1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Je, ODM inagawanyika? Taswira mpya ya mgogoro wa uongozi

12 Februari 2026

Mvutano umezuka ndani ya ODM baada ya Edwin Sifuna kuondolewa kama Katibu Mkuu. Je, ni vita ya misimamo kuelekea 2027 au mapambano ya urithi wa uongozi? Mgogoro huu unaweza kubadili mwelekeo wa siasa za chama.

Kenya Nairobi 2022 | Edwin Sifuna bei der Abschlusskundgebung der Azimio la Umoja One Kenya Koalition
Ediwn Sifuna, alietimuliwa ukatibu mkuu wa ODM, anasisitiza kuwa yeye bado ni kiongozi halali wa chama hicho.Picha: Donwilson Odhiambo/ZUMA/picture alliance

Mgogoro unaotikisa chama cha ODM nchini Kenya umechukua sura mpya baada ya uamuzi wa Baraza la Kitaifa kumwondoa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna katika wadhifa wa Katibu Mkuu.

Lakini zaidi ya uamuzi huo, kinachoibuka sasa ni vita ya tafsiri—nani ana mamlaka, nani ana uhalali, na nani anasimamia misingi ya chama?

Katika mkutano uliofanyika Mombasa, ukiongozwa na kinara wa chama Oburu Odinga, Baraza Kuu lilipitisha azimio la kumbandua Sifuna. Nafasi yake imekabidhiwa kwa Catherine Omanyo kama kaimu Katibu Mkuu.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi, hatua hiyo ilitokana na madai ya kukaidi misimamo ya chama. Hata hivyo, haikuchukua muda mrefu kwa uamuzi huo kugeuka kuwa mjadala wa kitaifa.

Aliekuwa kiongozi wa ODM Raila Odinga, enzi za uhai wake, alifanikiwa kukiweka pamoja chama hicho licha ya tofauti za kimtazamo.Picha: Simon Maina/AFP

Sifuna ajibu Mapigo

Akizungumza na wanahabari jijini Nairobi, Sifuna alikanusha uhalali wa hatua hiyo, akisema haikufuata katiba ya chama wala kumpa nafasi ya kujitetea.

Aliambatana na viongozi kadhaa wa ODM, akiwemo Gavana wa Siaya James Orengo na Winnie Odinga, ishara inayotafsiriwa na wachambuzi kama kuonyesha kuwa hana upweke ndani ya chama.

Sifuna anasisitiza kuwa bado ni Katibu Mkuu halali na kwamba mchakato wa kumwondoa ulikuwa na dosari za kisheria.

Chanzo cha mpasuko kinaelezwa kuwa ni tofauti za kimkakati kuhusu mustakabali wa kisiasa wa chama kuelekea uchaguzi wa 2027. Ripoti kutoka vyombo vikuu vya habari nchini zinaonyesha kuwa baadhi ya viongozi wa ODM wanatajwa kutaka msimamo wa upatanisho au ushirikiano na Rais William Ruto.

Sifuna, kwa upande wake, ameweka wazi kuwa hatamuunga mkono Ruto kwa muhula wa pili. Msimamo huo unaonekana kuwagawa viongozi wa ODM kuhusu mwelekeo wa chama baada ya enzi ya Raila Odinga.

Mivutano ya uongozi yatishia kuigawa ODM

17:36

This browser does not support the video element.

Je, ODM yajidhoofisha yenyewe?

Wachambuzi wa siasa wanaonya kuwa mzozo huu unaweza kuathiri mshikamano wa chama. Wapo wanaoona hatua dhidi ya Sifuna kama jaribio la kurekebisha nidhamu ya chama, huku wengine wakihisi ni dalili ya mapambano ya urithi wa uongozi.

Kwa mtazamo wa kisiasa, tukio hili linaweza kumjengea Sifuna taswira ya kiongozi anayesimamia msimamo wake bila kuyumbishwa—jambo linaloweza kuongeza uzito wake kisiasa.

Hivi sasa ODM inakabiliwa na swali muhimu: Je, itafanikiwa kusuluhisha tofauti hizi ndani ya vikao vya chama, au mgawanyiko utaendelea kujidhihirisha hadharani?

Mustakabali wa chama hicho kuelekea 2027 unaweza kuamuliwa si tu na wapinzani wake wa kisiasa, bali pia na jinsi kitakavyoshughulikia mgogoro huu wa ndani.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW