1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Masuala tete hayajateguliwa katika mkutano wa COP26

8 Novemba 2021

Mkutano wa kujadili mabadiliko ya tabia COP26 umeingia wiki ya mwisho Jumatatu, lakini nchi bado zinatofautiana kuhusu masuala tete.

England Weltklimagipfel COP26 in Glasgow
Picha: Erin Schaff/The New York Times/AP/picture alliance

Baadhi ya masuala tete ni pamoja na jinsi ya kudhibiti hewa ukaa, kusaidia nchi ambazo tayari zinakumbwa na athari za ongezeko la joto duniani.

Baada ya wiki ya kwanza iliyojaa ahadi kubwa kubwa kutoka Uingereza ambayo ndiyo mwenyeji wa mkutano huo za kumaliza ukataji misitu na kuzika kwenye kaburi la sahau matumizi ya mkaa wa mawe, wataalam wanasema mkutano wa COP26 haujapiga hatua yoyote muhimu kutatua masuala yaliyopo.

Japo ahadi hizo huweza kuashiria kwamba wanakaribia muafaka, masuala mengi ambayo ni tete bado hayajapata ufumbuzi.

Soma: Wanaharakati vijana waandamana katika mkutano wa COP26

Mshauri wa sera wa shirika la kimataifa la Climate Action Network Sven Harmeling asema huenda maazimio yatakosa nguvu ikiwa hakutakuwa na maelewano muafaka wiki hii.

   ”Tunahitaji makubaliano dhahiri kuhusu kupunguza uzalishaji hewa ukaa kwa sababu bila hiyo, hasara na madhara yataendelea zaidi. Lakini nadhani kila mmoja anapaswa kujua kwamba wiki hii matokeo jumla yako hatarini ikiwa hatutapiga hatua muhimu kuelewana kuhusu hasara na athari ambazo zimeshatokea na vilevile suala la fedha,” amesema Harmeling.

Masuala yanayosababisha mkwamo ni yapi?

Miongoni mwa masuala hayo ni pamoja na mipango ya kila nchi kupunguza utoaji wa gesi ukaa, kutimiza ahadi ya muda mrefu ya kuchanga dola bilioni 100 kila mwaka kusaidia mataifa masikini pamoja na sheria za kushughulikia masoko ya gesi ukaa.Picha: Nikolay Doychinov/DW

Stephen Leonard ambaye ni mtaalamu wa sheria na sera kuhusu tabianchi na vilevile muangalizi wa muda mrefu wa mikutano ya COP ameliambia shirika la AFP kwamba nchi zote zimeshikilia misimamo mikali.

Soma: Uchafuzi wa hewa kuongezeka tena mwaka huu

Kwa mfano, Umoja wa Ulaya unataka mkakati wa hali ya juu kabisa uchukuliwe kupunguza utoaji gesi ukaa.

Nchi za Afrika zinahitaji fedha zaidi kukabiliana na madhara, huku Australia na Japan kwa upande wao zikitaka zaidi kuendelea kutumia mkaa wa mawe.

Katika kikao cha leo, serikali zitajaribu kupata muafaka wa jinsi ya kuzisaidia nchi ambazo ziko katika hatari kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi na kuzifidia kutokana na athari ambazo tayari zimeshatokea. Huo utakuwa mtihani kubaini ikiwa nchi tajiri na maskini zitaweza kumaliza mkwamo kuhusu suala la fedha.

Ahadi lukuki

Katika wiki ya kwanza ya mkutano huo, nchi 100 ziliahidi kupunguza utoaji wao wa gesi chafu ya methane kwa asilimia 30 ifikapo mwaka 2030.

Soma: Viongozi COP26 waahidi juhudi mpya kuokoa misitu ya dunia

India ambayo ni miongoni mwa mataifa yanayochangia utoaji hewa ukaa kwa kiwango kikubwa pia ilitangaza itafaulu kutokomeza utoaji wa gesi hiyo ifikapo mwaka 2070

Kulingana na ripoti ya wataalam, ili kudhibiti ongezeko la joto kuwa katika kiwango cha 1.5 celcius, ni sharti gesi hizo chafu zipunguzwe kwa asilimia 45 katika karne hii.Picha: Duncan McGlynn/AP Images for AVAAZ/picture alliance

Uingereza ambayo ni mwenyeji wa mkutano huo ilitangaza ahadi mpya ya pauni milioni 290, pamoja na msaada kwa nchi za kanda ya Asia Pasifiki kupambana na ongezeko la joto duniani.

Wataalam wanasema ahadi hizo zinaweza kuwa na matokeo chanya siku za baadaye kukabili ongezeko la joto.

Wito wa Obama kwa wajumbe wa Glasgow

Lakini uchunguzi uliofanywa na Umoja wa Mataifa wiki iliyopita uligundua kwamba utaoaji wa gesi chafuzi utaongezeka kwa asilimia 13.7 ifikapo mwaka 2030.

Rais wa zamani wa Marekani Barrack Obama ambaye leo amehutubia mkutano huo leoametoa wito kwa mkutano wa kimataifa wa mabadiliko ya tabianchi wa COP26 unaofanyika mjini Glasgow kushughulikia kitisho kinachoyakabili mataifa ya visiwa kutokana na kupanda kwa kina cha bahari.

Nchi zinazohudhuria mkutano huo wa Glasgow zinatarajiwa kujadili jinsi ya kutekeleza malengo ya mkataba wa Paris ya kupunguza ongezeko la viwango vya joto kati ya nyuzijoto 1.5 na 2.0.

(APE, AFPE, RTRE)