Maoni ya wahariri.
17 Julai 2008Magazeti mengi ya Ujerumani leo yametoa maoni yao juu ya kutekelezwa hatua ya kubadilishana wafungwa baina ya Israel na Hezbollah.
Mhariri wa gazeti la Dresdener Neueste Nachrichten anasema Israel imemwachia muuaji mkubwa Samir Kuntar. Mhariri huyo anasema kuachiwa kwa gaidi huyo kunathibitisha ni kwa kiasi gani serikali ya Israel inaweza kushinikizwa. Gazeti hilo pia linasema kuwa hatua hiyo pia inathibitisha kuwa Hezbollah ni jumuiya yenye uzito mkubwa kisiasa na kijeshi. Mhariri wa Dresdener Neueste Nachirichten anaeleza katika maoni yake kwamba hakuna anaeweza kuipuuza Hezbollah.
Gazeti la Rhein Neckar pia linazungumzia juu ya hatua hiyo ya kubadilishana wafungwa baina ya Israel na Hezbollah.
Mhariri wa gazeti hilo anauliza vipi itawezekana kuleta amani katika eneo ambapo upande fulani unashingilia kifo kinachotokea katika upande mwingine? Mhariri huyo anasema Mashariki ya Kati ni mahala ambapo watoto wa kipalestina wanageuzwa kuwa watu wenye itikadi kali na Israel. Ni vigumu kwa Israel kukabiliana na uchokozi uliopo sasa bila ya kuchukua hatua za kijeshi.
Lakini gazeti la Rhein Neckar linasema, kuwa siasa ya kutoana macho na meno sasa haifai tena.Kinachotakiwa ni sera ya maridhiano kama jinsi ilivyofanyika nchini Afrika Kusini na Ireland.
Gazeti la Badische Zeitung linauliza jee nani ni mshindi katika mgogoro wa Mashariki ya Kati ?
Au nani ameshindwa katika mgogoro huo? Gazeti hilo linasema pande zote zimeondoka na majeraha usoni. Yumkini kiongozi wa Hezbollah Hassan Nasrallah anashingilia ushindi kutokana na kuachiwa wafungwa wa Hezbollah. Lakini ukweli ni kwamba kiongozi huyo anatoka nje ya maficho yake kwa nadra sana. Mhariri wa gazeti hilo pia anakumbusha juu ya walebanon 1200 waliouawa katika vita vya mwaka 2006. Gazeti la Badische Zeitung pia linasema kwamba Israel nayo ilipata funzo kubwa kutokana na vita hivyo. Mhariri anahoji kuwa haikuwa lazima kwa Israel kwenda vitani ati kwa sababu ya askari wake kuvamiwa mpakani na wapiganaji wa Hezbollah.