1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nchi za magharibi zakosoa hukumu ya Tikhanovsky

15 Desemba 2021

Mataifa ya Magharibi yamelaani vikali hukumu iliyotolewa kwa kiongozi wa upinzani wa Belarus, Srgei Tikhanovsky kwa kosa la kuchochea machafuko pamoja na vitendo vya uchochezi wa chuki nchini humo.

Belarus-politics-CZECH-BELARUS-POLITICS-DIPLOMACY
Picha: Roman Vondrous/POOL/AFP via Getty Images

Tikhanovsky, mwenye umri wa miaka 43 amehukumiwa kifungo cha miaka 18 gerezani. soma Belarus yamfunga jela Tsikhanouski, mpinzani wa Lukashenko

Msemaji wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya Peter Stano, ameitaja hukumu hiyo kama sehemu ya ukandamizaji wa kikatili na wa kimfumo kubinya uhuru wa kujieleza unaoendelea nchini Belarus.

Stano ameongeza kuwa Umoja wa Ulayaunalaani vikali ukiukaji huo wa wazi wa haki za binaadamu unaofanywa na serikali ya Belarus.

Wakati huo huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Annalena Baerbock ameitaja hukumu hiyo kuwa ni kashfa na kwamba wanadhalilisha utawala wa sheria na majukumu yake ya kimataifa.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Antony Blinken amesema wananchi wa Belarus hawastahili ukandamizaji mkubwa kama huo.

soma Umoja wa Ulaya yaiwekea vikwazo vya kiuchumi Belarus

Upinzani wanyamazishwa

Rais Alexander LukaschenkoPicha: Sergei Sheleg/BelTA/Handout via REUTERS

Licha ya maandamano ya kimataifa, watu kadhaa mashuhuri wa upinzani tayari wamehukumiwa nchini Belarus katika miezi ya hivi karibuni. Kwa mfano, Maria Kolesnikova alihukumiwa kifungo cha miaka 11 gerezani. Mwanasiasa wa upinzani Viktor Babariko alihukumiwa kifungo cha miaka 14 jela. Soma Mwanaharakati wa Belarus apatikana amekufa Ukraine

Mke wa Tsikhanouski Sviatlana Tsikhanouskaya ambaye alikuwa mchanga kisiasa wakati wa kukamatwa kwa mumewe, alichukua nafasi yake kama mgombea wa urais lakini alishindwa na Lukashenko katika uchaguzi huo. 

Tsikhanouskaya amepinga uamuzi wa mahakama na kupitia ukurasa wake katika mtandao wa twitter aliandika "Dikteta hulipiza kisasi hadharani dhidi ya wapinzani wake wakuu," .

Tsikhanouski alikamatwa mwaka uliopita baada ya kuongoza vuguvugu la maandamano kupinga utawala wa rais wa Belarus Alexander Lukashenko, na alipanga kuwania urais dhidi ya Lukashenko Agosti mwaka 2020 nchini Belarus.

Wakati wa kampeni zake, Tsikhanouski alibuni tusi dhidi ya Lukashenko kwa kumuita ‘kombamwiko'. Kauli mbiu ya kampeni yake ikawa ni mkomeshe kombamwiko, huku wafuasi wake wakijibu kwa kubeba ndara kuashiria wanamuua mdudu. soma Upinzani waitisha mgomo wa taifa nchini Belarus

Punde tu alipotangaza kuwa atawania urais, mwanaharakati huyo aliwekwa kizuizini na kushtakiwa kwa makosa ya kuvuruga utulivu wa umma.

 

Vyanzo/AFP, Reuters,

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW