Merkel akabiliwa na changamoto uchaguzi NRW
13 Mei 2012Uchaguzi huo ambao umeitishwa na mapema unaweza kutoa msukumo kwa mahasimu wakubwa kansela wakati huu wa kuelekea katika uchaguzi wa kitaifa mwaka 2013.
Wiki moja baada ya wapiga kura nchini Ugiriki na Ufaransa kukataa sera za kubana matumizi, raia wa jimbo la North Rhine Westphalia (NRW) huenda wakawaadhibu wahafidhina ambao wamekuwa wakipigia upatu sera za kubana matumizi.
Kiasi ya wapiga kura milioni 13.2 , ikiwa ni sehemu ya tano ya wapiga kura wote kitaifa , wanachagua bunge jipya la jimbo, katika jimbo hilo la magharibi ya Ujerumani ambalo lina viwanda vingi.
NRW ushawishi kitaifa
Jimbo hilo kihistoria linanafasi kubwa katika siasa za shirikisho, ambapo mwaka 2005 , chama cha kansela wa wakati huo Gerhard Schroeder kilipoteza uchaguzi na kumlazimisha kuitisha uchaguzi wa shirikisho wa mapema na ndipo kansela Angela Merkel akaingia madarakani.
Chama cha kihafidhina cha kansela Angela Merkel cha Christian Democratic Union, CDU, kinapambana kukamata jimbo hilo kutoka kwa muungano unaoundwa na vyama vya mrengo wa shoto vya Social Democratic SPD na kile cha kijani.
Uchunguzi wa maoni
Licha ya uchunguzi wa maoni ya wapiga kura kuwa unaonyesha mara kwa mara kuwa chama cha Merkel kinaungwa mkono na wapiga kura wengi kwa msimamo wake wa kubana matumzi katika bara la Ulaya , chama cha CDU kiko nyuma ya SPD kwa alama sita hadi saba katika maoni ya wapiga kura katika jimbo la NRW.
Maoni ya wapiga kura yanaonesha kuwa mgombea wa chama cha SPD, waziri mkuu wa jimbo hilo Hannelore Kraft, huenda akaunda serikali pamoja na chama cha kijani, na tofauti na mara iliyopita , atapata wingi wa kutosha.
Uchaguzi huo uliitishwa baada ya serikali yake iliyokuwa ikitawala mbali ya kuwa na wingi mdogo bungeni , bila kutarajiwa ilianguka wakati bunge la jimbo hilo liliposhindwa kupitisha mswada wa bajeti baada ya kuwapo madarakani kwa muda wa miezi 22 tu
FDP chafufua matumaini
Washiriki wa Merkel kitaifa , chama cha FDP , kimepanda kwa mujibu wa maoni ya wapiga kura yaliyokusanywa yakimuunga mkono mgombea wa chama hicho Christian Lindner.
Mwaka jana na mapema mwaka huu chama cha FDP kimeshindwa kwa kudhalilika kupata kura za kutosha kuweza kuingia katika mabunge ya majimbo sita. Merkel amekana kuwa ushirika wake na chama cha FDP kitaifa utaathirika kutokana na matokeo ya uchaguzi huo.
Uchaguzi huo wa Jumapili ni uchaguzi muhimu kwa jimbo la North Rhine Westphalia basi, Merkel ameliambia gazeti la Ruhr Nachrichten wiki hii.
Lakini chini ya kichwa cha habari , kinachosema , "ni muda gani zaidi", gazeti la Die Zeit limedokeza kuwa uchaguzi wa NRW unaweza kuwa siku ya maangamizi kwa kansela Merkel.
Angela Merkel yuko katika kilele cha wakati wake wa madaraka, na anatambua kuwa kwa sasa hali ni ngumu, gazeti hilo limesema. Anayekabiliana na waziri mkuu Kraft ni mgombea wa chama cha CDU , Norbert Roettgen , ambaye ni waziri wa mazingira wa serikali ya kansela Merkel , ambaye kampeni yake iliyogubikwa na makosa kadha , ililenga katika kubana matumizi.
Chama kingine ambacho kinapaswa kutupiwa macho ni chama kipya cha Pirate, ambacho kimeingia hivi sasa katika mabunge ya majimbo matatu tangu mwezi Septemba kwa kunadi sera za uwazi katika hatua za kisiasa na uhuru katika mtandao wa internet.
Mwandishi : Sekione Kitojo/ AFPE
Mhariri: Amina , Mjahid