1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miaka 10 tangu vuguvugu la maandamano nchini Yemen

10 Februari 2021

Vuguvugu la maandamano yalioshuhudiwa katika nchi za kiarabu wakati wa msimu wa machipuko nchini Yemen yalisababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vimesababisha mateso makubwa kwa watu wa nchi hiyo.

Arabischer Frühling in Jemen - 10 Jahre seit der Revolution
Picha: Suhaib Salem/REUTERS

''Siku za mwanzo zilikuwa nzuri: Tulikutana katika uwanja wa Tahriri na kufurahi kukutana na watu waliokuwa na maono sawa,'' anasema Reem Jarhum huku akikumbuka mwanzo wa vuguvugu hilo katika mji mkuu wa Yemen, Sana'a. Ni miaka 10 tangu Jarhum ambaye sasa ana umri wa miaka 32, rafiki zake na vijana wengine nchini humo kuanza kutoa wito wa mabadiliko.

Wakati huo, mbabe Ali Abdullah Saleh alikuwa uongozini tangu mwaka 1978 hadi mnamo mwezi Mei mwaka 1990 kama rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Yemen na kutokea hapo kama rais wa Yemen. Kwa ujumla aliongoza kwa miaka 33 ikiwa ni mwaka mmoja zaidi ya rais wa Misri Hosni Mubarak aliyondolewa mamlakani mnamo mwezi Februari 11 mwaka 2011 wakati mapinduzi wa Yemen yalikuwa yakiendelea. Jarhum anakumbuka kuwa ni kuondolewa kwa Mubarak ndiko kulikotoa muongozo kwa raia wa Yemen na kile ambacho tayari kilikuwa kimeanza kupitia mtandao wa Facebook kilipelekwa barabarani.

Kiini cha mapinduzi

Mwanaharakati wa kijamii Tawakkol Karman pia alikuwa katika eneo hilo, ijapokuwa haikuwa mara ya kwanza kushiriki katika maandamano hayo. Karman ambaye sasa ana umri wa miaka 42 amepewa jina la utani '' Mama wa mapinduzi.'' Amekuwa akiandamana dhidi ya ufisadi tangu mwaka 2007. Kila wakati alisisitiza kuhusu mazungumzo ya amani na serikali licha ya mashambulizi ya mara kwa mara ya serikali hiyo ya gesi za kutoa machozi na msako wa vurugu kutoka kwa polisi dhidi ya waandamanaji wa wadogo.

Baadaye mnamo mwaka 2011 alishinda tuzo ya amani ya Nebel pamoja na mwanaharakati wa amani wa Liberia Ellen Johnson Sirleaf na Leymah Gbowee kama mwanamke wa kwanza wa kiarabu na kutoka Yemen kufanya hivyo. Alishinda tuzo hilo kwa jukumu lake la uongozi katika harakati za kutetea haki za wanawake na kwa demokrasia na amani nchini Yemen.

Katika mahajiano na shirima la habari la Reuters, Karman alikumbuka kuwa baada ya mapinduzi, waliishi maisha mazuri yaliodumu miaka mitatu na kwamba zilikuwa zimesalia siku chache za kufanya kura ya maamuzi na kuandaa chaguzi kadhaa. Lakini kile kilichoanza kama azma ya amani ya mabadiliko kwa kuimba na kucheza katika uwanja huo pamoja na kujiuzulu kwa Ali Abdullah mnamo Februari 25, 2012, kumegeuka kuwa mzozo mbaya zaidi wa kibinadamu duniani.

Kulingana na shirika linalowashughulikia wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR, asilimia 80 ya idadi ya watu takriban milioni 30 sasa inahitaji msaada, watu milioni 20 wanakabiliwa na uhaba wa chakula na zaidi ya watu laki moja wameuawa.

Hali ya kudorora

Mwanajeshi muasi wa serikali ya rais Ali Abdullah Saleh ajeruhiwa katika maandamano ya 2011, YemenPicha: picture alliance/dpa

Hali tete ambayo imedumu kwa muda wa miaka 10 huku sasa ikighubikwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe, ilianza kwa kushindwa kisiasa kwa mrithi wa Ali Abdullah Saleh, Abed Rabbo Mansour Hadi ambaye kama rais aliyekuwepo, hakuwa na majibu kwa ufisadi, ukosefu wa ajira na uhaba wa chakula.

Hali ilifanya kuwa mbaya zaidi na mashambulizi ya itikadi kali katika eneo la Kusini na ukweli kwamba maafisa wa usalama walibaki kuwa watiifu kwa aliyekuwa rais Saleh. Kwa kuongezea katika hali hiyo, vuguvugu la Kihouthi lililoanza kutoka kwa jamii ya walio wachache ya Kishia na kuungwa mkono na uongozi wa kishia katika kanda hiyo, Iran, lilithibiti eneo la Kaskazini mwa nchi hiyo. Kundi hilo la Kihouthi liliungwa mkono na raia wa Yemen waliokata tamaa wakati walipouteka mji wa Sana'a mwishoni mwa mwaka 2014.

Ahadi ya Biden yaleta matumaini

Marekani chini ya uongozi wa Barack Obama na Donald Trump limekuwa moja ya mataifa ambayo yamehusika kwa njia isiyokuwa ya moja kwa moja katika vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Yemen. Uongozi wa Barack Obama uliidhinisha kampeini ya mashambulizi ya kutoka angani yaliyoongozwa na Saudi Arabia dhidi ya waasi wa Kihouthi mnamo mwaka 2015.

Rais wa Marekani - Joe BidenPicha: Doug Mills/UPI/Imago Images

Lakini baada ya takriban miaka 7 ya mapigano, serikali mpya chini ya uongozi wa Joe Biden sasa imetangaza mabadiliko makubwa. Katika tangazo lake la kwanza kubwa kuhusu sera za kigeni mnamo Februari 4, rais Biden alisema, '' Vita hivi lazima viishe,'' na kuongeza, '' Kusisitiza kujitolea kwetu, tunatamatisha usaidizi wote wa Marekani wa operesheni za mashambulizi katika vita nchini Yemen ikiwa ni pamoja na uuzaji wa silaha.'' Biden pia alivitaja vita hivyo kuwa janga la kibinadamu na kimkakati. Hata hivyo, kusitishwa kwa uuzaji wa silaha hakujumuishi zile zinazotumika kupigana na na kundi la wanamgambo la al-Qaida.

Hata hivyo, wachambuzi wa siasa wanaamini kuwa uteuzi wa mjumbe wa Marekani na mtaalamu wa masuala ya Mashariki ya Kati Timothy Lenderking kama mjumbe maalumu nchini Yemen ni hatua muhimu zaidi katika kutafuta amani.

Mateso lakini bila majuto

Huenda ikaja kama hatua ya kushangaza kwamba licha ya vifo zaidi ya laki moja wakati wa vita hivyo, mateso yaliosababishwa na magonjwa mengi kama vile kipindupindu na COVID-19 na baa la njaa katika muda wa zaidi ya miaka 10 iliyopita, vuguvugu hilo la maandamano nchini humo la mwaka 2011 halichukuliwi kwa hasira.

Mwenyekiti na mwanzilishaji mwenza wa kituo cha elimu ya kimkakati ya Sana'a na mwanachama wa taasisi ya utafiti wa masuala ya kimataifa ya Chatham House yenye makao yake mjini London, Farea Al-Muslimi, ameliambia shirika la DW kwamba wasifu wao umebadilika  na kwamba huo ndio mwaka uliobadilisha ufahamu wao kuhusu uongozi.

Huku raia wa nchi hiyo wakipata mateso katika viwango tofauti, ni vigumu kufikiria kuhusu vuguvugu lengine la kutetea demokrasia nchini humo kwa sasa.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW