1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan

Norway yahimiza baraza la haki la UN kuchunguza ghasia Sudan

30 Septemba 2023

Marekani, Uingereza, Norway na Ujerumani zinapanga kuwasilisha pendekezo kwa Baraza la haki la Umoja wa Mataifa kuanzisha uchunguzi juu ya madai ya kufanyika kwa vitendo vya kikatili nchini Sudan.

Mkuu wa jeshi la Sudan Jenerali Abdel Fattah Abdelrahman al-Burhan na kiongozi wa kikosi cha RSF Mohamed Hamdan Dagalo
Mkuu wa jeshi la Sudan Jenerali Abdel Fattah Abdelrahman al-Burhan na kiongozi wa kikosi cha RSF Mohamed Hamdan DagaloPicha: Mahmoud Hjaj/AA/picture alliance

Rasimu ya pendekezo hilo iliyoonekana na shirika la habari la Reuters, inalaani visa vya ukiukaji wa haki za binadamu na unyanyasaji uliofanywa wakati wa vita vya miezi mitano nchini Sudan.

Rasimu hiyo inanuia kuunda jopo la watu watatu ili kuchunguza ghasia hizo. Jopo hilo limetwikwa jukumu la kuainisha visa vya ukiukwaji wa haki za binadamu na kuandika ripoti kwa baraza la Baraza la haki la Umoja wa Mataifa lenye wanachama 47.

Umwagaji damu, ghasia na visa vya watu kuhama makwao vimeongezeka tangu kuanza kwa vita kati ya jeshi la Sudan na kikosi cha msaada wa dharura RSF mwezi Aprili, na kuipeleka Sudan kwenye ukingo wa vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Sehemu zilizoathirika zaidi na vita hivyo ni Darfur Magharibi, ambapo mashambulizi yaliyochochewa kikabila yamesababisha vifo vya mamia ya watu.