1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miito yahanikiza Tanzania kumuachia Freeman Mbowe

George Njogopa26 Julai 2021

Bado kumekuwa na kitendawili kuhusu hatma ya mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania Chadema, Freeman Mbowe ambaye yuko mikononi mwa polisi tangu wiki iliyopita. Miito inazidi kutolewa kutaka aachiwe.

Tansania Opposition Freeman Mbowe
Picha: Ericky Boniphace/AFP/Getty Images

Jeshi la polisi hadi sasa halijatoa taarifa yoyote wala kutoa tamko lingine kuhusu sakata hilo mbali na taarifa yake ya mwisho iliyoonesha kwamba, Mbowe aliletwa Dar es Salaam akitokea Mwanza na anatuhumiwa kwa makosa ya ugaidi  makosa ambayo yanafanya makundi ya watu kugawika kimaoni kutokana na tuhuma hizo.

Katika ujumbe wake aliotuma kwa wanachama wake kupitia kwa familia yake, Mbowe amesema licha ya yale anayopitia bado hatavunjika moyo na juhudi zake za kisiasa.

James Mbowe ambaye ni mmoja wa wanafamilia wake, amesema Mbowe ameonekana kuwatia moyo wale wanaoendesha vuguvugu la kudai katiba mpya kutorudi nyuma.

Jeshi la polisi mpaka sasa halijamfikisha mahakamani Mbowe tangu alipokamatwa wiki iliyopita.Picha: DW/S. Khamis

Chama chake Chadema kimelaani hatua ya kuendelea kushikiliwa kwa kiongozi huyo na kulingana na mkurugenzi wa itifaki ya mambo ya nje wa chama hicho, John Mrema ameimbia DW kuwa Mbowe anajisikia vibaya kiafya.

Mbowe aliletwa jijini Dar es salam mwishoni mwa wiki akiwa na viongozi wengine kadhaa waliokamatwa jijini Mwanza, lakini viongozi hao wengine wameachiwa wakati yeye akiendelea kushikiliwa na jeshi hilo.

Chama cha wanasheria chaungana na wanaotoa miito ya kuachiwa Mbowe

Tangu kukamatwa kwake kwa tuhuma zinazomkabili, kumekuwa na miito inayoendelea kutolewa ikitaka kuachiwa kwake huru au afikishwe mahakamani.

Miongoni mwa walijitokeza kuzungumzia sakata hilo, ni pamoja na chama cha wanasheria cha Tanganyika Law Society kilicholaani tukio hilo, kikisema limefanywa kinyume na katiba ya nchi.

Rais wa chama hicho Dokta Edward Hoseah katika ujumbe wake aliotuma kwa njia ya mtandao wa kijamii amesema msimamo kamili wa TLS utatolewa baada ya baraza la uongozi kukutana na kujadili jambo hilo.

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliahidi kuruhusu shughuli za kisiasa kuendelea baada ya mtangulizi wake John Magufuli kuzipiga marufuku. Lakini pia aliwataka wanasiasa kuwa wavumilivu kuhusu suala la katiba.Picha: AP Photo/picture alliance

Wakati hayo yakiendelea hivi, familia ya Mbowe imetoa ombi la kumwachia kiongozi huyo ili apate kushiriki maziko ya baba yake mdogo yanayotazamiwa kufanyika siku ya Jumatano, Machame Moshi.

Mbowe alitiwa mbaroni na jeshi la polisi wakati akiwa katika maandalizi ya mwishomwisho kuongoza kongamano la kudai katiba mpya lililopangwa kufanyika jijini Mwanza.

Katika kipindi cha wiki kadhaa chama hicho kimekuwa kikiendesha makongamano ya ndani katika maeneo mbalimbali nchini kwa ajenda hiyo hiyo moja ya kuamsha vuguvugu la mabadiliko ya katiba.

Suala la katiba mpya ni hoja inayoendelea kutawala vinywani mwa wapinzani wanaodai kuwa katiba ya sasa haitoi uwanja sawa wa ushindani wa kisiasa na chama tawala CCM.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW