1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Cherif Chekatt ni mhalifu aliyeshitakiwa mara kadhaa

14 Desemba 2018

Mshukiwa anaeaminika kushambulia soko la krismasi mjini Strasbourg, Ufaransa na kuwaua watu watatu kabla kuuuwawa na polisi baada ya kusakwa kwa siku tatu, ni mhalifu aliyeshitakiwa mara kadhaa nchini Ufaransa

Frankreich Straßburg Attentat
Picha: picture-alliance/dpa/J.-M. Loos

Cherif Chekatt aliye ana miaka 29 amewahi kushitakiwa kwa makosa kadhaa ya uhalifu ambayo ni pamoja na vurugu na wizi, na aliwekwa pia katika orodha ya watu walio na misimamo mikali alipokuwa jela nchini Ufaransa, mwaka 2015 ambapo wakati huo alielezwa na serikali ya nchi hiyo kwamba alikuwa miongoni mwa watu walio na itikadi kali.

Cherif Chekatt anaeaminika kushambulia soko la Krismasi la Strasbourg Picha: picture alliance/dpa

Kuanzia wakati huo amekuwa akifuatiliwa na idara ya ujasusi ya Ufaransa inayowafuatilia pia maelfu ya washukiwa hao nchini humo.

Ashahukumiwa mara 27  Ufaransa na hata nchini Ujerumani, Switzerland na Luxembourg, maeneo yanayofikiwa kwa urahisi kutoka Strasbourg.

Aidha mkanda wa video uliotolewa, unaonesha namna tukio la kuuwawa kwa Cherif Chekatt lilivyotokea, na kuwaonesha pia maafisa wa polisi wakiwa katika eneo la tukio huku mwili wa Chekat ukiwa umelala kando ya mlango.

Maafisa wengine zaidi wanaonekana wakifika mahala hapo huku wachunguzi wa masuala ya uahalifu wakichukua picha zaidi za mwili wa Chekatt.

Soko la Krismasi lafunguliwa tena baada ya shambulio

Huku hayo yakiarifiwa, soko hilo la Krismasi mjini Strasbourg limefunguliwa tena hii leo siku kadhaa baada ya shambulizi kutokea siku ya Jumanne wiki hii. Hapo jana Waziri wa mambo ya ndani wa Ufaransa Christophe Castaner alisema soko hilo litafunguliwa muda mfupi baada ya saa tano mchana hii leo.

Siku ya Jumanne jioni Cherif Chekatt aliwamiminia risasi watu waliokuwa katika soko hilo na kuwauwa watu watatu huku wengine 13 wakijeruhima. Waendesha mashtaka wa Ufaransa wanalichukulia shambulizi hilo kama shambulizi la kigaidi. Kundi la wanamgambo wa dola la kiislamu wamekiri kuhusika na shambulizi hilo.

Soko la Krismasi la StrasbourgPicha: Reuters/V. Kessler

Duru za kuaminika zinasema kuwa wakati alipokuwa kizuizini mwaka 2008 picha ya kiongozi wa kundi la kigaidi Osama bin Laden ilikutwa chumbani mwake.

Lakini jirani zake Chekatt wamemuelezea kama mtu pole ambaye hakuwa sana katika masuala ya kidini na hawamuoni kama mhalifu  aliishi katika chumba kimoja kidogo karibu na familia yake.

Mwandishi: Amina Abubakar/AFP/AP/dpa

Mhariri: Mohammed Khelef