1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUganda

Mbabe wa kivita wa Kongo atishia kuanzisha upya mapambano

16 Julai 2025

Mbabe wa siku nyingi wa vita nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Thomas Lubanga amekosoa mchakato wa mazungumzo kati ya serikali ya Kinshasa na waasi wa M23 akisema yametanguliza maslahi ya kigeni.

Uganda Kampala 2025 | Thomas Lubanga
Mbabe wa siku nyingi wa vita Thomas Lubanga atishia kuanzisha upya mapigano dhidi ya serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya KongoPicha: Lubega Emmanuel

Amesema aidha kwamba mazungumzo hayo yanafungulia milango wageni kuingia nchini humo kupora rasilimali za nchi badala ya kuleta amani hasa Mashariki mwa nchi hiyo.

Katika kikao cha waandishi wa habari mjini Kampala siku ya Jumatano, Lubanga ametisha kuanzisha tena mapambano ya kijeshi dhidi ya utawala wa rais Tshisekedi ambaye licha ya kuwasiliana naye mara kadhaa kuhusu masuala nyeti ya kuleta amani ya kudumu amendelea kumpuuza.

Kila wakati jina Thomas Lubanga linahusishwa na harakati za kijeshi na kisiasa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ameibuka tena na kufahamisha kuwa angali mdau muhimu katika siasa za DRC chini ya vuguvugu lake la Mjumuiko wa Kimapinduzi CRP.

Amepongeza mazungumzo yanayoendelea huko Doha, kati ya serikali ya rais Tshisekedi na kundi la AFC/M23. Lakini anachokosoa ni kwamba maafikiano kati ya Marekani, DRC na Rwanda yamejikita zaidi katika namna rasilimali za Kongo za madini zinavyoweza kutumiwa bila kusababisha mgogoro miongoni mwa makundi mbalimbali.

Rais Donald Trump wa Marekani alipozungumza kwenye ofisi ya Oval, White House baada ya makubaliano ya amani yaliyoratibiwa na Marekani Picha: Joe Raedle/Getty Images

Lubanga alikuwa mshtakiwa wa kwanza wa ICC, 2012

Ikumbukwe kuwa Thomas Lubanga ndiye alikuwa mtu wa kwanza kushitakiwa kwenye Mahakama ya Kimataifa ya ICC mwaka 2012 kwa uhalifu dhidi ya ubinaadamu na uhalifu wa kivita. Kwa zaidi ya miaka 20 amekuwa akihusishwa na harakati "za kuikomboa DRC" na kuleta amani nchini humo. Lakini kwa baadhi ya raia wa Kongo, yeye alikuwa miongoni mwa wale waliochochea vita.

Lubanga analalamika kuwa kundi lake limetengwa katika mchakato wa kuleta amani DRC na hadhani kama kuunaweza kuwa na suluhu kwenye suala la utawala wa nchi hiyo, ikiwa wadau muhimu kama yeye hawatahusishwa.

Baada ya kutumikia kifungo cha ICC cha miaka 14 alichohukumiwa 2020, Lubanga alitafuta hifadhi ya kisiasa Uganda. Uganda imekosolewa mara kadhaa kuwa inamsaidia katika harakati zake. Lakini Lubanga anakana madai hayo akisema  hakuna sheria zozote za kimataifa zilizokiukwa katika kumpa hifadhi.

Hadi wakati wa kuandaa taarifa hii, serikali ya Uganda kupitia kwa jeshi na wizara ya masuala ya kigeni walikuwa hawajatoa tamko kuhusu hatua ya Lubanga kuelezea kuwa ana nia ya kuendesha mapambano dhidi ya utawala wa DRC.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW