1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mbilikimo wakabiliwa na hali ngumu DRC

13 Februari 2017

Katika msitu wa Jamuhuri ya Afrika ya kati mashirika mawili yanapambana na hatima ya takriban Mbilikimo elfu 50 ambao wanakabiliwa na umasikini mkubwa, njaa na baadhi yao wametumbukia katika ulevi wa kupindukia.

Kongo Ituri Pygmäen
Picha: imago/ARCO IMAGES

Huku idadi ya wanyama pori ikiendelea kupungua na makundi ya wafadhili yakiendelea kutoa mamilioni ya Dola katika juhudi za kuwalinda wanyama hata hivyo wakosoaji wanasema juhudi hizo zinaweka kipaumbele zaidi kwa wanyama na kupuuza maisha ya binadamu.  

Shirika la kimataifa linaloendesha kampeni za kutetea haki za watu ambao makabila yao yanakabiliwa na hatari ya kutoweka nchini Cameroon la "Survival " limelilaumu shirika la ulinzi wa wanyama pori la World Wildlife Fund for Nature WWF kwa kuwafadhili walinzi wanaopambana na ujangili na ambao wamekuwa wakiwatesa kwa kuwapiga na hata kuwauwa watu Mbilikimo katika eneo hilo la Baka. Shirika la Survival limedai kuwa walinzi hao wamekuwa hawachukuliwi hatua zozote za kisheria.  WWF pia imelaumiwa kwa kukiuka sheria ya kimataifa na kuunga mkono kuanzishwa kwa hifadhi tatu za taifa katika ardhi ya Baka bila ridhaa ya wenyeji wa eneo hilo katika mwongo uliopita, lawama ambazo WWF inazikanusha.

Nembo ya Shirika la kimataifa la WWF

 

Mbilikimo hao tangu walipofurushwa kutoka kwenye ardhi yao ya jadi huku wengi wao wakiwa hawana elimu wanaishi hovyo katika nyumba za majani, Mikoko au nyumba zilizojengwa kwa matofali ya udongo ya kuchoma kandoni mwa barabara za eneo la kusini - mashariki mwa Cameroon nje kido ya maeneo yanayolindwa ambapo ni lazima wapate ruhusa kabla ya kuingia kwenye maeneo hayo.  Maisha ya Wambilikimo hao yanategemea kuishi msituni hasa wakati wa kuvua au wakati wa kutafuta viwavi na vilevile wakati wa msimu wa maembe na katika nyakati hizi huwa wanajikuta wanaingia kwenye mgogoro mgumu baina yao na walinzi.

Michael Hurran mwanaharakati wa shirika la Survival kanda ya Afrika la kutetea haki za watu ambao makabila yao yamo hatarini kutoweka lenye makao yake mjini London nchini Uingereza amesema kwamba iwapo WWF haiwezi kudhibiti unyanyasaji huu na wakati huo huo kuendelea kukataa kutafuta ridhaa ya wenyeji wa Baka basi shirika hilo halina budi kuondoka kutoka kwenye eneo hilo.

Kuongezeka kwa uwindaji haramu duniani ikiwa ni pamoja na kuua Tembo kwa ajili ya vipusa vyao kunasababisha mgongano baina ya walinzi wa mazingira waonaijaribu kuwalinda wanyama waliomo hatarini kutoweka na makabila ambayo yanashindwa kutetea haki ya kumiliki ardhi yao ambayo wamekuwa wanaitegemea kwa karne nyingi.

Idara za serikali za nchini Uswisi ambapo shirika la ulinzi wa wanyama pori lina makao yake zilikubali mnamo mwezi Desemba mwaka uliopita kusuluhisha mgogoro huo wa nchini Cameroon. Katika malalamiko yake rasmi shirika la kimataifa la Survival liliwailisha matamko zaidi ya 20 ikiwa ni pamoja na barua zilizoandikwa kwa mkono na mashirika ya kutetea haki za Mbilikimo wa Baka. Matamko hayo yanaorodhesha madai juu ya unyanyasaji uliyofanywa na walinzi.

Shirika la ulinzi wa wanyama pori duniani WWF linaunga mkono haki za wenyeji katika karatasi tu lakini si kwa matendo amesema Huran mwanaharakati wa shirika la Survival kanda ya Afrika. 
Mbilikimo wamekuwa wanabaguliwa na kufanyiwa dhuluma kwa muda mrefu. Kwa mfano wameonyeshwa kama bidhaa barani Ulaya. Wametumikishwa kama watumwa na katika Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo baadhi yao wamegeuzwa kitoweo.  Watu wa jamii ya Baka na wenyeji wengine watanufaika ikiwa sheria za nchini Cameroon zitabadilishwa ili kuwaruhusu watu hao kuwinda na kuendesha shughuli za kutafuta chakula msituni.

Mwandishi Zainab Aziz/RTRE

Mhariri:Josephat Charo

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW