1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUlaya

Nchi za Magharibi kutumia mali za Urusi kuifadhili Ukraine

14 Juni 2024

Viongozi wa G7 wanapanga kutumia riba kutoka mali za Urusi zilizozuwiliwa za dola bilioni 300 kusaidia Ukraine. Fedha hizo zitatumika kama dhamana ya mkopo mkubwa kwa Kyiv, kuimarisha ulinzi wake dhidi ya Urusi.

Sarafu ya Urusi ya Rouble
Mataifa ya Magharibi yamekamata karibu dola bilioni 300 katika mali za benki kuu ya Urusi muda mfupi baada ya uvamizi wa Ukraine.Picha: MOSCOW NEWS AGENCY/REUTERS

Ufadhili wa mapambano ya Ukraine dhidi ya uvamizi wa Urusi umetoka kuwa hali ya lazima hadi kuwa suala zito la kisiasa katika takriban miaka miwili na nusu. Ulimwengu tayari umetoa Euro bilioni 297 ( katika msaada kwa Ukraine. Lakini nchi hiyo inahitaji zaidi.

Marekani na Umoja wa Ulaya pia zimepambana kuafikiana kuhusu nini cha kufanya na baadhi ya mali za benki kuu ya Urusi zenye thamani ya dola bilioni 300 ambazo zilizuiliwa kama sehemu ya vikwazo vya Magharibi muda mfupi baada ya vifaru vya Urusi kuingia Ukraine.

Washington ilitaka kutumia pesa zilizokamatwa kufadhili juhudi za vita vya Ukraine. Kwa kuwa fedha nyingi zilizokamatwa zilikuwa Ulaya, Brussels ilisema hapana, kutokana na mashaka ya kisheria yanayotokana na kuzuwiliwa kwa mali hizo wakati nchi za Magharibi hazishiriki moja kwa moja vita na Urusi.

Soma pia: Viongozi wa nchi za G7 wakubaliana kuipa msaada zaidi Ukraine

Baada ya miaka miwili ya kuzozana, muafaka umepatikana na viongozi wa G7 wameeleza jinsi watakavyotumia fedha hizo. Badala ya kutumia kiasi kikuu cha dola bilioni 300, mpango huo mpya utatumia riba itokanayo na mali hizo - inayokadiriwa kuwa bilioni chache kwa mwaka - kama dhamana ya mkopo wa mara moja wa hadi dola bilioni 50 kwa Ukraine.

Wanajeshi wa Ukraine wanapambana na uvamizi wa Urusi mashariki na Kusini mwa nchi hiyo.Picha: Ozge Elif Kizil/Anadolu/picture alliance

Wakati dola hizi bilioni 50 zitakaribishwa zaidi huko Kyiv, hata suluhisho hilo la muafaka limeleta changamoto kwa watunga sera, kwani itahitaji miaka kadhaa ya malipo ya riba kwa mali zilizozuwiliwa ili kulipa mkopo huo.

Jacob Kirkegaard, afisa mwandamizi katika ofisi ya Brussels ya Shirika la Kijerumani la Marshall Fund, aliiambia DW kuwa kulipia mkopo huo, inahitajika mali zilizozuwiliwa zisirejeshwe kwa Urusi kwa angalau kipindi cha miaka 10 hadi 20.

Kirkegaard aliongeza kuwa inaweza kuwa vigumu kuachilia kiasi kikuu baada ya vita kusaidia kufadhili ujenzi mpya wa Ukraine kwa sababu fedha hizo zitatumika kwa zaidi ya muongo mmoja ili kudhamini mkopo huu mpya.

Soma pia:Mkutano wa kujadili amani Ukraine huko Uswisi utafanikiwa? 

"Ikiwa unaamini kwamba Ukraine itashinda na itahitaji kujengwa upya wakati fulani, basi mali hizi, ikiwa zitaendelea kufungwa au kuzuwiliwa kwa miaka 10, zinaweza zisipatikane wakati ujenzi mpya unaanza, tuseme, miaka mitatu hadi mitano," alisema Kirkegaard.

Ulinzi dhidi ya turufu ya Trump

Mkopo huo wa mara moja, hata hivyo, unazisaidia nchi za Magharibi kutokana na upungufu mkubwa wa ufadhili. Umoja wa Ulaya umepambana kuziba pengo la ufadhili wa Marekani uliochelewa katika miezi michache iliyopita.

Kwa muda mfupi, muafaka huu utasaidi kuzuwia turufu ya Trump. Rais huyo wa zamani wa Marekani hapo awali aliapa kupunguza msaada kwa Kyiv iwapo atachaguliwa tena mwezi Novemba lakini hivi karibuni amepunguza makali ya matamshi yake kuhusu suala la ufadhili.

Baadhi ya Waukraine waamua kutoroka kuliko kupigana na Urusi

04:33

This browser does not support the video element.

Yuriy Gorodnichenko, profesa wa uchumi wa Kiukreni katika Chuo Kikuu cha California, Berkeley, aliiambia DW, kuwa matokeo ya uchaguzi wa Marekani yanaweza yasiwe mazuri kwa Ukraine, kwa hivyo viongozi wa G7 wanataka kupata ufadhili kwa angalau mwaka mmoja zaidi.

Hatimaye, hata hivyo,washirika wa Ulaya wanahitaji kufanya uamuzi wa kisiasa kuhusu kama wanataka kugusa mali kuu za Urusi au la.

Mahitaji ya msaada ya Ukraine yanaweza kudumu kwa miaka mingi zaidi, ikiwemo  mabilioni ya jenzi mpya wa miundombinu ya umeme iliyoharibika wakati wa mzozo, na ujenzi wa miji mara tu vita vitakapomalizika.

Soma pia: Scholz: Hakuna hatari Ukraine kushambulia ndani ya Urusi kwa silaha za Ujerumani

Wakati huo huo, serikali ya Ukraine inaishiwa na njia za ufadhili. Baada ya kusitasita kuongeza kodi katikati mwa mzozo, jambo linaloweza kudidimiza uchumi ambao tayari ni dhaifu, Kyiv sasa inaandaa kupandisha kodi ya mapato, ushuru wa bidhaa, kodi ya mauzo na ushuru mwingine usio wa moja kwa moja.

Urusi pia imekuwa ikiongeza kodi ili kuendelea kufadhili vita vyake. Lakini wachambuzi wanaamini kuwa Kremlin itakabiliwa na vikwazo vikubwa vya bajeti ndani ya miaka miwili ijayo, na hivyo kuamsha tena miito kwa Washington na Brussels kuipa Ukraine faida kwa kutumia dola bilioni 300 zote ambazo zilizuiliwa mwaka 2022.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW