1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa NAM: Mursi ataka waasi wa Syria waungwe mkono

30 Agosti 2012

Mkutano wa mataifa 120 wanachama wa Jumuiya ya Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (NAM) nchini Iran umetoa fursa ya kukutana kwa mara ya kwanza kwa maraisi wa Misri na Iran kujadiliana mgogoro wa Syria.

Rais wa zamani wa Iran, Ali Akbar Rafsanjani (kushoto), Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon (katikati), na Rais Mohammad Mursi wa Misri wakisikiliza hotuba ya Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatullah Ali Khamenei.
Rais wa zamani wa Iran, Ali Akbar Rafsanjani (kushoto), Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon (katikati), na Rais Mohammad Mursi wa Misri wakisikiliza hotuba ya Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatullah Ali Khamenei.Picha: MEHR

Imebidi Iran, mwenyeji wa mkutano huo, kuonesha kiwango cha juu cha uvumilivu, pale wawili kati ya viongozi muhimu kutoa kauli isizozitegemea kwenye kikao cha ufunguzi wa mkutano huo.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, alitumia hotuba yake kuushambulia vikali msimamo wa Iran kuelekea taifa la Israel na kuiita kuwa haukubaliki.

"Kudai kwamba mwanachama mwengine wa Umoja wa Mataifa, Israel, haina haki ya kuwepo au kuizungumzia kwa maneno ya kibaguzi sio tu kwamba si sahihi, bali pia kunahujumu misingi ambayo sote tumeapa kuilinda." Alisema Ban Ki-moon.

Mara kadhaa, Rais Mahmoud Ahmadinejad wa Iran amekuwa akisema kwamba kile kinachoitwa "mauaji ya maangamizi dhidi ya Mayahudi barani Ulaya" ni hadithi ya kubuni tu, huku pia akiielezea Israel kama "saratani ya ubongo" isiyopastahiki kuwepo.

Mursi ataka waasi Syria waungwe mkono

Kwa upande wake, Rais Mohammed Mursi wa Misri ametumia hotuba yake ya ufunguzi kuunga mkono upinzani nchini Syria, na kuutaka ulimwengu kuwasaidia wale aliowaita "wapiganiaji uhuru na haki dhidi ya utawala wa kikandamizaji" wa Rais Bashar al-Assad.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon mjini Tehran, Iran.Picha: MEHR

"Dola ya watu wa Misri iliyotokana na mapinduzi ya umma ni kigezo kwa Wimbi la Mageuzi ya Arabuni yaliyoanzia Tunisia.... Na sasa mapinduzi yako Syria dhidi ya utawala wa kidhalimu." Alisema Mursi.

Msimamo huu unatafautiana sana na wa Syria na Iran ambao wanawaita waasi nchini Syria kuwa ni "magaidi" wanaotimiza mpango wa Marekani na majirani wa Syria.

Iran ni mshirika mkubwa wa utawala wa Assad, na kauli hii ya Rais Mursi inachukuliwa kama kibao cha uso kwa mwenyeji wake, Rais Ahmadinejad.

Ujumbe wa Syria watoka nje

Ujumbe wa Syria kwenye mkutano huo ulitoka nje kulalamikia kauli hiyo ya Rais Mursi, na baadaye Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria, Walid al-Muallim, aliielezea kauli hiyo kama "inayochochea umwagaji damu na uingiliaji wa mambo ya ndani ya Syria."

Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatullah Ali Khamenei, akifungua mkutano wa kilele wa NAM.Picha: MEHR

Hata hivyo, mkutano huo ulitoa fursa kwa Rais Ahmadinejad kukutana na mgeni wake, Rais Morsi, katika mazungumzo ya faragha.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Hussein Amir Abdullahian, amekiambia kituo cha habari ya al-Alam kwamba viongozi hao wawili walijadiliana mgogoro wa Syria na mahusiano ya nchi zao.

"Walisisitiza haja ya kutatua mgogoro wa Syria kwa diplomasia na kuzuia uingiliaji kati wa mataifa ya nje. Na pia walijadiliana njia za kuimarisha mahusiano kati ya Misri na Iran." Alisema Abdullahian.

Rais Mursi amehudhuria mkutano huo wa mataifa yasiyofungamana na upande wowote, pamoja na mengine, kukabidhi uwenyekiti wa jumuiya hiyo kwa Iran. Uongozi wa jumuiya hiyo huenda kwa mzunguuko na sasa ni zamu ya Iran.

Mwandishi: Mohammed Khelef/AFP/Reuters/DPA
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman