1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa G8; suala la Syria lagubika mkutano

18 Juni 2013

Vita nchini Syria vimetawala mwanzoni mwa mkutano wa mataifa ya G8 nchini Ireland ya kaskazini Jumatatu(17.06.2013)wakati viongozi wa mataifa ya magharibi wakiongeza mbinyo kwa Urusi kuacha kumuunga mkono rais Assad.

U.S. President Barack Obama (L) meets with Russian President Vladimir Putin during the G8 Summit at Lough Erne in Enniskillen, Northern Ireland June 17, 2013. REUTERS/Kevin Lamarque (NORTHERN IRELAND - Tags: POLITICS TPX IMAGES OF THE DAY)--eingestellt von haz
Rais Obama na rais Putin katika mkutano na waandishi habariPicha: Reuters

Urusi imepuuzia uvumi kuwa mataifa ya magharibi yanajaribu kuweka eneo ambalo ndege hazitaruhusiwa kuruka nchini Syria kusaidia majeshi ya waasi kupambana na majeshi ya Assad wakati waziri mkuu David Cameron anatoa msukumo wa kuweza kupiga hatua katika kufanyika mkutano wa amani.

Kwa upande mwingine Umoja wa Ulaya na Marekani zimetangaza hatua za mwanzo za majadiliano kuhusiana na mkataba mkubwa wa kimataifa wa eneo la biashara huru, katika jitihada za kuimarisha ukuaji wa uchumi na kutengeneza nafasi za kazi katika uchumi wa dunia unaolega lega.

David Cameron na rais Putin katika mkutano wa G8Picha: Reuters

Lakini mtazamo ulielekezwa zaidi katika mazungumzo tete kuhusu Syria kati ya rais Vladimr Putin na Barack Obama wa Marekani katika eneo la kupendeza lenye uwanja wa kuchezea golf katika ukingo wa mto Lough Erne.

Msaada wa Marekani

Tangu pale Marekani ilipotangaza rasmi kuwa itawapatia msaada wa kijeshi waasi nchini Syria baada ya kugundua kuwa serikali inatumia silaha za kemikali , Obama na Putin sasa wanatoa msaada kwa pande zinazopingana katika vita hivyo.

Putin akiwa katika mkutano wa G8 Ireland ya kaskaziniPicha: picture alliance/Photoshot

Cameron ametaka mkutano huo kulenga katika juhudi za kupambana na wakwepa kodi na kulazimisha makampuni makubwa duniani kuwa wazi zaidi, lakini mzozo unaozidi kuleta maafa nchini Syria unatishia kugubika kila kitu katika mkutano huo.

Waziri mkuu wa Uingereza amesema kabla katika kikao hicho ambacho kilikuwa kinazungumzia zaidi suala la Syria jana Jumatatu kuwa watahakikisha mkutano wa kimataifa wa amani unafanyika baadaye mwaka huu mjini Geneva.

"Kile tunachokihitaji ni kufanikisha mkutano huu wa amani na kipindi cha mpito, ili watu nchini Syria wataweza kuwa na serikali ambayo inawawakilisha , badala ya serikali ambayo inajaribu kuwauwa." Cameron amesema katika mahojiano katika televisheni.

Marekani na Urusi zavutana

Marekani na Urusi zimekuwa zikizitaka serikali za Syria na waasi kufanya mazungumzo ya amani mjini Geneva , lakini juhudi hizo hadi sasa zimegonga ukuta.

Katika mazunguzo yao , rais Obama na Putin wamekuwa wakivutana juu ya vipi wanaweza kumaliza vita nchini Syria.

Wakizungumza baada ya mazungumzo yake na Obama, rais Putin amesema kuwa nchi yake na Marekani zinatofautiana kimawazo kuhusu Syria lakini wanakubaliana kimsingi kuwa umwagikaji wa damu ni lazima ukome na kwamba pande zinazopigana ni lazima zifikishwe katika meza ya majadiliano.

Viongozi hao wote walionekana kuwa katika hali si ya utulivu wakati wakizungumza na waandishi habari baada ya mazungumzo yao ya saa mbili , huku Putin akitazama wakati mwingi sakafuni wakati akizungumza kuhusu Syria na Obama alikuwa nae akimwangalia rais huyo wa Urusi kwa jicho pembe.

Putin amesema nchi yake haivunji sheria za kimataifa kwa kupeleka silaha syria.

"Tunapeleka silaha kwa utawala halali wa Syria na kwa hiyo hatuvunji sheria yoyote ya kimataifa. Tunazitaka pande zote kuheshimu wajibu wao wa kisheria ."

Mgawanyiko kuhusu Syria umetawala hali wakati viongozi wa dunia wakiingia katika mji unaofanyika mkutano huo nchini Ireland ya kaskazini, eneo ambalo hapo kabla lilikumbwa na ghasia kubwa ambalo hivi sasa Uingereza inataka kuonekana kuwa ni mfano wa mafanikio katika kutatua mizozo.

Obama amezungumzia kuhusu urithi wa watu wa Ireland katika dunia kwa kusema.

Obama akihutubia mjini BelfastPicha: Reuters

"Hiki ni kizazi cha kwanza katika nchi hii kurithi mengi kuliko tabia zilizokwisha jikita na mambo ya kufikirika yaliyopita. Kwa maelfu na maelfu mmesaidia kuifanya Marekani ikomae."

Wanaharakati waandamana

Wanaharakati kadha kwa muda walijaribu kukiuka uzio wa chuma uliowekwa wa usalama kuzunguka eneo hilo la mkutano wa G8, lakini waliondoka baada ya polisi kutishia kuwakamata.

Wanaharakati wakiweka mabango yanayosema Tumalize njaaPicha: Reuters

Waandamanaji walikimbia kutoka kile kilichoonekana kuwa ni maandamano ya amani ya wanamazingira wapatao 1,000 pamoja na wanaharakati wa kupigania haki za binadamu katika eneo unakofanyiwa mkutano huo .

Mkutano huo unamalizika hii leo Jumanne.

Mwandishi : Sekione Kitojo / rtre / afpe

Ruka sehemu inayofuata Gundua zaidi
Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW