1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Scholz: Bado tunakabiliwa na changamoto kwenye muungano

Angela Mdungu
3 Oktoba 2024

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz amesema muungano wa nchi hiyo umepiga hatua licha ya kuwa bado unakabiliwa na changamoto kadhaa. Ameyasema hayo wakati wa maadhimisho ya miaka 34 ya muungano wa nchi hiyo.

Olaf Scholz
Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz katika maashimisho ya Muungano wa Ujerumani 03.10.2024 Picha: Chris Emil Janßen/Pool/Getty Images

Akihutubia wakati wa maadhimisho hayo ya kuungana kwa iliyokuwa Ujerumani Mashariki na Ujerumani Magharibi, Scholz ameelezea namna taifa hilo linavyofanya maadhimisho hayo huku likikabiliwa ugumu katika na mapambano dhidi ya itikadi kali na siasa kali za kizalendo. Ameweka wazi kuwa si Ujerumani mashariki pekee ambako karibu robo tatu ya wapiga kura wanawachagua viongozi wenye siasa kali.

Soma zaidi:Ujerumani inaadhimisha miaka 34 ya muungano

Licha ya changamoto hizo ameongeza kuwa hakuna taifa lililowahi kukabiliwa na changamoto kama ya Ujerumani ya kuunganisha jamii kutoka pande mbili kubwa zilizokuwa zimetenganishwa kwa zaidi ya miongo minne zilizokuwa na taratibu tofauti za kiuchumi, kisiasa, na hata kiakili.

Zaidi Kansela Scholz amezungumzia hatua kubwa iliyopigwa katika kupunguza pengo kati ya pande mbili za taifa hilo na kusema kuwa, "Tofauti kati ya Mashariki na Magharibi siyo kigezo tena, hasa kwa vijana wa Ujerumani, wakati huohuo, kiwango cha watu kuridhishwa na maisha katika pande zote kimekuwa na uwiano kwa kiasi kikubwa. Kampuni nyingi za kimataifa za teknolojia sasa zinaanza kupeleka shughuli zake Ujerumani Mashariki."

Scholz amesisitiza kuwa kuna haja ya kuwa na uwiano zaidi wa hali ya maisha kati ya eneo la mashariki na magharibi mwa Ujerumani. Licha ya hilo Kansela uyo wa Ujerumani ametahadharisha kuwa, wazo la muungano wa Ujerumani linaweza kukamilika kutakapokuwa na usawa kati ya pande hizo mbili.

Maelfu wajitukeza maandamano ya Muungano wa kupinga vita

Wakati huohuo, maelfu ya wafuasi wa Muungano unaopinga vita wamefanya maandamano katikati mwa Berlin wakati Ujerumaniikisherehekea miaka 34 tangu muungano wa pande mbili za nchi hiyo.

Maandamano ya kupinga vita mjini Berlin 03.10.2024Picha: Sebastian Gollnow/dpa/picture alliance

Waandamanaji hao wameonekana wakiwa wamebeba mabango yanayotoa wito wa kutumia diplomasia badala ya vita na kusitisha upelekaji silaha Ukraine.

Maafisa takriban 1,000 wa polisi wamesambazwa Berlin ili kuhakikisha usalama atika maandamano hayo. 

Kulingana na taarifa ya polisi, maandamano hayo yamehudhuriwa na karibu watu 10,000 huku waandaaji wakidai kuwa watu 30,000 wameshiriki. 

Baadhi ya waandamanajiwamieonesha mshikamano na Ukanda wa Gaza kwa kushikilia mabango yaliyoandikwa "Mwisho wa vitisho na ukaliaji wa maeneo kimabavu", na "NATO inachochea vita na mauaji ya kimbari".