa kama mlinzi wa wafalme tajiri wa mafuta wa Ghuba dhidi ya vitisho vinavyoweza kutokea kama vile Iran.

Lakini katika miaka ya hivi karibuni, Washington ilianza kupunguza ushiriki wake wa kijeshi katika eneo hilo, hata wakati washirika wake wa karibu Saudi Arabia na UAE wakishambuliwa na waasi wa Kihouthi wa nchini Yemen.

Vituo vya kampuni kubwa ya mafuta ya Saudia Aramco vilipigwa mwaka 2019 na waasi hao wanaofungamana na Iran.

Nchi za Ghuba "zinaelewa kuwa zinahitaji kubadilisha miungano yao ili kufidia kile kinachodhaniwa kuwa ni kujiondoa kwa Marekani katika eneo hilo", alisema Gadel.

Mwanfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman hajazungumzia chochote kuhusu mzozo kati ya Urusi na Ukraine.Picha: SAUDI PRESS AGENCY/VIA REUTERS

Siasa ni muhimu pia

Saudi Arabia na UAE, washirika wawili wa Marekani wanaowapokea wanajeshi wa Marekani, wameshuhudia uhusiano wao na Washington ukibadilika na kuwa uhusiano wa chuki ya upendo kutokana na mikataba ya silaha na masuala ya haki za binadamu.    

Mauaji ya mwaka 2018 ya mwandishi wa habari wa Saudia Jamal Khashoggi ndani ya ubalozi mdogo wa Istanbul yamezorotesha uhusiano na Riyadh, na UAE imetishia kufuta mpango mkubwa wa ndege za kivita chapa F-35 zilizotengenezwa na Marekani. 

"Urusi inaonekana kama mshirika wa kiitikadi huku masharti ya haki za binadamu ya Marekani yanayoambatana na msaada wao yanazidi kutia ugumu," alisema Andreas Krieg, mtaalam wa Mashariki ya Kati na profesa msaidizi katika Chuo cha King's College London.

Soma: Urusi yaiteka miji miwili midogo ya Kusini mwa Ukraine

 "Kumekuwa na uunganishwaji wa mkakati mkuu kati ya Moscow na Abu Dhabi linapokuja suala la kanda. Wote wapinga mapinduzi na walikuwa na azma ya kudhibiti Uislamu wa kisiasa."

Licha ya kuongezeka kwa ushirikiano wa kiusalama na Urusi, ambayo inahusika moja kwa moja katika mizozo ya Syria na Libya, Krieg anasema mataifa mengi ya GCC "bado yataweka mayai yao ya usalama kwenye kapu la Marekani".

Mwanamfalme wa Abu Dhabi, Mohammed bin Zayed al-Nahyan.Picha: Thomas Samson/AFP/Getty Images

Lakini "wameanza kubadilisha uhusiano na washindani wa Marekani na wapinzani katika nyanja zingine".

Biashara kati ya Urusi na nchi za GCC ilipanda kutoka karibu dola bilioni 3 mwaka 2016 hadi zaidi ya dola bilioni 5 mwaka 2021, hasa kwa UAE na Saudi Arabia, takwimu rasmi zinaonyesha.

UAE, haswa Dubai, imeonekana kwa muda mrefu kama kivutio cha uwekezaji wa Urusi, na mahali pa likizo kwa matajiri wa Urusi.  Kama washiriki wakuu katika soko la nishati, mataifa mengi ya GCC yana uhusiano na Urusi kama wazalishaji wenza. 

Soma: Maoni: Hatimaye Ujerumani yaja na msimamo dhidi ya Urusi

Riyadh na Moscow zinaongoza muungano wa OPEC+, zikidhibiti kikamilifu uzalishaji ili kudhibiti bei katika miaka ya hivi karibuni.    

"Wanachama wa Kiarabu wa OPEC wako katika wakati mgumu kidiplomasia, kwani kudumisha" mpango wa OPEC+, ambao unadhibiti uzalishaji, "ni wazi kuwa mstari wa mbele katika fikira zao", alisema Ellen Wald, mkuu mwenzake wa taasisi ya ushauri ya Baraza la Atlantiki.

Mauaji ya mwandishi habari Jamal Khasshoggi yalisababisha kushuka kwa uhusiano kati ya Marekani na Saudi Arabia.Picha: Sean Gallup/Getty Images

"Nchi za Ghuba zinahofia kuharibu uhusiano huu na kutafuta kudumisha ushiriki wa Urusi katika OPEC+... Ikiwa Urusi itaondoka kwenye kundi hilo, makubaliano yote huenda yakasambaratika."

Licha ya wito wa baadhi ya waagizaji wakubwa wa mafuta kutaka wazalishaji ghafi kuongeza usambazaji na kusaidia kuleta utulivu wa bei, Riyadh, msafirishaji mkuu duniani, hajaonyesha nia.

"Kukaa kimya kuhusu hatua ya Urusi nchini Ukraine pengine ndiyo njia bora kwa hili kwa sasa," Wald alisema.  "Lakini msimamo huu wa kimantiki unaweza usilindike, ikiwa mataifa hayo yatatashinikizwa juu ya msimamo wao na viongozi wa Magharibi."

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW