1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Netanyahu: Mwanasiasa anayesaka kubaki madarakani

Lilian Mtono
24 Machi 2021

Benjamin Netanyahu ameitawala Israel kwa miaka 12 mfululizo kwa sehemu kutokana na kuwashawishi wapiga kura kwama pekee ndio atakayeweza kuliweka taifa hilo katika hali ya usalama. 

Prognose: Netanjahus Likud-Partei gewinnt Wahl in Israel
Picha: Ronen Zvulun/REUTERS

Benjamin Netanyahu ameitawala Israel kwa miaka 12 mfululizo kama waziri mkuu na kufanikiwa kuvunja rekodi ya kiutawala kwa sehemu kutokana na kuwashawishi wapiga kura wengi kwamba yeye ni kiongozi pekee atakayeweza kuliweka taifa hilo la Wayahudi katika hali ya usalama, lakini pia kulipambania kwenye makujwaa ya kimataifa. 

Lakini siku ya Jumanne, Netanyahu mwenye miaka 71 alishindwa kufikia malengo yake kwa kuwa matokeo ya awali ya uchunguzi wa maoni ya waliopiga kura yanaonyesha yeye pamoja na washirika wake wameshindwa kupata idadi inayotakiwa ya viti bungeni kwenye uchaguzi wa nne uliofanyika katika kipindi cha chini ya miaka miwili. Matokeo hayo yalichapishwa na vituo vitatu vikubwa kabisa vya televisheni nchini humo.

Uchunguzi huo unaashiria kwamba manusura huyo wa kisiasa anayetambulika sana kwa jina la Bibi alikuwa anapungukiwa wingi wa kati ya saba ama vinane vinavyotakiwa bungeni miongoni mwa viti 61, ili apewe mamlaka ya kuunda serikali.

Iwapo matokeo hayo yataakisi matokeo ya mwisho, uungwaji mkono wa chama cha Netanyahu cha Likud utakuwa umeshuka kutoka viti 36 kwenye uchaguzi uliopita, licha ya kufanikisha makubaliano ya kihistoria na mataifa manne ya Kiarabuna kampeni kubwa kabisa ulimwenguni ya chanjo dhidi ya virusi vya corona.

Mkataba wa Israel na Umoja wa Falme za Kiarabu una tija?

This browser does not support the audio element.

Sababu moja inayofanya mazingira yake ya kisiasa kusalia tete ni vile anavyoshirikiana na washirika wa muungano wake amao hugubikwa na wingu la kutokuaminiana, amesema msomi mwandamizi katika chuo cha SOAS cha London Collin Shindler. Shindler ambaye ni mwandishi wa kitabu cha The Rise of the Israel Right: from Odessa to Hebron, amesema Netanyahu ana tabia ya kujiundia miungano na washirika ambao ana hakika watakidhi maslahi yake.

Lakini licha ya kuwa ni waziri mkuu wa kwanza kukabiliwa na madai ya ufisadi akiwa mamlakani,upo uwezekano kwamba anaweza kushinda. Hii ni kwa sababu baadhi ya wapiga kura bado wanamuona kama kiongozi anayeweza kuliongoza salama taifa hilo, anasema Shindler.

Netanyahu amewataka Wayahudi kutopuuzia vitisho.

Netanyahu ni mtoto wa kiume wa mwanahistoria aliyekuwa mfuasi thabiti wa kundi la Mazayuni wanaofuata mrengo mkali wa kulia, itikadi ambayo aliirithi na kumjenga kisiasa waziri mkuu huyo.

Alipohutubia kwenye kumbukumbu ya kimataifa ya mauaji ya Halaiki ya Wayahudi, Netanyahu alisema Wayahudi wanatakiwa wakati wote kutovipuuzia vitisho kutoka kwa wale wanaotaka kulivuruga taifa hilo.

Miongoni mwa picha zinazoonyesha wahanga wa mauaji ya halaiki ya Wayahudi Picha: JENS SCHLUETER/AFP

Netanyahu hadi sasa bado hajajihusisha na mazungumzo ya aina yoyote ya amani na Wapalestina, katika wakati ambapo kunashuhudiwa kupanuka kwa ujenzi wa makazi ya kilowezi katika eneo ambalo Israel inalikalia kwa mabavu la Ukingo wa Magharibi.

Mara kwa mara huzungumzia hatari inayoikabili Israel kutoka kwa kundi la Kishia la Hezbollah lililoko nchini Lebanon na aliuita utawala wa Iran kuwa ndio kitisho kikubwa zaidi kwa Wayahudi tangu enzi ya utawala wa Nazi, wa nchini Ujerumani.

Miongoni mwa matukio tata kabisa ya kidiplomasia aliyoyafanya mwanasiasa huyo ni lile la kuhutubia kikao cha pamoja cha baraza la Congress la nchini Marekani bila hata ya kualikwa na aliyekuwa rais wakati huo Barack Obama na kumkosoa kufuatia hatua ya kuingia makubaliano ya nyuklia na Iran.

Netanyahu hujichukulia kama mtetezi mkuu wa Wayahudi dhidi ya majanga, hatua iliyomfanya kuhalalisjha karibu kila kitu ambacho kingemsaidia kumbakisha madarakani, aliandika Obama kwenye kitabu chake cha Kumbukumbu ya urais alichokiita "A Promised Land" ama Nchi ya Ahadi.

Kufuatia chaguzi tatu ambazo hazikutoa mshindi kati ya mwaka 2019 na 2020, Netanyahu alikubali kuunda serikali ya umoja pamoja na mpinzani wake Benny Gantz. Netanyahu alitakiwa kumkabidhi madaraka Gantz baada ya miezi 18, ingawa wataalamu walitabiri mapema kwamba Netanyahu angetafuta namna ya kuuzamisha muungano huo hata kabla ya kumruhusu Gantz kuwa waziri mkuu.

Mashirika: AFPE