1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Sheria na HakiAmerika ya Kaskazini

Nani alimuua Tupac Shakur?

19 Agosti 2026

Kwa karibu miaka 30, swali la nani aliyemuua Tupac Shakur halijapata jibu la kisheria. Kesi ya Duane Davis sasa inachunguza madai ya kisasi, magenge na simulizi za mtu anayekanusha kupanga mauaji hayo.

Marekani Tupac Shakur 1994
Miaka 30 tangu kuuawa, je, haki itapatikana kwa Tupac Shakur?Picha: Globe Photos/ZUMAPRESS/picture alliance

Kwa karibu miaka 30, swali la nani aliyemuua Tupac Shakur limeendelea kuwatesa wanafamilia, mashabiki na wachunguzi wa historia ya muziki wa hip-hop. Majina mengi yametajwa, nadharia nyingi zimeenea, lakini hakuna mtu aliyewahi kutiwa hatiani kwa mauaji hayo.

Jibu fupi ni kwamba mpaka sasa haijathibitishwa mahakamani nani aliyefyatua risasi zilizomuua Tupac. Hata hivyo, waendesha mashtaka wanaamini wamebaini jinsi mauaji hayo yalivyopangwa na nani aliyeratibu shambulizi.

Duane "Keffe D” Davis, aliyekuwa kiongozi wa genge la South Side Compton Crips, ndiye mtu pekee aliyeshtakiwa. Hatuhumiwi kuwa ndiye aliyefyatua risasi, bali kupanga na kuwezesha shambulizi la kulipiza kisasi lililotokea Las Vegas mwaka 1996.

Kesi yake imeanza wakati mashahidi wengi muhimu wakiwa wamefariki, kumbukumbu zikiwa zimefifia na simulizi mbalimbali kuhusu kilichotokea zikiwa zimechanganyika na utamaduni wa kutowasaliti wanachama wa magenge.

Duane Davis ndiye mtu pekee aliesalia katika kundi la watu waliokuwa ndani ya gari ambako risasi zilizomuua Tupac zilifyatulia, na anashtakiwa kwa kupanga mauaji hayoPicha: Steve Marcus/REUTERS

Usiku wa mwisho wa Tupac

Mnamo Septemba 7, 1996, Tupac, aliyekuwa na umri wa miaka 25, alihudhuria pambano la ndondi kati ya Mike Tyson na Bruce Seldon katika hoteli ya MGM Grand mjini Las Vegas. Alikuwa pamoja na Marion "Suge” Knight, mkuu wa kampuni ya muziki ya Death Row Records.

Baada ya pambano, Tupac na baadhi ya watu waliokuwa pamoja naye walionekana katika kamera za usalama wakimshambulia Orlando "Baby Lane” Anderson katika eneo la hoteli hiyo. Anderson alikuwa mpwa wa Davis na mwanachama wa genge hasimu la South Side Compton Crips.

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka, ugomvi huo haukuwa tukio la bahati mbaya. Anderson alidaiwa kuhusishwa na jaribio la awali la kupora mkufu wenye nembo ya Death Row kutoka kwa mtu aliyekuwa karibu na Suge Knight. Kipigo cha MGM Grand kikawa sababu ya kulipiza kisasi.

Saa chache baadaye, Tupac na Knight waliondoka kuelekea Club 662, ambako Tupac alitarajiwa kutumbuiza katika hafla ya hisani. Wakiwa wamesimama kwenye taa za barabarani ndani ya gari jeusi aina ya BMW, gari jeupe aina ya Cadillac lilifika upande wao.

Mtu aliyekuwa ndani ya Cadillac alifyatua risasi kadhaa. Tupac alipigwa kifuani na katika sehemu nyingine za mwili, huku Knight akijeruhiwa kidogo. Tupac alikimbizwa hospitalini, lakini akafariki siku sita baadaye, Septemba 13, 1996.

Nani alikuwa ndani ya Cadillac?

Waendesha mashtaka wanasema watu wanne walikuwa ndani ya Cadillac: Duane Davis, mpwa wake Orlando Anderson, Terrence "T-Brown” Brown na DeAndre "Dre” Smith. Wote isipokuwa Davis wamefariki.

Kwa miaka mingi, Anderson alitajwa kuwa mshukiwa mkuu na baadhi ya wachunguzi waliamini ndiye aliyefyatua risasi. Alikana kuhusika na hakuwahi kushtakiwa. Aliuawa katika shambulizi jingine la magenge mwaka 1998.

Hata hivyo, utambulisho wa mtu aliyekuwa na bunduki bado haujaamuliwa na mahakama. Baadhi ya simulizi zimemtaja Anderson, huku ushahidi mwingine uliowasilishwa mbele ya jopo la awali la mahakama ukimtaja DeAndre Smith. Kwa hiyo, madai kuhusu aliyefyatua risasi yanapaswa kutenganishwa na shtaka linalomkabili Davis la kupanga shambulizi.

Sheria ya Nevada inaweza kumruhusu mtu kushtakiwa kwa mauaji hata kama hakufyatua risasi, iwapo alisaidia kupanga, kutoa silaha au kuwezesha uhalifu. Hicho ndicho kiini cha kesi dhidi ya Davis.

Naibu Mwendesha Mashtaka Mkuu Binu Palal akitoa hoja za ufunguzi katika kesi ya Duane Davis inayohusu mauaji ya rapa Tupac Shakur mwaka 1996, katika Mahakama ya Wilaya ya Clark mjini Las Vegas, Nevada, Marekani, Agosti 17, 2026.Picha: Steve Marcus/REUTERS

Simulizi za Davis zageuka ushahidi

Kwa mujibu wa waendesha mashtaka, Davis alizungumza na wachunguzi mara kadhaa kuhusu mauaji hayo. Katika mahojiano ya mwaka 2008 na kikosi cha pamoja cha serikali kilichokuwa kikichunguza mauaji ya Notorious B.I.G., alidai kuwa alikuwamo ndani ya Cadillac na kwamba aliwapa bunduki wanaume waliokuwa nyuma.

Davis pia alizungumza kuhusu shambulizi hilo katika mahojiano ya hadhara na kitabu chake cha mwaka 2019, Compton Street Legend. Maelezo hayo yaliisaidia polisi kufufua uchunguzi uliokuwa umekwama kwa miaka mingi.

Polisi walipekua nyumba inayohusishwa na Davis mjini Henderson, Nevada, Julai 2023. Jopo kuu la mahakama baadaye lilimfungulia shtaka la mauaji na Davis akakamatwa Septemba mwaka huo.

Upande wa mashtaka unasema Davis aliratibu shambulizi, akatoa bunduki na kusaidia kundi hilo kumsaka Tupac baada ya kipigo cha Anderson. Mwendesha mashtaka Binu Palal amewaambia majaji kwamba Davis hakufyatua risasi, lakini alipanga mauaji hayo kama kisasi.

Mahakamani, upande wa mashtaka unadai Davis alipanga mauaji ya Tupac, huku utetezi ukisema kesi hiyo imejengwa juu ya simulizi za kubuni na ushahidi usioaminika.Picha: Steve Marcus/REUTERS

Utetezi: Simulizi hizo ni za kubuni

Davis amekana shtaka. Wakili wake Michael Sanft anasema upande wa mashtaka umejenga kesi juu ya simulizi zisizoaminika, mahojiano ya zamani na kitabu kilicholenga kumletea Davis umaarufu na fedha.

Utetezi unasema kama polisi waliamini maelezo ya Davis, wangemshtaki miaka mingi iliyopita. Sanft amedai uchunguzi wa awali ulikuwa na mapungufu, nyaraka muhimu zimepotea na muda mrefu uliopita umeathiri uwezo wa mashahidi kukumbuka matukio kwa usahihi.

Davis pia amedai kwamba baadhi ya kauli alizotoa kwa wachunguzi zililindwa na makubaliano yaliyomruhusu kuzungumza bila maelezo yake kutumiwa dhidi yake. Mahakama ya Juu ya Nevada ilikataa kusitisha kesi kwa msingi huo, lakini haikutoa uamuzi wa mwisho kuhusu hatia yake.

