1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo ya muafaka wa Brexit Uingereza yavunjika

Sekione Kitojo
18 Mei 2019

Chama cha upinzani cha Labour nchini Uingereza kimevunja mazungumzo ya wiki sita sasa ya Brexit ya kupata muafaka na waziri mkuu  Theresa May,na kulalamika kuwa mamlaka yake yanayeyuka na utawala wake unakaribia mwisho.

UK Brexit | Kombobild Theresa May und Jeremy Corbyn
Picha: picture-alliance/dpa

Kiongozi  wa  chama  cha  labour  Jeremy Corbyn  amesema mpasuko kati yao hauwezi  kuzibwa, na ile  hali ya kujiamini  haipo tena  kwamba  mrithi wake  ataendelea  na  maridhiano yoyote yanayoweza  kupatikana. Majadilino "yamekwenda  hadi  yalipofikia," Corbyn  amesema  katika  barua  kwa  May.

Kiongozi wa upinzani bungeni Jeremy Corbyn Picha: picture-alliance

"Ongezeko  la  udhaifu  na  kutokuwa  thabiti kwa  serikali  yako kuna  maana  hakutakuwa  na  imani  katika  kulinda  chochote kinachoweza  kukubaliwa  baina  yetu," amesema.

Corbyn  amesema  chama  cha  Labour kwa hiyo  kitaendelea kupinga  makubaliano  ya  taalka yaliyofikiwa  na  serikali  kama yalivyo  hivi  sasa.

Wabunge  mara  tatu  waliyakataa  makubaliano  yaliyofikiwa  na May  pamoja  na Umoja  wa  Ulaya, na  kumlazimisha kuchelewesha tarehe ya  Brexit  mara  mbili na  kukinyooshea  mkono  chama  cha Labour.

Muda mpya  wa  mwisho  ni  Oktoba  31.

Bunge linatarajiwa  kupiga  kura  kwa  mara  ya  nne  mapema mwezi  Juni  kuhusiana  na  masharti  ya  Uingereza  kujitoa  kutoka Umoja  wa  Ulaya.

Waziri mkuu Theresa May wa UingerezaPicha: picture-alliance/NurPhoto/W. Szymanowicz

May anaonekana kuchoka

May  ambaye ameonekana  kuchoka  alisema  wabunge watakabiliwa  na  kile  alichosema  kuwa  ni " chaguo gumu": kupiga kura  kukubaliana  na  Brexit , ama  "kukataa  tena".

Alikuwa  akizungumza  katika  tukio  mahsusi  la  kampeni kabla  ya uchaguzi  wa  bunge  la  Ulaya, utakaofanyika  nchini  Uingereza siku ya  Alhamis, ambapo  maoni  ya  wapiga  kura  yanaonesha  chama chake  cha  Conservative  kinaweza  kushika  nafasi  ya  tano.

Uingereza  haikutaka  kushiriki  katika  uchaguzi  huo  lakini  itafanya hivyo kwasababu  ya  kuahirishwa  kwa  Brexit.

bango linalosisitiza Uingereza kubakia katika Umoja wa Ulaya wakati wa maandamano mjini LondonPicha: Getty Images/AFP/B. Stansall

Kuvunjika  kwa  mazungumzo  hayo  kumekuja  siku  moja  baada  ya May  kukubali kuweka  muda  maalum kwa  ajili  ya  kuachia  wadhifa wa  uwaziri  mkuu  kufuatia  kura  ya  kujitoa  kutoka  Umoja  wa Ulaya  bungeni, ambayo  itafanyika  katika  muda  wa  wiki  moja kuanzia  Juni 3. Makubaliano  hayo  yamefikiwa  katika  mkutano  wa faragha pamoja  na  wanachama  na  viongozi  wa wabunge wa chama  cha  Conservative.

Inafikiriwa  kwamba  May atazindua  mpambano wa kuwania  nafasi ya  uongozi mara  mswada wa  makubaliano ya   kujitoa  ama ukishindwa, kama  inavyoonekana  kuwa , ama utakamilishwa.

Mwandishi: Sekione Kitojo

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW