1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mvutano wa kibiashara watarajiwa kutawala mkutano wa G20

Mohammed Abdulrahman
29 Novemba 2018

Suala la mvutano wa kibiashara kutokana na msimamo wa Marekani kujilinda kibiashara linatarajiwa kutawala zaidi katika mkutano wa G20 unaotarajiwa kuanza Ijumaa mjini Buenos Aires Argentina.

Peking Donald Trump Xi Jinping
Picha: Getty Images/AFP/J. Watson

Mkutano wa kilele wa  nchi 20 zinazostawi kiuchumi, kundi linalojulikana kama G20, utafunguliwa kesho mjini Buenos Aires Argentina.  Suala la mvutano wa kibiashara kutokana na msimamo wa Marekani kujilinda kibiashara linatarajiwa kutawala zaidi katika mkutano huo.

Kutokana na  sera yake ya "Marekani kwanza," katika suala la biashara  rais Donald Trump hakuvutana  tu na Umoja wa Ulaya na Canada , bali pia na  China. Mvutano kuhusu biashara unasababisha biashara ya dunia kuwa katika hali ya msukosuko huku mkuu wa  Shirika la fedha la Kimataifa IMF Christine Lagarde ambaye  atashiriki katika mkutano huo, akionya kwamba  mgogoro wa  kibiashara una athari kubwa kwa uchumi wa dunia, ambapo ukuaji wa  uchumi wa dunia umeporomoka kwa 0.5 asilimia.
 

Kansela Angela Merkel wa Ujerumani pamoja na viongozi wengine katika kundi hilo la G20 ukimuweka kando Trump,  wanatarajiwa kupigia upatu  biashara huru. Kwa wakati huu kutokana  na hali ilivyo, mtu anaweza kusema ingawa sio rasmi kwamba  kauli mbiu ya mkutano huo  wa kilele  ni " sote dhini ya mmoja , sote dhidi ya Trump."

Rais Trump na Xi Jinping watarajiwa kukutana kuondoa tofauti zao

Mrithi wa ufalme wa Saudi Arabia Mohamed bin Salman akiwasili Argentina kuhudhuria mkutano wa G20Picha: Reuters/Argentine G20

Wakati wa mkusanyiko huo wa Buenos Aires, Trump anatarajia kukutana na Rais wa China Xi jinping kujaribu kufikia makubaliano ya kuondoa tafauti zao. Lakini tayari alikwisha onya kwamba pindi itashindikana  basi China iwe tayari kwa vikwazo vya Marekani, akioonya ana mpango  wa kuitoza  China  ushuru wa jumla wa dola 250 bilioni  kwa biadhaa zake zinazoingia Marekani pindi hapatokuweko  makubaliano yoyote ..
 

Iwapo rais wa Halmashauri kuu ya Umoja wa Ulaya Jean-Claude Juncker atakutana kwa mazungumzo na Trump kandoni mwa mkutano huo wa kilele wa G20 bado haijafahamika wazi. mabishano na Umoja wa Ulaya ni kuhusu ushuru katika biashara ya magari kutoka nchi wanachama wa Umoja huo.

Rais Trump atarajiwa kukutana na Rais Putin

Rais Trump na Putin pia wanatarajiwa kukutana kujaribu kufikia maelewano. Picha: Getty Images/B. Smialowski

Kwa upande mwengine yamepangwa mazungumzo kati ya Trump na Rais wa Urusi Vladimir Putin, lakini haiko wazi ikiwa watafikia maelewano au la Akiulizwa  kama  mazungumzo yatavunjwa kutokana na mgogoro mpya  kati ya Urusi na Ukraine, Trump aliliambia gazeti la Washington Post kwa mkato tu." Sipendi tabia ya uchokozi dhidi ya wengine."

Kandoni mwa sarakasi yote hiyo  kumhusu Trump, Duru za kibalozi za Umoja wa Ulaya zinasema suala jengine litakalopewa kipa umbele katika mkutano wa Buenos Aires ni  kuwashajiisha waajiri kuwa  na mpango bora wa mafunzo  kwa vijana utakaofungua nafasi za ajira. Hiyo ni mada muhimu kwa Afrika na suala linalopigiwa upatu na  Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini, ambaye  anasema,  upande huo Ujerumani ina mchango mkubwa wa kutoa kupitia  kile kinachoitwa, "Mpango kwa ajili ya Afrika,  uliobuniwa  wakati wa mkutano uliopita wa G20  katika jiji la kaskazini mwa Ujerumani la Hamburg, ambao Ramaphosa alishiriki.

Mwandishi: Mohammed Abdul-Rahman/Bernd Riegert (DW)

Mhariri: Mohammed Khelef

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW