1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIsrael

Raia wa kigeni waanza kuondoka Gaza kuelekea Misri

Sylvia Mwehozi
1 Novemba 2023

Raia wa kigeni ambao walikuwa wamekwama Ukanda wa Gaza wameanza kuondoka hii leo baada ya Misri kukifungua kivuko cha Rafah ikiwa ni mara ya kwanza tangu vita vya Israel dhidi ya Hamas vilipoanza mnamo Oktoba 7.

Rafah | Misri
Watu wakipita lango la kuingia kwenye mpaka wa Rafah kuelekea Misri katika Ukanda wa Gaza kusiniPicha: Mohammed Abed/AFP/Getty Images

Kwa mujibu wa chanzo kimoja cha usalama kutoka Misri ni kwamba raia wa kigeni wapatao 500 watavuka kivuko cha Rafah kutoka Gaza na kuingia Misri leo Jumatano. Picha za moja kwa moja kutoka eneo hilo zimeonyesha umati mkubwa wa watu wakisubiri upande wa Palestina kwenye kivuko hicho wakikadiriwa kufikia watu 200.

Ingawa malori zaidi ya 200 yaliyokuwa yamebeba misaada ya kiutuyaliruhusiwa kuingia Gaza kutokea Misri, hakuna watu ambao waliruhusiwa kuondoka Gaza. Serikali za kigeni zinasema raia wa kutoka takribani nchi 44 pamoja na mashirika 28 yakiwemo yale ya Umoja wa Mataifa walikuwa wakiishi Ukanda wa Gaza ambako wakaazi wake wapatao milioni 2.3 wamekabiliwa na mashambulizi ya Israel kwa zaidi ya wiki tatu, katika hatua ya kujibu shambulizi la Hamas la Oktoba 7.

Idadi kubwa ya watu wallo na pasi za kigeni za kusafiria waliokuwa wamekwama huko Gaza wakianza kuondoka katika eneo lililokumbwa na vita la PalestinaPicha: Mohammed Abed/AFP/Getty Images

Mbali na raia hao wa kigeni, pia Wapalestina wapatao 90 waliojeruhiwa vibaya au wako katika hali mbaya sana ya kuumwa wanatarajia kuvuka na kupatiwa matibabu Misri. Idadi kubwa ya magari ya kubeba wagonjwa imeshuhudiwa ikisubiri katika kivuko hicho. Misri pia imesema itajenga kituo cha muda cha matibabu cha kuwapokea watu waliojeruhiwa katika mji wa Sheikh Zuweid ambao upo kilometa 15 kutoka Rafah.

Soma pia: Israel na Misri zaruhusu misaada ya kibinaadamu kupelekwa Gaza

Jeshi la Israel limesema kwamba askari wake 11 wameuawa katika mapigano ya ardhini ndani ya Gaza siku ya Jumanne, na kufanya idadi jumla ya wanajeshi waliouawa tangu Oktoba 7 kufikia 326. Askari wengine wawili walijeruhiwa vibaya katika mapigano ya Jumanne huku jeshi la Israel likidai kuyalenga zaidi ya maeneo 11,000 ya wanamgambo tangu ilipoanza vita vyake dhidi ya Hamas. Katika hotuba yake kwa taifa Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ameahidi "ushindi" dhidi ya Hamas licha ya "athari za kuumiza."

"Tuko kwenye vita vikali. Vitakuwa ni vita vya muda mrefu. Tumekuwa na mafanikio makubwa lakini pia hasara chungu nzima. Wanajeshi wetu wameanguka katika vita vya haki kabisa, vita dhidi ya nyumba zetu. Na ninaahidi kwa raia wote wa Israeli tutafanya kazi hiyo. Tutasonga mbele hadi ushindi," alisema Netanyahu. 

Magari yakisubiri nje ya lango la mpaka wa Rafah na Misri katika Ukanda wa Gaza kusini.Picha: Mohammed Abed/AFP/Getty Images

Hayo yakiendelea, Bolivia ilitangaza hapo jana kwamba inavunja uhusiano wa kidiplomasia na Israel. Katika tangazo lake  naibu waziri wa mambo ya nje wa Bolivia Freddy Mamani alisema wamechukua hatua hiyo katika "kukataa na kulaani mashambulizi makali ya kijeshi na yasiyo na uwiano yanayotekelezwa katika Ukanda wa Gaza na Israel." Baadae waziri mwingine katika ofisi ya rais wa Bolivia Maria Nela Prada, naye pia alitangaza kwamba watapeleka misaada ya kiutu huko Gaza.

Janga la kiafya: Gaza kutumbukia janga la kiafya - WHO

Israel tayari imeukosoa uamuzi wa Bolivia wa kukata uhusiano wa kidiplomasia ikisema ni "kukubali ugaidi na kujisalimisha kwa utawala wa Iran". Wizara ya mambo ya kigeni ya Israel imeongeza katika taarifa hiyo kwamba "kwa kuchukua uamuzi huo serikali ya Bolivia inajifungamanisha na kundi la kigaidi la Hamas."

Bolivia limekuwa taifa la kwanza la Amerika ya Kusini kuvunja uhusiano na Israel tangu mzozo huo ulipozuka upya na kundi la Hamas.

 

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW