1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan

Marekani yatangaza vikwazo kwa wanaovuruga amani ya Sudan

29 Septemba 2023

Marekani imeziwekea vikwazo kampuni mbili ikiwemo moja iliyoko nchini Urusi, pamoja na mtu mmoja inayomtuhumu kuchochea mapigano Sudan yaliyosababisha mauaji ya maelfu ya watu, huku wengine wengi wakipoteza makaazi yao.

Sudan | die Generäle Abdel Fattah Abdelrahman al-Burhan und Mohamed Hamdan Dagalo
Kiongozi wa jeshi la kitaifa Sudan Jenerali Abdul Fattah Al Burhan na kiongozi wa Kikosi cha Wanamgambo wa RSF Mohammed Hamdan Dagalo wakiwa mjini KhartoumPicha: Mahmoud Hjaj/AA/picture alliance

Vikwazo hivyo ni hatua ya hivi karibuni iliyochukuliwa na Marekani, baada ya vita kati ya Jeshi la Sudan linaloongozwa na Jenerali Abdul Fattah Al Burhan na kiongozi wa Kikosi cha Wanamgambo wa RSF Mohammed Hamdan Dagalo, kuanza mwezi Aprili kufuatia mipango ya mabadiliko ya mpito ya kisiasa na kujumuishwa kwa kikosi cha RSF ndani ya jeshi, miaka minne baada ya kiongozi wa muda mrefu nchini humo Omar al Bashir kuondolewa madarakani kupitia maandamano ya kuupinga utawala wake.

MSF:Mashambulizi ya raia yamefikia kiwango cha kutisha Sudan

Waziri mdogo wa hazina ambaye pia anasimamia masuala ya ugaidi na mienendo ya miamala ya fedha nchini Marekani Brian Nelson, amesema hatua iliyochukuliwa ni ya kuwawajibisha wale waliopindisha hatua za upatikanaji wa amani na suluhu ya kidemokrasia Sudan.

Amesema Marekani itaendelea kuwalenga wale wanaochochea mgogoro kwa manufaa yao binafsi. 

Ali Karti, Waziri wa mambo ya kigeni chini ya utawala wa Bashir, aliyekuwa kiongozi wa vuguvugu la wanamgambo wa Sudan, baada ya Bashir kuondolewa madarakani mwaka 2019 ameguswa moja kwa moja na vikwazo hiyvo. Al Karti ni kiongozi maarufu na mtiifu aliyeongoza kwa miaka mingi katika utawala wa Bashir, anadaiwa kuwa miongoni mwa viongozi wanaolinda masilahi yao na kujiimarisha baada ya mapinduzi ya 2021 yaliyofanywa na jeshi pamoja na kikosi hicho cha RSF.

Kiongozi wa Sudan aonya juu ya kuenea kwa vita

Blinken: Marekani inachukua hatua dhidi ya wanaovuruga amani ya Sudan.

Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Antony BlinkenPicha: Alex Brandon/AP Photo/picture alliance

Wanachama wa vuguvugu hilo wameliunga mkono jeshi katika vita vyake na vikosi vya RSF. Baada ya vikwazo hivyo kutangazwa hapo jana, vuguvugu la Al Karti lilitoa taarifa kusema linaunga mkono uthabiti wa Sudan.

Pia vikwazo vilivyowekwa na Marekani vimelengwa kwa kampuni na GSK ya Sudan ambayo Marekani inasema ilitumiwa kufanya manunuzi kwa vikosi vya RSF. GSK inadaiwa kufanya kazi na kampuni ya usambazaji ya kijeshi ya Urusi Aviatrade iliyowekewa vikwazo pia.

Kiongozi wa kijeshi wa Sudan akutana na kiongozi wa Qatar

Kampuni hiyo inasemekana kutoa mafunzo ya ndege zake zisizokuwa na rubani zilizonunuliwa na RSF hivi karibuni. Hata hivyo mshauri wa RSF aliliambia shirika moja la utangazaji la Kimataifa kwamba hawana uhudiano wowote na kampuni hizo mbili zilizowekewa vikwazo.

Huku hayo yakiarifiwa waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Antony Blinken amesema Marekani imechukua hatua ya kudhibiti utoaji wa visa za kusafiria kwa watu wanaoaminika kuwa chanzo cha kuvuruga amani ya Sudan.

Chanzo: reuters