1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MichezoNigeria

Nigeria yawacharaza wenyeji Australia 3-2 Kombe la Dunia

27 Julai 2023

Timu ya taifa ya Wanawake ya Nigeria imeishushia kichapo Australia ambao pia ni wenyeji wa michuano ya Kombe la Dunia la Wanawake kwa magoli 3-2 katika mchezo uliotamatika muda mfupi uliopita.

FIFA Fußball Frauen-WM | Australien vs Nigeria | Asisat Oshoala
Nyota wa Nigeria Asisat Oshoala akishangilia baada ya kufunga goli katika mchezo dhidi ya Australia hii leoPicha: James Whitehead/SPP/IMAGO

Timu ya taifa ya wanawake ya Nigeria imeishushia kichapo Australia ambao pia ni wenyeji wa michuano ya Kombe la Dunia la Wanawake kwa magoli 3-2 katika mchezo uliotamatika muda mfupi uliopita.

Soma zaidi: Timu nne za Afrika zinashiriki Kombe la Dunia la Wanawake 2023

Australia walikuwa wa kwanza kupata goli katika dakika za nyongeza kipindi cha kwanza kupitia kwa Emily Van Egmond kabla ya Uchenna Kanu wa Nigeria kusawazisha katika muda huo huo wa nyongeza kipindi cha kwanza.

Hadi wakati wa mapumziko, timu hizo zilikuwa zimetoshana nguvu, japo dakika ya 65 ya mchezo beki wa Nigeria Osinachi Ohale akaipatia Nigeria goli la pili na dakika saba baadaye Asisat Oshoala akapachika goli la tatu na kuifanya ngome ya Nigeria kujihakikishia alama tatu muhimu katika mchezo huo.

Mchezaji wa timu ya taifa ya Wanawake ya Australia Alanna Kennedy akijipiga kifua baada ya kufungwa na Nigeria katika mchezo muhimu wa Kombe la DuniaPicha: Mark Baker/AP pHoto/picture alliance

Ushindi huo umefufua matumaini yaliyoanza kupotea kwa timu za Afrika mara baada ya Zambia kutolewa katika michuano hiyo katika hatua ya makundi.

Nigeria sasa inaongoza kundi B kwa alama 4 sawa na Canada walioko nafasi ya pili huku vibonde Jamhuri ya Ireland wakiwa mkiani. 

Nigeria itakutana na Jamhuri ya Ireland ambayo tayari imeshafungashwa virago hapo jana katika mchezo wao mwisho na iwapo itashinda, basi itajikatia tiketi ya kuingia katika hatua ya 16 bora ya michuano hiyo ya  Kombe la Dunia kwa Wanawake ya 2023.

Canada ambao wako kundi moja na Nigeria watacheza mechi yao ya mwisho dhidi ya Australia na mchezo huo utaamua ni nani atatinga hatua ya 16 bora na nani ataungana na Jamhuri ya Ireland kurejea nyumbani.

Mechi za mwisho za kundi B zitachezwa kwa wakati mmoja na baada ya hapo mbivu na mbichi zitakuwa zimeshajulikana.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW