1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan Kusini

Mgogoro bado unaendelea kuitikisa Sudan Kusini

28 Februari 2023

Wataalam wasema vita bado vinaendelea Sudan Kusini, nusu muongo tangu viongozi wake walipotangaza mwisho wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyowaua watu 380,000.

Südsudan, Juba | Soldaten bereitet sich auf ihre Abschlussfeier vor
Picha: Waakhe Simon Wude/DW

Wakati Sudan Kusini ilipokuwa ikisubiri ziara ya kihistoria ya kiongozi wa kanisa Katoliki ulimwenguni Papa Francis, serikali ilitoa taarifa iliyokusudia kuwahakikishia wageni kwamba kuna utulivu. Mstari wa kwanza wa taarifa hiyo ilisema "Sudan Kusini ni mahali pa amani.”

Lakini siku yake ya kwanza Juba, wakati kiongozi huyo alipowapungia mkono waumini, kaburi la pamoja lilikuwa linachimbwa umbali wa kilomita 100 kwa ajili ya raia 27 waliouawa kwa risasi wakati wa mapambano.

Papa Francis akamilisha ziara yake nchini Sudan Kusini na amehimiza juu ya kukomeshwa chuki na ghasia.

Tukio hilo la kuuawa kwa watu linaonyesha ukweli unaohuzunisha nchini Sudan Kusini kwamba licha ya uhakikisho wa serikali na vilevile licha ya mabilioni ya dola kutumika kwenye juhudi za kulinda amani, sheria na utaratibu. Juhudi hizo huenda zaidi ya mji mkuu kwa nadra sana.

Rais Salva Kiir na mpinzani wake Riek Machar waliunda serikali ya mpito na walijitolea kuunganisha vikosi vyao kuwa jeshi moja kwa lengo la kuwalinda raia wao ambao wameteseka kwa muda mrefu. Kiir na Machar waliahidi amani na maendeleo Sudan Kusini. Lakini hilo halijafanikiwa. Badala yake vurugu za kutisha bado zinaendelea kiholela.

Kiongozi wa kanisa Katoliki ulimwenguni Papa Francis akikabidhiwa shada la maua ya mtoto kama sehemu ya makaribisho alipozuru Juba Februari 3, 2023.Picha: VATICAN MEDIA/AFP

Miongoni mwa visa vya uhalifu ambao vilivyolishuhudiwa kwenye vita vya kati ya mwaka 2013 na 2018, ni pamoja na utumwa wa kingono na njaa iliyokusudiwa. Wataalamu wanasema hata leo, kadhia hizo bado zinaendelea kutokea.

Mtaalamu wa wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Barney Afako aliwaambia waandishi habari baada ya kuzuru Sudan Kusini mwezi Februari kwamba kuhusiana na machafuko nchini humo, hawaoni mabadiliko na kwamba, japo mji wa Juba ni salama, kuna wasiwasi kuhusu yanayoendelea nje ya Juba.

Mwezi uliopita, Umoja wa Mataifa ulionya kuwa vikosi vyenye silaha viliendelea kujipanga upya katika jimbo la Upper Nile, ambapo kumekuwa na mashambulizi ya makombora na roketi dhidi ya vijiji katika operesheni kubwa zinazohusisha maelfu ya wanajeshi.

Machafuko ya kikabila yashamiri Jonglei na Greater Pibor

Huko Jonglei na Greater Pibor, katika miezi ya hivi karibuni, vijana wenye silaha nzito wamefanya mashambulizi ambayo yamesababisha maafa huku wakiwalenga wapinzani wao wa kikabila.

Vurugu zimeendelea Sudan Kusini licha ya mkataba wa amani

Katika maeneo mengine yasiyokuwa na utulivu, idadi isiyojulikana ya raia wameuawa katika mapigano ya kulipiza kisasi.

Maelfu ya watu wamekimbilia kambi za Umoja wa Mataifa kwa ajili ya ulinzi mnamo wakati kuna mzozo mbaya zaidi wa wakimbizi barani Afrika.

Wataalam wasema japo mapigano makubwa baina ya vikosi vya Kiir na Machar vimepungua, ghasia zimeongezeka miongoni mwa makundi mengine.Picha: Samir Bol/ZUMAPRESS/picture alliance

Lakini wachunguzi wanasema serikali imefeli kulinda raia hapo awali na askari wao wamekuwa moja kwa moja wakihusika na ghasia.

Wataalam wanasema ghasia zimeongezeka hata wakati mapigano makubwa kati ya vikosi vya Kiir na Machar vimepungua tangu makubaliano ya amani.

Hata kambi ambako watu wamekuwa wakikimbilia zimekuwa zikishambuliwa. Ken Scott, kamishna wa zamani wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Sudan Kusini, na mshauri wa  kampuni ya sheria (Global Rights Compliance), inayoitaka mahakama ya kimataifa ya uhalifu The Hague kuwachunguza maafisa wakuu nchini humo kwa uhalifu wa kivita, amesema anadhani wale wanaodai kwamba vita vya wenyewe kwa wenyewe vimeisha Sudan Kusini wanakosea, kwani kulingana naye mgogoro unaendelea kwa njia nyingine".

Wakati wa ziara yake, Papa Francis alilalamika juu ya "ukosefu wa usalama endelevu" na ahadi "zisizotimizwa" za amani nchini humo.

(Chanzo: AFPE)