1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Putin asema hawezi kushindwa na Ukraine

9 Februari 2024

Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema kwamba nchi za Magharibi zinapaswa kuelewa kuwa haitawezekana kuishinda Urusi katika vita vya nchini Ukraine.

Putin Carlson
Mahojiano kati ya rais wa Urusi Vladimir Putin na mwanahabari Tucker Carlson.Picha: Tucker Carlson Network/Zuma Press Wire/dpa/picture alliance

Putin ameyasema hayo katika mahojiano yaliyodumu kwa saa mbili na mtangazaji wa zamani wa Fox News wa Marekani Tucker Carlson yaliiyorekodiwa siku ya Jumanne mjini Moscow. Mahojiano haya yanajiri kabla ya maadhimisho ya miaka miwili ya uvamizi wa Urusi nchini Ukraine.

Soma pia: Urusi, Ukraine zashambuliana kwa droni usiku kucha

Kuhusu mwanahabari wa Wallk Street Evan Gershkovich Putin amesema makubaliano ya kumuachia yanaweza kufikiwa lakini "Kuna masharti fulani yanajadiliwa kupitia njia maalum,"  huku akisisitiza kwamba mwandishi huyo ni jasusi jambo ambalo Jarida na serikali ya Marekani linakanusha vikali.

Putin alitumia mahojiano hayo kutuma ujumbe kwa Bunge la Marekani, ambalo tayari wanachama wa Republican wanazidi kusitasita katika kuendelea kuiunga mkono Ukraine kwa silaha na misaada mingine ya kijeshi akisema ikiwa kweli wanataka mapigano yasitishwe basi waache kusambaza silaha.

Alipoulizwa kama Moscow inafikiria kuvamia nchi nyingine katika kanda hiyo, Putin alisema hana mpango wa kuivamia Poland, Latvia ama eneo jingine lolote na wala hana nia ya kuvipanua vita vyake nchini Ukraine.

 

Uwanja wa mapambano

Jeshi la Ukraine likitayarisha ndege isiyo na rubani.Picha: Inna Varenytsia/REUTERS

Urusi na Ukraine zilirushiana jumla ya ndege 35 zisizo na rubani usiku kucha, huku pande zote mbili zikifanya majaribio ya kuvunja mkwamo katika vita hivyo.

Soma pia: Zelensky amfuta kazi mkuu wa majeshi

Wizara ya Ulinzi ya Urusi imesema jeshi lake lilidungua droni 19 za Ukraine katika mikoa minne tofauti na Bahari Nyeusi, huku Ukraine ikisema ilidungua droni 10 kati ya 16 zilizorushwa na Urusi.

Katika miezi ya karibuni Ukraine imeongeza mashambulizi yake ya droni dhidi ya Urusi, yakilenga hasa mikoa ya mpakani, lakini pia mji mkuu Moscow, na mji wa kaskazini wa Saint Petersburg.

Pia imeshambulia vituo kadhaa vya nishati, katika kile ambacho Kyiv, imetaja kama kisasi cha "haki" kwa mashambulizi ya Moscow yanayolenga vituo vya umeme kote nchini Ukraine.

Ukraine imekuwa chini ya mashambulizi ya mara kwa mara ya angani yanayofanywa na majeshi ya Urusi kwa karibu miaka miwili. Maelfu ya watu wameuawa katika mashambulizi hayo.

Soma pia: Watu 28 wameuwawa katika shambulio lililofanywa na Ukraine

Ukraine imetoa wito kwa washirika wake wa nchi za Magharibi juu ya kuimarishwa mifumo yake ya ulinzi.

 

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW