1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiAfrika Kusini

Moto mkubwa mjini Johannesburg waibua mjadala Afrika Kusini

Sylvia Mwehozi
1 Septemba 2023

Vikosi vya uokozi nchini Afrika Kusini vikisaidiwa na mbwa wa kunusa vimeendelea kuwatafuta wahanga wa ajali ya moto uliotetekeza jengo moja la ghorofa mjini Johannesburg, na kusababisha vifo vya watu 74.

Südafrika | Gebäudebrand in Johannesburg
Picha: Themba Hadebe/AP Photo/picture alliance

 Ajali hiyo imeisukuma serikali ya Afrika Kusini kuanza kushughulikia tatizo la makazi haramu. Mamlaka iliwaomba jamaa wa wahanga hao kwenda katika chumba cha kuhifadhia maiti katika kitongoji cha Soweto ili kutambua miili ya ndugu zao huku msako ukiendelea katika eneo hilo.

Soma pia: Waliokufa kwenye mkasa wa moto Afrika kusini waongezeka

Moto huo uliounguza jengo la ghorofa tano umeibua kwa mara nyingine mjadala kuhusiana na majengo yaliyovamiwa, katika maeneo yaliyotelekezwa ambayo yanakaliwa na makundi ya wahalifu ambao huchukua kodi kutoka kwa wakaazi wenye vipato duni.

Rais Cyril Ramaphosa amesema wakati alipozuru eneo la ajali jana jioni kwamba, moto huo ni kama indhari kwa serikali kuanza kushughulikia hali ya makazi katikati ya majiji.