Netanyahu aishutumu jamii ya Kimataifa
3 Septemba 2012Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, alisema wakati wa kuanza kikao chake cha kila wiki cha baraza la mawaziri kuwa jamii ya kimataifa haitoi msimamo kamili kuhusu Iran. Alisema Iran haiwezi kusitisha mpango wake wa kinyuklia hadi pale itakapoona jamii ya kimataifa ikichukuwa msimamo mkali zaidi. Netanyahu alisema :
Hayo ndiyo matamshi ya kwanza ya Netanyahu tangu ripoti kutoka kwa Shirika la Kimataifa la Kudhibiti Matumizi ya nishati ya nyuklia kutolewa Alhamisi iliopita. Ripoti hiyo ilisema Iran imeongeza mara mbili uwezo wake wa urutubishaji wa madini ya uranium katika kwianda cha chini ya ardhi cha Fordo, licha ya maazimio ya Baraza la Usalama, vikwazo na matamshi ya Israel kuichukulia hatua ya kijeshi.
Shirika la IAEA pia lilisema kuwa uwezo wake wa kukagua kambi ya kijeshi ya Parchin ambako inashukiwa Iran ilifanya utafiti wa silaha katika siku za nyuma, umeathirika kwa kiasi kikubwa baada ya eneo hilo kusafishwa.
Ripoti hiyo ilionyesha kuwa Iran sasa ina mashine 2,000 ya kurutubisha madini ya uranium, ikilinganishwa na takriban 1,000 ilizokuwa nazi mnamo mwezi Mei, katika kiwanda cha Fordo. Madini yaliyorutubishwa ya Uranium yanaweza kutumika kwa sababu za amani lakini katika viwango vya juu zaidi yanaweza kutumika kwa ajili ya silaha za nyuklia, na maazimio kadhaa ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa yameitaka Iran kusitisha mpango wake wa urutubishaji.
Msemaji wa Ikulu ya Rais nchini Marekani Jay Carney, akizungumza na waandishi habari ndani ya ndege ya rais Air Force One, alisisitiza kuwa hakuna tofauti yoyote baina ya Marekani na Israel linapokuja suala la kuizuia Iran dhidi ya kutengeneza silaha za nyuklia.
Hata hivyo, Netanyahu amesema kuwa ripoti ya IAEA ilithibitisha kile ambacho amekuwa akikisema kwa muda mrefu. Vikwazo vya kimatifa huenda vinauathiri sana uchumi wa Iran, lakini haviizuii Iran kuendelea na mpango wake wa nyuklia.
Iran imefanya awamu kadhaa za mazungumzo na kundi la mataifa yenye nguzu ulimwenguni Uingereza, China, Ufaransa, Urusi na Marekani, lakini mazungumzo hayo hayajazaa matunda yoyote, huku awamu mpya ikitarajiwa katika siku chache zijazo.
Israel, nchi yenye nguvu katika Mashariki ya Kati, imeongoza jumuiya ya kimataifa kuiwekea Iran shinikizo la kusitisha mpango wake wa Kinyuklia. Taifa hilo la Kiyahudi na mataifa mengi ulimwenguni yaanaamini kuwa shughuli za kinyuklia za Iran ni za mpango wa kutengeneza silaha, madai ambayo Iran inakanusha.
Israel inasema inaziona silaha za nyuklia za Iran kuwa ni kitisho kikubwa na mara nyingi imeonya kuchukua hatua zote ikiwa ni pamoja na kuishambulia Iran kijeshi, ili kuizuia nchi hiyo kuwa na silaha za aiana hiyo.
Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri:Mohammed Abdul-Rahman