1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa mawaziri wa NATO mjini Bruxelles

Hamidou, Oumilkher6 Machi 2008

Jumuia ya kujihami ya magharibi yapanga kuzikubalia uanachama nchi zaidi za kambi ya mashariki ya zamani.

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier akizungumza na maripota mjini BruxellesPicha: AP


Mawaziri 26 wa mambo ya nchi za nje wa jumuia ya kujihami ya magharibi NATO wameanza kutathmini mpango mwengine wa kupanuliwa jumuia yao hadi katika nchi ambazo zamani zilikua za kikoministi-kwanza katika eneo la Balkan kuanzia albania,Kroatia na Macedonia na baadae katika jamhuri mbili za zamani za Usovieti-Georgia na Ukraine.


Lakini pekee Kroatia na Albania ndizo zinazoonyesha kua na nafasi nzuri ya kuweza kupasi ipasavyo mtihani na kujumuika haraka na nchi 10 za kambi ya zamani ya mashariki zilizokwishajiunga-kwa awamu mbili na jumuia ya kujihami ya magharibi Nato,Awamu ya kwanza ilikua ya nchi tatu zilizojiunga mwaka 1999 na ya pili zilikua nchi sabaa za kambi ya mashariki ya zamani zilizojiunga na jumuia hiyo ya kujihami ya magharibi katika mwaka 2004.


Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier anasema :


"Ningependelea kuona nchi zote tatu zikikubaliwa uanachama.Kama maridhiano hayatofikiwa kuhusu majina ya nchi zote tatu,basi hakutokua na haja ya kupiga kura kutokana na ule utaratibu wa makubaliano kupitishwa kwa sauti moja."


Maombi ya Macedonia ya kutaka kua mwanachama wa NATO yanakabiliwa na upinzani wa Ugiriki,amekumbusha waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinemeier alipowasili leo asubuhi mjini Bruxelles kushiriki katika kikao cha mawaziri wa mambo ya nchi za nje kuandaa mkutano wa kilele wa NATO utakaofanyika April pili na nne ijayo mjini Bucharest nchini Rumania.


Serikali ya mjini Athens imeshasema itatumia kura yake ya turufu kuzuwia nchi jirani ya Macedonia isikubaliwe uanachama na NATO ikiwa maridhiano hayatafikiwa hadi mkutano wa kilele utakapoitishwa.


Tangu mwaka 1991 Ugiriki imekua ikikorofisha kutambuliwa Macedonia kimataifa kwasababu ya jina.Nchi hiyo inatambuliwa na Umoja wa mataifa mwaka 1993 kwa jina la mpito la "FYROM-au jamhuri ya zamani ya Yugoslavia ya Macedonia.


 Maandamano ya jana usiku yaliyofanywa na wafuasi wa siasa za kizalendo wa Ugiriki kupinga aina yoyote ya ridhaa na nasaha iliyotolewa leo na wawakilishi wa Macedonia mbele ya waandishi habari kushadidia umuhimu wa nchi yao kujiunga na NATO bila ya kulazimika kubadilisha jina,hayatoi ishara njema ya maridhiano kuweza kufikiwa mjini Bruxelles.


Katika eneo la balkan hakuna tatizo isipokua la Ugiriki na Macedonia-amesema waziri wa mambo ya nchi za nje wa Luxembourg Jean Asselborn.


Hata nafasi za Ukraine na Georgia kukubaliwa uanachama si nzuri.Na waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank Walter Steinemeier anasema hafichi wasai wasi wake.


Ukraine na Georgia zilizoan za majadiliano ya kina pamoja na NATO zinapendelea kuingia katika awamu ya pili-nayo ni ile ya mpango wa kimkakati kujiandaa kujiunga na NATO.


Hata hivyo baadhi ya nchi za NATO zinapendelea subira ili kutoikasirisha Urusi.


"Jumuia ya kujihami ya magharibi inadhamini amani,utulivu na wezani sawa.Kupanuliwa ni hatua muhimu lakini wezani sawa nao pia lazma uzingatiwe" amesisitiza waziri wa mambo ya nchi za nje wa Luxembourg Jean Asselborn.



►◄