Michuano ya ligi za ndani barani Afrika (CHAN) yaanza
2 Agosti 2025
Mchezo huo wa kwanza kabisa wa michuano hii, inayoandaliwa kwa pamoja na mataifa ya Kenya,Tanzania na Uganda, utachezwa muda wa saa mbili usiku kwa saa za Afrika mashariki na unatarajiwa kushuhudiwa na maelfu ya mashabiki watakaofika uwanjani na wale watakaofuatilia kwenye televisheni.
Mchezo huo utatanguliwa na sherehe za ufunguzi wa michuano hiyo na mgeni rasmi atakuwa Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa. Michuano hii ya CHAN inashirikisha jumla ya mataifa 19 ambapo kundi A linaundwa na mataifa ya, Kenya, Morocco, Angola, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Zambia.
Tanzania ipo kwenye kundi B pamoja na Madagascar, Burkina Faso, Mauritania na Afrika ya Kati. Uganda, Niger, Guinea, Algeria na Afrika kusini ziko kwenye kundi C na kwenye kundi D zipo Senegal, Nigeria, Congo na Sudan .
Fainali ya michuano hii itafanyika Agosti 30 katika uwanja wa Kasarani nchini Kenya.