1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUlaya

Mataifa ya Ulaya kujadiliana namna ya kukabiliana na droni

26 Septemba 2025

Umoja wa Ulaya utafanya mazungumzo ya kwanza yanayolenga kuja na pendekezo la kujenga mfumo wa kuzuia droni. Hii ni baada ya uvamizi wa droni za Urusi kwenye anga za wanachama wake unaoibua kitisho kwa muungano huo.

Poland Czosnowka 2025 | Ndege isiyo na rubani ya Urusi iliyoharibiwa baada ya kuanguka katika kijiji cha Poland
Ndege isiyo na rubani iliyoharibika ikiwa imeanguka baada ya kuanguka katika kijiji cha Czosnowka mashariki mwa Poland, katika picha hii iliyopatikana kutoka kwa mitandao ya kijamii, huko Czosnowka, Poland, Septemba 10, 2025.Picha: Dariusz Stefaniuk/REUTERS

Siku ya Ijumaa, Kamishna wa Umoja wa Ulaya wa masuala ya Ulinzi Andrius Kubilius amesema atazungumza kwa njia ya video na maafisa wa mataifa kama 10 hivi kati ya 27 ya umoja huo kuangazia mapendekezo ya kuwa na mifumo hiyo ya kuzuia droni.

Washiriki wengi ni wale wanaotoka kwenye mataifa ya Umoja wa Ulaya lakini yanayopakana na Urusi na Ukraine. Hata hivyo, Denmark iliongezwa kwenye orodha ya washiriki kufuatia matukio ya karibuni ya droni kuingia kwenye anga yake.

Ukraine ambayo licha ya kuwa na mfumo wake wa kugundua na kudungua droni za Urusi pia itashiriki.  

Wito watolewa wa kuunda "drone wall"

Mapema mwezi huu, Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von de Leyen  alitoa wito wa kuwa na mfumo kama huu ama "drone wall" alipokuwa akitoa hotuba, masaa machache baada ya marubani wa NATO kudungua droni za Urusi nchini Poland.

Watu wakiwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Aalborg, mjini Aalborg, Denmark, Septemba 25, 2025. droni zilionekana kwenye uwanja wa ndege Jumatano jioni na usiku wa kuamkia Alhamisi, na uwanja huo wa ndege wa Aalborg kufungwa.Picha: Bo Amstrup/Ritzau Scanpix/REUTERS

Mjini Copenhagen, kisa kipya cha droni iliyoonekana kwenye anga ya Denmark kimesababisha uwanja wa ndege kufungwa hii ikiwa ni mara ya pili katika kipindi cha masaa machache, baada ya Waziri Mkuu Mette Frederiksen kusema kwamba safari za ndege ni sehemu ya "mashambulizi mseto" ambayo huenda yanafanywa na Urusi. 

Droni zimeonekana zikirandaranda kwenye eneo kuliko viwanja vya ndege vya Denmark tangu siku ya Jumatano na kusababisha moja ya viwanja hivyo kufungwa kwa masaa kadhaa baada ya tukio kama hilo kusababisha kiwanja kikubwa cha Copenhagen kufungwa mapema wiki hii. 

Mette amesema "Wapi tulipo kufikia sasa? Kwanza mamlaka zimeongeza hali ya tahadhari. Na zinajiandaa kwa matukio ya aina yoyote. Hii inamaanisha, kwamba, pamoja na mambo mengine wanajeshi na polisi wengi zaidi watakuwa na uwezo mkubwa na mbinu za kuzuia mashambulizo ya droni katika maeneo ya miundombinu muhimu siku za usoni."

Visa kama hivi tayari vimeshuhudiwa kwenye mataifa ya Norway na Romania pamoja na ukiukwaji ulioshuhudiwa kwenye anga ya Estonia baada ya ndege za kijeshi za Urusi kuingia kwenye eneo hilo, hali iliyoibua wasiwasi katikati ya uvamizi wa Urusiuvamizi wa Urusi nchini Ukraine.

Mkurugenzi wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki, IAEA Rafael Grossi akizungumza kwenye mkutano Juni 25, 2025Picha: Helmut Fohringer/APA/picture alliance

IAEA laonya kitisho cha droni kwenye vinu vya nyuklia

Katika hatua nyingine, Shirika la Umoja wa Mataifa la Nguvu za Atomiki, IAEA limesema leo kwamba kwa mara nyingine droni zimesababisha  kitisho cha kiusalama kwenye vinu vya nyuklia nchini Ukraine.

Mkuu wa shirika hilo Rafael Grossi amesema kwenye taarifa yake kwamba droni hizo zinazoruka karibu sana na vinu hivyo zinaviweka hatarini baada ya droni moja kudunguliwa ikiwa umbali wa mita 800 kutoka kwenye kinu kilichopo mkoa wa Mykolaiv jana usiku. Droni nyingine kama 22 zilikaribia kinu hicho kiasi cha mita 500, ingawa hakukuripotiwa uharibifu.

Huku hayo yakiendelea, Kyiev imeendeleza mashambulizi yake ya kupanga ya droni kwenye vituo vya mafuta vya Urusi mamlaka zimesema hii leo, huku wataalamu wakikisia kwamba Urusi imekwishapoteza robo ya uwezo wake wa kuchakata mafuta kutokana na mashambulizi ya kila mara kwenye vituo vyake.

Ruka sehemu inayofuata Gundua zaidi
Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW