Mitaro yaangamiza makaazi katika maeneo mbalimbali Kongo
21 Septemba 2025
Mitaro mikubwa imeenea kama makovu katika miji ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Utafiti uliochapishwa na kundi la watafiti wa kimataifa mwezi Agosti umechora ramani ya mitaro hii kwa mara ya kwanza nchini Kongo — na kubaini takriban mianzi 3,000.
Kiwango cha tishio hili ni cha kutisha. Kuanzia mwaka 2004 hadi 2023, inakadiriwa kuwa karibu watu 120,000 wamefurushwa makazi yao kutokana na mitaro ya mijini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Wanasayansi wanatahadharisha kuwa mamia ya maelfu zaidi wanaweza kupoteza makazi yao katika kipindi cha miaka kumi ijayo. Kwa mamilioni ya watu wanaishi katika maeneo yenye hatari kuelewa mianzi hii ni jambo la msingi.
Lakini mitaro ni nini hasa?
Mitaro ni aina kali ya mmomonyoko wa ardhi. Ni mifereji mikubwa inayochongwa na maji, na inaweza kuwa na upana wa zaidi ya mita kadhaa na urefu wa mamia ya mita. Katika miji, mianzi ni tishio linalokua ambalo huishia kumeza nyumba, biashara, na miundombinu mingine kama barabara na reli.
Ili kuifuatilia, watafiti walichanganya takwimu za msongamano wa watu na picha za setilaiti, wakilinganisha na picha za anga zilizopigwa miaka ya 1950. Waligundua kuwa zaidi ya nusu ya miji iliyochunguzwa imeathirika. Karibu katika kila kisa, mitaro imeongezeka katika kipindi cha miaka kumi iliyopita.
Mitaro huundwa vipi?
Sababu za asili na zile zinazotokana na shughuli za binadamu huchangia kuundwa kwa korongo. Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, mvua kubwa na udongo unaosombwa kwa urahisi huungana na ukuaji wa haraka wa miji na ukosefu wa mipango bora ya miji, na kugeuza maji kuwa mtiririko wa uharibifu.
"Sababu kuu zinazochochea hali hii ni mapungufu na dosari katika mipango ya miji na usimamizi wa matumizi ya ardhi,” alisema Guy Ilombe Mawe, mwandishi wa utafiti na mtafiti kutoka Chuo Kikuu cha Bukavu. Ukuaji wa haraka wa miji nchini Kongo umeacha jamii bila mifumo ya kutosha ya mifereji ya maji.
Kinshasa, jiji la tatu kwa ukubwa barani Afrika, limeathirika sana likiwa na zaidi ya korongo 800. Mwaka 1950, lilikuwa na wakazi wapatao 200,000. Leo, karibu watu milioni 18 wanaishi humo.
"Kongo ni miongoni mwa nchi ambazo miji inakua kwa kasi sana" alieleza Matthias Vanmaercke, mwandishi wa utafiti kutoka KU Leuven nchini Ubelgiji. "Sehemu kubwa ya ukuaji huu wa miji hauna mpangilio, ni wa fujo... watu wanapojenga nyumba, mara nyingi huwa bila miundombinu sahihi ya kudhibiti maji," Vanmaercke aliambia DW.
Ukuaji wa miji huambatana na ukataji miti. Paa za nyumba, barabara, na nyuso nyingine zilizofunikwa huchukua nafasi ya mimea. Hii huacha ardhi ndogo yenye uwezo wa kufyonza maji. Utafiti ulibaini kuwa asilimia 98 ya mianzi ya mijini inahusiana moja kwa moja na mtandao wa barabara za maeneo husika.
Mitaro mara nyingi hutokea katika maeneo yenye udongo wa mchanga unaoathirika kwa urahisi. Mvua kubwa pia huchangia na inaweza kupanua mianzi iliyokwisha kuundwa. Kwa kuwa mabadiliko ya tabianchi yanatarajiwa kuongeza mvua, wanasayansi wanatahadharisha kuwa hatari inaendelea kukua.
Je, mitaro ni sawa na maporomoko ya ardhi?
Sivyo kabisa. Ingawa yote ni ya kuharibu, mitaro na maporomoko ya ardhi yana tofauti muhimu. Mitaro hupatikana hasa pembezoni mwa nyanda za juu zenye udongo wa mchanga, ilhali maporomoko ya ardhi hutokea katika maeneo ya milima yenye miteremko mikali na udongo wa mfinyanzi.
Vyote vinaweza kutokea bila kutarajiwa. Lakini kuna tofauti muhimu — mara mitaro inapojitokeza, huwa ya kudumu na huendelea kukua kila mvua inaponyesha. Hii ni hatari zaidi mijini, ambako nyumba huwa katika hatari ya kuharibiwa kila wakati.
"Mitaro inaweza kuundwa haraka sana ndani ya tukio moja la mvua, na mara nyingi huwa hatari kwa sababu watu hawatarajii — ghafla kuna pengo kubwa linaloharibu nyumba zao," alisema Vanmaercke. "Lakini pia, mara mitaro inapojitokeza, husalia hapo, na kila mvua mpya huongeza mtiririko wa maji ndani ya pengo hilo."
Nani yuko katika hatari ya mitaro ya mijini?
Mitaro ya mijini ni tishio kwa miji kote barani Afrika na katika maeneo kama Brazil. Tangu mwaka 2020, korongo zimekuwa zikiongezeka kwa kasi, mara nyingi kwa madhara makubwa katika maeneo yenye msongamano mkubwa wa watu. Kupitia Google Earth, unaweza kuona jinsi korongo zinavyopanuka kwa muda katika miji ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Jamii maskini ndizo zilizo hatarini zaidi. "Idadi ya watu wanaoishi katika maeneo haya yaliyo wazi inaendelea kuongezeka kwa msongamano kadri muda unavyopita [...] licha ya hatari iliyopo, wakaazi wanaonekana kutokuwa na chaguo," alieleza Mawe.
Kwa mujibu wa watafiti, watu wapatao 12,000 nchini Kongo wako katika hatari ya kupoteza makazi yao kila mwaka, ambapo takriban asilimia 60 ya uhamishaji unasababishwa na upanuzi wa mitaro badala ya mitaro mipya kuundwa.
"Watu wanaoishi pembezoni mwa korongo hujikuta wakihatarishwa zaidi, mita moja baada ya nyingine," alisema Vanmaercke. Anaelezea athari za kisaikolojia kwa kusema kuwa watu hubaki macho usiku katika nyumba zao "kila mvua inaponyesha, wakitumaini tu kwamba haitaiharibu nyumba yao."
Je, mitaro inaweza kutabiriwa?
Bado haijafikia hapo. Wanasayansi wanasema ni vigumu kutabiri mitaro itatokea wapi au lini, lakini ni muhimu sana katika kuzuia uharibifu zaidi.
Watafiti wanaendelea kuchunguza kwa kina jinsi mitaro inavyoundwa na kutafuta suluhisho. "Mojawapo ya malengo yetu ni kuunda mifumo ya tahadhari ya mapema na [...] kutuma onyo kama vile: ‘usiku huu kutakuwa hatari sana, jaribu kutafuta hifadhi sehemu nyingine," alisema Vanmaercke.
Nini kinaweza kufanyika?
Kudhibiti mitaro ni gharama kubwa — kurekebisha moja tu kunaweza kugharimu zaidi ya dola milioni moja (€920,000). Hali hii huzilazimu jamii za mitaa kuchukua hatua peke yao.
"Kuna juhudi za kijamii zinazolenga kuzuia upanuzi wa mitaro," alisema Mawe. Aliiambia DW kuwa juhudi hizo zinajumuisha "kupanda mianzi na mimea mingine ili kuimarisha udongo, kuweka mifuko ya mchanga kwenye kichwa cha mtaro na kuchimba mashimo au wakati mwingine kufunga matanki ya maji ndani ya viwanja ili kuhifadhi maji ya mvua."
Hata hivyo, kwa mujibu wa Mawe, juhudi hizi mara nyingi hazitoshi na hazifanikiwi kuzuia upanuzi wa mitaro.
"Nadhani jambo la kutisha zaidi ni kwamba, mara unapokuwa unaishi karibu na mitaro, unajikuta umekwama [...] kwa sababu pia thamani ya ardhi hushuka kwa kiwango kikubwa," alisema Vanmaercke.
Hatua bora zaidi, wanasisitiza, ni kupunguza kiasi cha maji kinachoingia kwenye mitaro tangu mwanzo. Kwa watu wanaoishi pembezoni mwa mitaro, kila mvua kubwa huleta hatari ya kupoteza makazi yao.
(Mwandishi: Amy Stockdale)