Mkutano wa Munich waiacha Afrika pembezoni
16 Februari 2026
Mkutano wa Usalama wa Munich umefungwa kwa hitimisho moja: dunia haina utulivu kuliko wakati mwingine wowote, na Ulaya haina tena nafasi ya kusubiri.
Kwa siku tatu, majadiliano yameongozwa na vita nchini Ukraine, suala la msaada wa kijeshi wa Magharibi kwa Kyiv na hofu ya kupungua kwa msukumo wa kisiasa, hususan kutoka Marekani. Mada nyingine iliyotawala ni mgogoro wa Mashariki ya Kati, huku kukiwa na wito wa mara kwa mara wa kuzuia kuenea kwa vita katika eneo zima.
Ujerumani inataka msimamo wa kimataifa ulio thabiti zaidi
Lakini Munich pia imekuwa jukwaa la mjadala mpana kuhusu mustakabali wa kimkakati wa bara la Ulaya: ulinzi wa pamoja, kujiongezea silaha, usalama wa mtandaoni, na mapambano dhidi ya uingiliaji wa mataifa ya kigeni.
China na ushawishi wake wa kiuchumi na kijeshi pia vimekuwa mada katika vikao vingi, pamoja na kuongezeka kwa tawala za kiimla na udhaifu wa demokrasia.
Ni katika muktadha huo ndio Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz amesema Ujerumani itakuwa na msimamo thabiti zaidi katika jukwaa la kimataifa.
"Tumeelewa kwamba katika zama za mataifa makubwa yenye nguvu, uhuru wetu sio salama tena: uko hatarini. zitahitajika nguvu na dhamira ya kweli ili kuutetea uhuru huo", alisema Merz.
Nafasi ndogo ya Afrika katika majadiliano?
Wajumbe wachache kutoka Afrika walihudhuria, lakini mijadala haikuzingatia kwa kina migogoro ya bara hilo, kama Sudan, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo au ukanda wa Sahel. Jambo ambalo limekosolewa vikali na Zerbo Lassina, Waziri Mkuu wa zamani wa Burkina Faso.
"Ningependa kuona watu wengi zaidi kutoka Sahel wakishiriki katika majadiliano. Ni muhimu kuzijumuisha nchi tatu za Sahel katika mijadala ya aina hii kama Mkutano wa Usalama wa Munich. Hilo pia linawezesha kusikia mtazamo wao. Ni jambo la muhimu sana", alisisitiza Lassina.
Lakini Waziri wa Mambo ya Ndani wa Rwanda, Vincent Biruta anaamini kuwa kutawala kwa mada za kimataifa kwenye mkutano huo wa Munich ni jambo la kawaida.
"Kwa vyovyote vile, haya ni migogoro inayotokea kwingine lakini inatuathiri. Vita nchini Ukraine vimetuathiri hata kama tuko mbali. Kwa hiyo ni muhimu pia sisi Waafrika kufuatilia mijadala hii na kuelewa vizuri zaidi changamoto zilizopo", alisema Biruta.
Hata hivyo mkutano wa Munich 2026 umethibitisha jambo moja: usalama wa dunia unayumbayumba na hakuna aliye salama.