Changamoto nyingine ni ukosefu wa mashahidi walio tayari kuzungumza. Mmoja wao, James McDonald, alionyesha wazi mahakamani kuwa hataki kufufua yaliyopita au kusaidia kumpeleka mtu mwingine mweusi gerezani. Polisi wa zamani pia wameeleza kuwa mashahidi wengi walinyamaza kwa hofu ya kulipiziwa kisasi.

Nadharia za magenge na ushindani wa hip-hop

Kwa miaka mingi, mauaji ya Tupac yamehusishwa pia na ushindani kati ya wasanii na kampuni za muziki za Pwani ya Mashariki na Pwani ya Magharibi ya Marekani. Tupac na Death Row Records walikuwa katika mgogoro mkali na Notorious B.I.G. pamoja na Bad Boy Records.

Mauaji ya Notorious B.I.G. huko Los Angeles miezi sita baada ya kifo cha Tupac yaliongeza dhana kwamba matukio hayo yalikuwa sehemu ya vita vya hip-hop. Hata hivyo, mauaji ya Biggie bado hayajatatuliwa, na madai mengi yanayounganisha watu mashuhuri wa muziki na kifo cha Tupac hayajathibitishwa mahakamani.

Ushahidi unaotolewa sasa unalenga zaidi mgogoro wa magenge na tukio la MGM Grand kuliko nadharia pana ya njama katika tasnia ya muziki. Waendesha mashtaka wanadai kipigo cha Anderson kilisababisha mpango wa haraka wa kulipiza kisasi katika muda wa saa chache.

Tupac Shakur na Notorious B.I.G. walikuwa vinara wa pande hasimu katika muziki wa hip-hop, na wote waliuawa kwa kupigwa risasi katika kipindi cha miezi sita.Picha: picture-alliance / Mary Evans Picture Library

Familia yasubiri kufungwa kwa ukurasa

Katika siku ya pili ya kesi, baadhi ya wanafamilia wa Tupac waliondoka mahakamani kabla ya picha za uchunguzi wa mwili wake kuonyeshwa. Wengine walibaki, ingawa baadhi yao waligeuza nyuso zao walipoona majeraha yake.

Binamu yake, Zayd Akinyela, alisema familia imesubiri karibu miaka 30 ili kuweza kuomboleza ipasavyo. Kwa maoni yake, kujua kilichotokea, namna kilivyotokea na nani aliyehusika ni sehemu ya kupata utulivu wa moyo.

Mtaalamu wa uchunguzi wa vifo Lisa Gavin ameeleza kuwa moja ya risasi ilisababisha pafu la Tupac kuporomoka na kuvuja damu. Madaktari waliliondoa wakijaribu kuokoa maisha yake, lakini risasi nyingine ziliharibu utumbo na sehemu nyingine za mwili.

Sasa jukumu la majaji si kutatua kila nadharia iliyozunguka mauaji hayo kwa miongo mitatu. Wanapaswa kuamua kama upande wa mashtaka umethibitisha bila shaka ya msingi kwamba Davis alipanga na kuwezesha shambulizi lililomuua Tupac.

P. Diddy alikuwa mkuu wa Bad Boy Records, iliyokuwa katika ushindani mkali na Death Row Records ya Tupac, lakini hajawahi kuthibitishwa mahakamani kuhusika na mauaji hayo.Picha: Kathy Willens/AP/picture alliance

Hukumu dhidi ya Davis haitathibitisha moja kwa moja nani aliyefyatua risasi ikiwa mahakama haitalazimika kuamua suala hilo. Lakini inaweza kuwa uamuzi wa kwanza wa kisheria kuwajibisha mtu kwa mauaji yaliyobadili historia ya hip-hop.

Kwa familia ya Tupac, kesi hiyo ni nafasi ya kupata majibu yaliyochelewa kwa karibu kizazi kizima. Kwa upande wa utetezi, kuchelewa huko ndiko kunakofanya ushahidi kuwa dhaifu na usioaminika. Hivyo, swali kuu sasa si tu nani alimuua Tupac Shakur, bali pia: Je, haki itapatikana baada ya miaka 30?

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW