Polisi yakanusha uwepo wa kundi la TFF Tanzania
23 Februari 2026
Taarifa iliyotolewa kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi jijini Dodoma na kusambazwa kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii, imeeleza kuwa jeshi hilo linakanusha madai yanayosambazwa na kikundi cha TFF, kwamba kimetenda matukio kadhaa ya uhalifu.
Aidha, jeshi hilo limesema kuwa kupitia mitandao ya kijamii kumekuwepo na watu wanaohamasisha wananchi kujiingiza katika vitendo vya kihalifu. Baadhi yao wameripotiwa kushawishika na kujiingiza katika uhalifu wa kimtandao, huku wengine wakikamatwa na wengine wakiendelea kutafutwa.
Taarifa hiyo imeongeza kuwa miongoni mwa wanaotuhumiwa kuhamasisha vitendo hivyo ni mtu au watu wanaojitambulisha kwa jina la TFF, wakidai kuwa wanafanya mazoezi porini na tayari wametekeleza matukio kadhaa ya kijinai. Jeshi la Polisi limekanusha vikali madai hayo, likisisitiza kuwa taarifa hizo si za kweli.
Madai ya uwepo wa kundi la TFF yanazua hofu
Kwa mujibu wa jeshi hilo, taarifa hiyo ni kanusho la kiusalama lenye lengo la kuzuia kikundi hicho au watu wanaojihusisha nacho kupata uungwaji mkono au nguvu kupitia mitandao ya kijamii.
Mchambuzi wa masuala ya usalama na kijeshi nchini Tanzania, Malcel Hamdun, anasema taarifa za aina hiyo hazipaswi kupuuzwa. Taarifa ya kuwepo kwa kundi la TFF imezua mijadala miongoni mwa wananchi wa kada mbalimbali, huku baadhi wakieleza kuwa madai ya uwepo wa kundi hilo yanazua hofu na wasiwasi.
Katika siku za hivi karibuni, kwenye mitandao ya kijamii kumejitokeza mtu anayejitambulisha kama kiongozi wa kikundi cha TFF (Tanzania Freedom Fighters), akidai kuwa kikundi chake kipo porini kikifanya mazoezi na kuratibu matukio ambayo Jeshi la Polisi linasema ni ya kijinai.