Polisi Ujerumani yahimiza kukomesha kwa vivutio vya uhamiaji
6 Oktoba 2025
Mkuu wa Polisi wa Shirikisho la Ujerumani (Bundespolizei), Dieter Romann, amesema tatizo la uhamiaji usiofuata sheria haliwezi kutatuliwa kwa ukaguzi wa mipaka pekee, bali linahitaji mkakati mpana unaounganisha sera za ulinzi, makazi na urejeshaji wahamiaji.
Akizungumza na gazeti la Welt am Sonntag, Romann alisema: "Tunahitaji mpango wa jumla. Hasa ni lazima kupunguza vichocheo ambavyo nchi yetu inaweka, hadi kiwango cha chini kinachoruhusiwa kikatiba.”
Ameonya kuwa Ujerumani inapaswa kutoa ujumbe wa wazi kuwa haiwezi kupokea watu bila mipaka na kwamba huduma kwa wahamiaji lazima ziambatane na masharti ya wazi.
Kwa kufanya hivyo, alisema, wahamiaji watapoteza motisha ya kujitosa katika safari hatarishi kuingia Ulaya.
Romann aliongeza kuwa bila mkakati wa kisiasa wa pamoja unaounganisha utoaji wa visa, ulinzi wa mipaka, haki za ukaaji, huduma za kijamii, na urejeshaji, tatizo la uhamiaji litaendelea "kwa ukubwa uleule.”
Wito kwa serikali kutekeleza sera kwa uthabiti
Romann alisisitiza kuwa Polisi wa Shirikisho wanaweza kufanya ukaguzi, kuwazuia wasafirishaji haramu na kurudisha wahamiaji, "lakini hawawezi kulitatua tatizo hilo peke yao.”
Alisema hatua madhubuti zinahitajika kutoka kwa wabunge na serikali yenye dhamira ya kweli kutekeleza maamuzi yake.
Akizungumzia suala la urejeshaji wahamiaji (Abschiebungen), Romann alifichua kuwa mwaka uliopita majimbo ya Ujerumani yaliwasilisha maombi ya kurejesha takriban watu 53,800 kwa Polisi ya Shirikisho.
Hata hivyo, kati ya idadi hiyo, zaidi ya maombi 33,600 yaliahirishwa kabla wahusika hawajafikishwa kwa maafisa wa uhamiaji.
Kati ya sababu kuu za kuchelewesha mchakato huo ni wahamiaji kutoweka siku ya safari au kuwasilisha vyeti vya ugonjwa ghafla.
Kwa sasa, alisema, Ujerumani ina zaidi ya watu 226,000 wanaotakiwa kurejea makwao, lakini kuna nafasi chini ya 800 pekee katika vituo vya mahabusu ya urejeshaji.
Vizuizi vya kisheria vya vituo vya urejeshaji
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Shirikisho, Alexander Dobrindt (CSU), amekiri kuwepo kwa changamoto za kisheria katika kuanzisha vituo vya urejeshaji (Rückführungszentren) kwa waombaji wa hifadhi waliokataliwa katika nchi za tatu.
Baada ya mkutano wa kilele wa uhamiaji uliofanyika mjini Munich, Dobrindt alisema: "Tupo mwanzoni mwa mchakato huu. Tayari kumekuwa na majaribio kadhaa na tumekutana na vikwazo vya kisheria.”
Amebainisha kuwa bado kuna tofauti za maoni miongoni mwa mataifa ya Ulaya kuhusu utekelezaji wa mpango huo, lakini mazungumzo yanaendelea ili kupata suluhisho la pamoja.
Kwa upande wake, Kamishna wa Uhamiaji wa Umoja wa Ulaya, Magnus Brunner, amesema ni muhimu Ujerumani iendelee kushinikiza hatua thabiti, akiongeza kuwa: "Ni hali isiyokubalika kwamba sasa ni mtu mmoja pekee kati ya watano wanaotakiwa kuondoka Ulaya ndiye anayefanya hivyo kweli.”
Chanzo: wa/pgr (kna, afp, dpa, rtr)