1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUganda

Museveni na Wine walaumiana kwa kupanga njama za ghasia

2 Januari 2026

Wagombea wawili wakuu wa kinyang’anyiro cha urais wa Uganda wamejibizana kuhusu suala la ghasia za uchaguzi. Rais Museveni anawania kubakia madarakani na anakabiliwa na mpinzani wake mkuu Robert Kyagulanyi.

Uganda | Rais Yoweri Museveni | kampeni ya uchaguzi nchini Uganda 2026
Picha ikimuonyesha Rais wa Uganda Yoweti Museveni akiwa kwenye kampeni ya uchaguzi wa 2026Picha: Uganda PPU

Rais Yoweri Museveni anayewania kubakia madarakani na mpinzani wake mkuu Robert Kyagulanyi, kila mmoja amemkosoa mwenzake kwa kupanga njama za kusabisha vurugu katika uchaguzi utakaofanyika tarehe 15 Januari.

Zikiwa zimesalia siku 13 uchaguzi ufanyike Uganda, Rais Yoweri Museveni amedai kuwa mpinzani wake mkuu Robert Kyagulanyi maarufu kama Bobi Wine amepanga ghasia akisaidiwa na wafadhili wake wa kigeni wasioitakia Uganda mema.

Museveni, Kyagulanyi watupiana lawama

Katika hotuba yake ya mwaka mpya kwa taifa, rais Museveni amemtaja mpinzani wake mkuu Robert Kyagulanyi kama mtu ambaye hajakomaa kisiasa na ndiyo maana hazingatii matokeo ya matamshi yake. Kiongozi huyo ambaye ametawala Uganda kwa miaka 40 sasa anakosoa mataifa ya kigeni ambayo yanafadhili kampeni za Bobi Wine akielezea kuwa hayana nia njema kwa Uganda.

Mgombea wa upinzani nchini Uganda na mgombea wa urais Robert Ssentamu Kyagulanyi "Bobi Wine"Picha: Lukeman Kampala

Kwa upande wake Bobi Wine amemjibu Museveni akisema kuwa ni wazi kwamba utawala wa Museveni ndiyo umejiandaa kuvuruga uchaguzi kutokana na kanuni ambazo zinazidi kutolewa kama vile kuwakataza watu kubaki kwenye vituo vya kupigia kura kufuatilia zoezi hilo kwa karibu. Msimamo huo wa utawala anaulezea kuwa hila ya kuweza kughushi matokeo na hii inawatishia  wapigaji kuhusiana na kushiriki katika uchaguzi.

Katika kipindi cha kampeni, majeshi na polisi wameshuhudiwa wakiwacharaza wafuasi wa upinzani hasa wa chama kikuu cha upinzani cha NUP wakiwa kwenye misafara na mikutano ya kampeni. Museveni amewahimiza kutotumia mbinu hiyo akiwashauri kutumia mabomu ya kutoa machozi lakini pia kwa tahadhari.

Kampeni za urais Uganda zavutia umati mkubwa wa watu

02:33

This browser does not support the video element.

Kamatakamata ya wanaharakati yahofiwa kuanza

Kwingineko kamatakamata ya wanaharakati wa haki za binadamu hasa viongozi wa asasi za kiraia inahofiwa kuwa imeanza kutekelezwa.

Kwenye uchaguzi uliopita wanaharakati kadhaa walikamatwa na kuzuiliwa katika kipindi cha uchaguzi. Kukamatwa kwa mwanaharakati maarufu wa masuala ya utawala na demokrasia Sarah Birete siku mbili zilizopita kumetajwa na wenzake kuwa mojawapo na njia za kutaka kuwatishia wasiendelee na shughuli zao za kufuatilia mchakato wa uchaguzi.

Mwito wa wapiga kura kubaki kwenye vituo vya uchaguzi umeungwa mkono pia na viongozi mbalimbali wakiwepo wa kidini. Ikumbukwe kuwa rais Museveni alitoa angalizo kuwa kila mwanajeshi na polisi atakuwa na risasi 120 kwa hiyo watu wasidhani kwamba watawazidi nguvu ikiwa watang'ang'ania kubaki kwenye vituo vya kupigia kura badala ya kurudi nyumbani baada ya kupiga kura.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW